Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nikushukuru kwa kunipa fursa hii ili niweze kuhitimisha hoja niliyoitoa mnamo tarehe 10 Juni mwaka huu na kabla sijaanza kuhitimisha nianze kwanza kwa kutoa shukrani na pongezi kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa imani kubwa anayoijenga kwa wananchi wa Tanzania pamoja na Jumuiya za Kimataifa, pamoja na maelekezo yake ya mara kwa mara yanayotuwezesha tutekeleza majukumu yetu kikamilifu, hakika kazi zake anazozifanya zinafanya kazi yetu pia iwe nyepesi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili nitumie fursa hii pia kukushukuru wewe mwenyewe Mheshimiwa Job Yustino Ndugai, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson - Naibu Spika pamoja na Wenyeviti kwa kuendesha kwa weledi mkubwa mjadala huu muhimu kwa maendeleo ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nitoe pongezi na shukrani kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu Bunge ya Bajeti Mheshimiwa Sillo Daniel Baran, Mbunge wa Babati Vijijini; Makamu Mwenyekiti Mheshimiwa Omari Mohamed Kigua, Mbunge wa Kilindi pamoja na Kamati nzima ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti ambayo wametupa ushirikiano mzuri na wa hali ya juu ambao umewezesha kazi yetu hii kuwa ya ufanisi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda pia nitoe shukrani zangu kwa Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri la Muungano wa Tanzania waliochangia kwa maandishi, kwa kuongea na wale waliotoa ushauri wao katika kuonana na sisi ana kwa ana, kwani wamewezesha sana shughuli hii iweze kukamilika kikamilifu na niwaombe wananchi wa Tanzania watambue tu kwamba Wabunge wao wametoa michango yenye maana kubwa sana kwa Taifa letu pamoja na kwamba huenda nikawataja wachache, lakini wapiga kura wao wote watambue kwamba Wabunge wao wamechangia kwa hoja za msingi na zenye tija kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni vile tu kwa wingi wao sitaweza kumtaja mmoja mmoja, kwa hiyo hata kama Mbunge wao hatatajwa watambue kwamba wamechangia kwa hoja makini sana ni wingi wao tu hatuwezi kuwataja wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jumla ya Wabunge 209 wamechangia na kati ya hao 206 wamechangia kwa kuongea na Wabunge watatu wamechangia kwa maandishi na kama nilivyotangulia kusema wengine wametupa ushauri wao kwa kuongea/kwa kujadiliana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kutoa ufafanuzi wa hoja zilizojitokeza; kati ya hoja ambazo kwenye mjadala zimejitokeza kwa kiwango kikubwa zilikuwa zinahusisha maeneo yale ambayo tuliweka tozo mpya.

Mheshimiwa Spika, la kwanza niwapongeze Wabunge kwa kuelewa hoja ya Serikali na umuhimu wa jambo lile ambalo tulikuwa tunaongea lugha moja ambalo kwa kiwango kikubwa Wabunge wenyewe walikuwa wameibua kwamba tunahitaji tuangalie kwa jicho la tofauti katika matatizo yanayojitokeza katika sekta zetu za muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sekta ya kwanza ambayo tuliangalia kwa umakini mkubwa ilikuwa ni sehemu ya TARURA, barabara zetu na pili tulikuwa tumeangalia kuhusu upande wa maji, la tatu tulikuwa tumeangalia kuhusu upande wa elimu, la nne tulikuwa tumeangalia upande wa afya, miundombinu yake pamoja na mwelekeo wa kwenda kwenye universal health care na kipengele cha mwisho tulikuwa tumeongelea kuhusu miradi ya kimkakati ambayo ni miradi urithi kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maeneo ambayo tulikuwa tumependekeza ambayo kwa kiwango kikubwa Waheshimiwa Wabunge pamoja na Watanzania walitamani kupata ufafanuzi, moja ya eneo ilikuwa kuhusu makato ya kwenye simu upande wa muda wa maongezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo hili kwa kiwango fulani lilikuwa halijaeleweka kile ambacho tulikuwa tunakimaanisha, kuna wale ambao walikuwa wanadhania makato haya yanaenda kukatwa kwa idadi ya siku kwenye mwezi, kwa maana kwamba itahesabiwa kuanzia tarehe ya kwanza ya mwezi mpaka tarehe ya mwisho na kama hukuweka salio siku ukiweka unahesabiwa siku zote katika mwezi husika.

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo ilikuwa inafananishwa kama ile ya nipige tafu ambayo kama jana hukuweka ama jana ulitumia kwa kukopa basi siku ukiweka inatakiwa ikatwe kwanza ile ambayo siku hiyo ilishapita. La hasha, sisi tulichopendekeza ni kwamba tumechukua takwimu za watumiaji wa simu, tukaweka makundi yao, kuna watumiaji wasiopungua milioni nane kwa viwango vya mwanzo ambao wana matumizi yao yasiozidi shilingi 1,000 inaenda inakuwa mpaka inafika wale wanaotumia shilingi 100,000 na kuendelea ambao wenyewe si wengi sana wako kwenye 60,000 naa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tulichoweka kwa wale watumiaji wanaotumia viwango vya chini kwa mfano anayetumia shilingi 1,000 na kwenda chini yeye atakatwa shilingi tano, na hiyo shilingi tano atakatwa pale alipoweka tu, kwa wale wanaotumia shilingi 7,500 hadi shilingi 10,000 atakatwa shilingi 76. Kwa wale wanaotumia shilingi 10,000 hadi shilingi 25,000 maana yake huyu inaweza ikawa ni mtu anayejiunga muda wa maongezi wa mwezi mzima kwamba ameweka kifurushi chake cha mwezi mzima kina range shilingi 10,000 mpaka shilingi 25,000; chukulia ni shilingi 25,000 kwamba ndicho anachojiunga nacho anakatwa shilingi 112; maana yake ni kwamba mwezi mzima amekatwa shilingi 112. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama anajiunga kwa shilingi 50,000 kwa mfano nani Halotel wana bundle linaitwa Tanzanite ambalo ukijiunga unaongea kwa mwezi mzima, chukulia ni shilingi 50,000; kwa hiyo kwa mwezi mzima anakuwa amekatwa shilingi 186; ni tofauti na ile hesabu tuliyokuwa tunapiga kwamba ni 200 kwa siku maana yake kwa mwezi ni shilingi 6,000 unaona hiyo tofauti kati ya shilingi 6,000 ambayo ilikuwa inatisha na shilingi 186 kwa mtu anayetumia shilingi 50,000.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema siku naweka hoja hapa mezani kwamba kwa kweli nachukia kuwapa Watanzania mzigo na kwa kweli nawahurumia Watanzania, lakini nikasema nawahurumia zaidi wanaojifungulia vichakani, kwa mtu anayeweza kutumia shilingi 50,000 kwa mazungumzo akichangia shilingi 180 ili kuokoa maisha ya mama zetu kuna shida gani kwa mwezi mzima! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mtu ambaye anaweza kutumia shilingi 25,000 ndio ni Mtanzania wa kawaida, akatumia shilingi 25,000 kwenye mazungumzo ndio ni Mtanzania na shilingi 100 ni kubwa, tukimuongezea kwenye matumizi yake ndio ni kubwa, mzigo, tunamhurumia, lakini shilingi 100 hiyo ikasaidia kupatikana vifaa tiba hospitalini, shilingi mia hiyo kwa mtu anayeweza kuongea kwa shilingi 25,000 kwa mwezi kwenye simu akasaidia tukapeleka vijana 21,000 waliokosa mkopo wa familia za kimaskini kuna shida gani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo niendelee kutoa rai kwamba nchi hii itajengwa na Watanzania wenyewe, ni lazima tubebe majukumu hayo kama wazazi, lazima tubebe majukumu hayo kama Watanzania kwa sababu majukumu hayo ni yetu. Hata anayetumia shilingi 1,000 mpaka shilingi 5,000 katikati mle kuna shilingi 1,000 mpaka shilingi 2,500 anapoweka akichangia shilingi 10 halafu fedha ile ikaenda ikatusaidia upatikaji wa maji, kuna watoto wadogo wanabakwa wakiwa wanatafuta maji usiku ipo hiyo na sasa hivi imeongezeka na shida ya corona inayotuhitaji tuwane kwa hiyo kuna maisha yatapotea tusipokuwa na maji kwa jambo dogo tu la kunawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nakumbuka vizuri haya matatizo ya maji tulipokuwa kule vijijini ilikuwa ikifika mwezi wa sita na kuendelea mpaka Krismas mnaanza kusoma nusu siku tu ili muende kutafuta maji. Sasa kwa umri wa nchi yetu hivi si vitu vya kuviruhusu viendelee, vitakuwa vinapingana na hatua ya maendeleo tuliyoyafikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi niliwahi kuumia hiki kidole tukiwa tunachimba maji, hakijawahi kupata shape, hakijawahi kurudi kwenye hali yake ya kawaida, shida ya maji bado ni tatizo katika kila eneo. Kwa hiyo, hili na lenyewe tuliona tuifanye hivyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo huu ndio mtiririko, tutaanza na shilingi tano na pale ni mtu anapoweka na itaenda inakuwa kufuatana na matumizi yake na mpaka inaenda hiyo shilingi 222 kwa wale ambao watatumia shilingi 100,000 na kuendelea na hili si jambo la kila siku, ni pale mtu anapotumia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukirudi upande wa miamala; kwenye miamala tulienda kuzingatia hivyo hivyo kwamba nchi yetu ina matatizo, pamoja na jitihada kubwa ambazo zimefanyika, lakini kila hatua ya maendeleo unayoifanya itakuletea changamoto zaidi; ndio utaratibu wa maendeleo ulivyo, kila hatua ya maendeleo unayoifanya ndio inakuletea changamoto zaidi, kwa mfano, tunapoongelea kila kijiji kiwe na umeme, kila mtaa uwe na umeme, kila familia iwe na umeme, umeme ule sio nguzo na nyaya za umeme, tunahitaji chanzo cha kufua umeme kitakachotosheleza mahitaji ya nyumba kwa nyumba kwa nchi nzima kuwa na umeme. Vinginevyo tukiwekeza tu kwenye kusambaza nguzo yatakuwa makao ya kunguru tu wanapandapanda mmewaongezea miti, lazima tuwe na chanzo cha uhakika kitakachofua umeme kiweze kusambaza umeme katika maeneo hayo ndio maana tunasema kila familia lazima iwe na umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo tuna miradi ya kimkakati ambayo na yenyewe tukasema lazima tupate fedha na tukasema kama tutatafuta fedha kwa njia ya mikopo tu, tuna mzigo mkubwa Waheshimiwa Wabunge kwenye bwawa la umeme peke yake kwa muda huu ili likamilike mpaka mwisho zimeshatumika trilioni kama mbili hivi bado tuna mzigo karibu trilioni nne.

Mheshimiwa Spika, ukitoka hapo ukiweka na reli, reli sio njia moja tu tunataka kuijenga, hii njia ambayo tunaondoka nayo, huu ni mwanzo kama alivyosema Waziri mwenye sekta, tuna na reli zingine Kusini, Kaskazini pamoja na yale matawi tukishafika Tabora mtawanyiko wake ule, ukipiga hesabu yake yote hiyo ni karibu dola bilioni 10 ambayo ni zaidi ya shilingi trilioni 22.

Mheshimiwa Spika, sasa fedha za aina hiyo ukisema tu uende ukakope zote tena uikamilishe kwa muda mfupi maana yake ni kwamba kwanza masharti tutakayopata hayatakuwa rafiki, lakini mbili mzigo utakalolibebesha Taifa utakuwa ni mzigo wa roho mbaya kwamba sisi tukope tu watakuja kulipa ambao hawajazaliwa, tutakuwa tunafanya kitendo ambacho vizazi vijavyo vitalaumu kizazi cha leo kwamba kama hawakutaka kujenga reli kwa nini wasingeacha tu tuje tujenge wenyewe uende tungekuja kukopa kwa masharti ambayo ni nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini sisi tumeona ni vyema tukafanya utaratibu wa kupata fedha kiasi tutapeleka kule wakati tunasubiri credit rating pamoja na taratibu zingine, lakini kwa wakati huo huo tuwe tunatafuta mikopo yenye masharti nafuu ambayo haitaipa mzigo mkubwa wa deni kwa Taifa letu ambao pia unaweza ukatusababisha tukaingia kwenye sifa mbaya za nchi zilizokopa kupita uwezo wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hicho ndicho ambacho tulikizingatia kwa upande huo wa miamala na mimi niwaombe Watanzania kama nilivyosema tunazingatia mambo yanayotukabili mbele yetu na ndicho tulichofanya kuamua tukasema ni vyema tukafanya hivyo. Na kwa nini tuliona tufanye hivyo; mfumo wa kodi wa kwetu ulivyo ile tax base ilivyo mpaka hivi tunavyopanga bajeti ya leo ukiiondoa indirect taxes zile kodi ambazo kila mtu anaguswa kwa matumizi ya bidhaa wale ambao wameandikishwa huo mzigo unaangukia kwa watu wachache.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano mpaka sasa tunavyoonge walipa kodi wakubwa ni 504; ukienda walipa kodi walioandikishwa ni 3,162,000; sasa kama una walipakodi wakubwa 504 na walioandikishwa milioni tatu; una miradi inayohitaji shilingi trilioni 20 na kuendelea; karibu shilingi trilioni 24 hiyo hatujataja miradi mingine ambayo na yenyewe ni mikubwa, miradi kama ya madaraja, barabara za kuunganisha, hapo hatujaenda kwenye hizi za kimkakati tunazosema za kwenye vijiji vyetu ambavyo ni za muhimu sana, unawezaje kupeleka malipo haya yote yaangukie kwa hawa watu niliowataja hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukasema kazi kujenga nchi yetu lazima ifanywe na Watanzania wote na Watanzania wajivunie kuijenga nchi yao. Kila Mtanzania anapoona jambo la maendeleo limefanyika ajivunie kwamba na mimi nimeshiriki, tukasema hii na yenyewe tushirikishe kwa upana wao, ndipo tulipoona tuanze kugusa awepo wa shilingi 10, shilingi 16, yupo wa shilingi 50, yupo wa shilingi 25, yupo wa shilingi 125, ukienda wa shilingi 30,000 ni shilingi 1,000 ukiienda shilingi 40,000 ni shilingi 1,500; ikaenda mpaka yule wa shilingi milioni tatu na kuendelea milioni tano, milioni 20, milioni 15 na kuendelea tukasema kwa kazi tuliyonayo kama Taifa kama unaweza ukawa na ukwasi wa milioni 15 tukichukua shilingi 10,000 kwako halafu ukajivunia kujenga nchi yako, kuna ubaya gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unaingia kwenye rekodi ya kujenga nchi yako, unaingia kwenye rekodi ya kujenga nchi yako, sisi wengine huwa tunajivunia sana lift hizi kwamba inapojengwa reli unaingia kwenye kumbukumbu kwamba reli inajengwa ilikuwa umri wetu kama wazee wanavyotuambia kwamba wakati vita vya Kagera vinapigana mimi nilipeleka ng’ombe, wanajivunia wakati wa vita vya Iddi Amini mimi nilipeleka ng’ombe, mwingine anasema mimi nilipeleka mbuzi, wanajivunia wazee wetu,

hawakuwa matajiri wakubwa kihivyo, walikuwa matajiri wa moyo kwamba mimi nilipeleka mbuzi wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wengine walikuwa na mabasi yalikuwa yanashusha abiria wa biashara wanabeba wanajeshi waende kupigana, ana-sacrifice fedha ambayo angeipata kwa biashara yake anapeleka basi liende kwenye ile vita. Sasa hivi hatuna vita za kiuvamizi, vita zilizosalia kwenye nchi zinazoendelea ni vita za kiuchumi kujenga mataifa yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lazima tuwe na moyo wa aina hiyo kwa sababu hii nchi lazima iende na sisi tujivunie kwamba hapa lilifanyika hili tukiwepo, lilifanyika na hili tukiwepo, hebu fikirieni vijana wa rika langu, wakubwa zetu na wadogo zetu mnaofuatia, siku ikitokea katika kizazi chetu tukajenga reli zote za Kusini huku Mtwara kwenda kwenye maeneo ya uzalishaji, tukajenga Kaskazini huku kote, tukajenga na hizi kubwa tukasema hizi zilijengwa katika kizazi hiki, na Rais aliyekuwepo alikuwa Mama yetu Samia Suluhu, hili ni jambo la heri kwa kila Mtanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivyo ndivyo tulivyowaza wenzenu, tukasema hii kazi lazima tuibebe wote, hivyo ndivyo tulivyofikia katika uamuzi huo na mimi naamini Watanzania tukikubaliana na mwenendo huu tutapiga hatua ambayo Tanzania itarudisha ile sifa iliyokuwa mbele inatajwa na kila mtu wakati wa ukombozi wa Kusini mwa Afrika. (Makofi)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, makofi hayo hayatoshi kwa kweli, kabisa. (Makofi)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, sasa tunachopendekeza, baada ya kuwa tumepata yale mapato nini tunapendekeza; tunapendekeza tupeleke shilingi bilioni 322 ziende kwenye maeneo yetu ambayo hayapitiki, hayana barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulishapitisha bajeti ya TARURA karibu shilingi bilioni 400 na sehemu, kama mnavyokumbuka. Zile zitafanya ile kazi ya kawaida ya spotting na periodic maintenance kama ambavyo zilikuwa zinafanyika na zingine mgao ulishapita. Tunapendekeza tuongeze ziada ya zile shilingi bilioni 400 na bahati nzuri hiki chanzo kinakwenda moja kwa moja kwenye mfuko. Kwa hiyo, tutakapotumia zaidi maana yake makadirio haya yanaweza yakazidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, twende tukafungue maeneo ambayo hayapitiki. Mijini na vijijini tuna maeneo mpaka karne hii, nilisema na siku ile tuna eneo unakuta kijiji kina shule ya msingi, taasisi ya Serikali, ina zahanati, lakini hakuna gari inaweza ikafika pale. Hali ya aina hiyo haiendani na umri wa nchi yetu na heshima ya kiuchumi ambayo nchi yetu imetambulika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata Jiji kubwa kama Dar es Salaam, nilikuwa naongea na Mbunge wa Kibamba akasema hata kwake kuna maeneo ambayo kwenye ramani yanaonekana kabisa yana mitaa, lakini hayapitiki. Sasa mtu anaishi Dar es Salaam, jiji kubwa ambalo linatambulika, lina mpaka flyovers halafu eneo lingine mlemle hata pikipiki haipiti, haya hayaendani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI alisema jana kwamba tunaondoa miradi ile ya DMDP pamoja na TACTIC, muielewe vizuri. Tulichokuwa tunasema fedha hizi siyo za kwenda kwenye mapambo yale, kwamba wengine waendelee kubandika na kubandua halafu kwenye eneo lilelile pawe pana watu ambao hawajawahi kupata kitu kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ile miradi itakuja, kama alivyosema Waziri, lakini alichomaanisha kwamba kuna maeneo yapo hayajafunguka kabisa, yapewe kipaumbele na haya yanakwenda kwenye majimbo yenu huko huko; awe Mbunge wa Dar es Salaam ana maeneo ya pale mjini na pembezoni; awe Mbunge wa kwenye miji ile 45, ana maeneo ya mjini na mle pembezoni. Kwa hiyo, hiki ndicho alichosema Waziri wa TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na tunakwenda kupata, ukiangalia kwenye hesabu, Wabunge na hapo ndiyo wapiga kura wenu waone kwamba walileta majembe kweli kweli; mnavyoondoka hapa kila mmoja ataondoka na siyo chini ya shilingi bilioni moja, inakwenda kwenye barabara hizo. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, mkifuatilia hapa mtakuta kuna wakati TARURA ilikuwa inapata shilingi milioni 30, majimbo mengine yalikuwa yanapita kapa, mwaka mzima unapita. Sasa waambie wananchi wako kwa jinsi Mbunge ulivyo mjanja sasa hivi, umeishauri Serikali sikivu na ulivyopaza sauti mama yetu akasikia kilio chenu, na akasikia kilio cha wananchi wote, unakwenda kuondoka na siyo chini ya shilingi bilioni moja, iende kwenye kufungua barabara ambazo hazijawahi kupitika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na tukienda na utaratibu huu mwaka wa kwanza, wa pili, wa tatu tukaendelea nao kama walivyoanza TANROADS, walianza na kufungua mkoa mmoja mmoja na sisi tukianza hivyo hivyo tukafungua kijiji kwa kijiji, mtaa kwa mtaa, tutafika wakati hatutaongelea changarawe mitaa yote, tutaanza sasa kuwaza makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vijana wengine wanadhani zile barabara kubwa za TANROADS za lami zinazounganisha mikoa zilikuwa hivyo hivyo, hawakusafiria yale mabasi yenye carrier juu. Mkipita mnavyofika mkishuka abiria na kondakta wote mko sawa, lakini tulianza na utaratibu huu huu na ndiyo maana tunasema Mheshimiwa Dkt. Magufuli, Mungu amrehemu kule aliko, wakiwa wanakwenda na utaratibu huo wa mfuko na kuanza hatua kwa hata wakaenda, sasa hivi tunaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa nchi ni kama ujenzi wa nyumba, kuna anayejenga msingi, kuna anayejenga kuta, kuta anayepaua, kuna anayeweka marumaru. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tunapendekeza na tumeongea na wenzetu wa Wizara ya Elimu, Mheshimiwa Profesa Ndalichako, tumeongea naye na wataalam wake na wametuambia wanafunzi 11,000 waliokosa mikopo mwaka jana na wa mwaka huu walikadiriwa kama 10,000; ni kama 21,000 plus, mahitaji ya fedha ni shilingi bilioni 70. Kwenye shilingi bilioni 500 ambayo tulishapeleka tunaongeza shilingi bilioni 70 ziende ziwapeleke watoto wa mwaka jana…(Makofi)

MBUNGE FULANI: Haleluya!

SPIKA: Mheshimiwa Waziri wa Fedha, hapa hujaeleweka, hebu rudia kidogo, maana yake Wabunge wengine naona kama hawajaipata hii vizuri. (Makofi)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, mwaka jana walikosa mikopo takribani watoto 11,000 wale ambao wana admission, wamepokelewa na vyuo kwamba wana sifa za kuingia vyuoni, lakini walikosa masomo kwa sababu walikosa mkopo na wazazi wao hawana uwezo, wengine hawana wazazi na wakabaki majumbani 11,000. Na wanakadiriwa mwaka huu tena wangekosa 10,000 na kuendelea.

Mheshimiwa Spika, kwenye familia zetu mtoto ambaye amefaulu mtihani huwa inakuwa faraja ya familia na ukoo mzima. Ikitokea amekosa mkopo, siyo fedha ya msaada, mkopo, inaleta majonzi kwenye familia na ukoo mzima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunapendekeza kuongeza kwenye bilioni tulizopitisha kwenye Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, shilingi bilioni takribani 500, tunaongeza shilingi bilioni 70 ambazo zinakwenda sambamba kuwapeleka watoto wote. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Haleluya!

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Ummy Nderiananga aliongelea upande wa wanafunzi wenye ulemavu; tumepokea mapendekezo yako na tunaendelea kuyafanyia kazi Kiserikali, tutajua kwenye utekelezaji wake kuhusu wanafunzi wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunapendekeza kwa upande wa maboma ya elimu, kama tusipopanga kuanzia sasa kule tunakokwenda watoto wetu watapata sifa za kuingia shuleni, lakini hawatakwenda kwa sababu kuanzia mwaka kesho tunakwenda kupata toleo la kwanza la wale wanafunzi walioandikishwa kwa elimu bila malipo shule ya msingi, darasa la kwanza, ndiyo wanakwenda kumaliza darasa la saba na wanatakiwa waanze kidato cha kwanza.

Mheshimiwa Spika, tusipojipanga kwenye miundombinu kuanzia sasa takwimu zinaonesha tutakuwa na uhitaji wa vyumba vya madarasa wa kiwango cha juu sana na hatutaweza kufanya kwa muda mfupi.

Mheshimiwa Spika, utakumbuka, bahati nzuri wewe ni kaka yetu tulio wengi hapa, utakumbuka zamani kwa ajili tu ya kukosekana miundombinu watu ni hawa hawa, Watanzania ni hawahawa na akili zao ni hizihizi, lakini ilikuwa inatokea kijiji kizima, darasa lenye watu sitini, mia, inatoka kapa. Mnaambiwa tu wamefaulu 50 lakini hawakuchaguliwa, maana yake wakichaguliwa wanakwenda wapi, ndivyo ilivyokuwa. Mimi nakumbuka hata Mazengo tulikwenda watano.

Mheshimiwa Spika, lakini sasa hivi tulivyojenga shule kwenye kila kata mmeona wanaobaki wameendelea kuwa kidogo sana. Maana yake nini; wana pa kwenda na kule kule wanakokwenda ili muone kwamba akili wanazo, wanapata division one kule kule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kuna rika hapa la enzi ya wamefaulu ila hawakuchaguliwa, kuna rika la watu wana akili sana na wangelitumikia Taifa, hawakwenda kwa sababu ya nafasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na hata sasa kuna baadhi ya mikoa kwa sababu bado tunagawanya chumba kimoja tunaweka ubao katikati, watoto wengine waangalie ubao mmoja wengine waangalie mwingine; kwa hiyo, mikoa ile ikitokea ametokea mtoro amekwenda kuchunga kama tulivyokuwa tunachunga wengine, hata hawahangaiki kumtafuta kwa sababu wanajua ametupunguzia na kero ya madawati huyu, ametupunguzia na mbanano. Tumefanya suala la elimu liwe la kuviziana kwa sababu miundombinu haitoshi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi kama Wizara tunaoshughulika na mipango tunaona hili jambo tunaweza tusilimalize mara moja, lakini ni vyema tukaanza kupanga haya mambo tunakokwenda. Uamuzi wa maeneo mengi tunaufanya kwa kuviziana kufuatana na miundombinu iliyopo na ndiyo maana familia tulizokuwa tumezaliwa watoto kumi au 11 hatukuwa tunafanya birthday, utakumbuka birthdays ngapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hata kwenye masuala ya miundombinu, uamuzi wa kupeleka watoto shuleni miundombinu inachangia. Hata haya mambo tumebishana ya waliopata ujauzito warudi ama wasirudi, unaweza ukakuta uamuzi unakuwa shaped na wakirudi wanakwenda wapi. Tunafanya kuviziana kwa sababu ya miundombinu.

Mheshimiwa Spika, lakini suala la elimu linatakiwa liwe wazi tu, hata ukitaka kusoma lini wewe soma, si tunataka upate akili, upate uelewa? Mbona elimu ya watu wazima tuliwasomesha wazee, tulisomesha na wana wajukuu. Kwa hiyo, tumeona lazima tushughulike na miundombinu.

Mheshimiwa Spika, nini tunachopendekeza; tunapendekeza tuanze na maboma 10,000 ambapo tunapendekeza tupeleke shilingi bilioni 125 kwenye upande wa maboma na hapa kila Halmashauri mtaondoka na maboma yasiyopungua kumi kwenye maeneo yenu ili kila mmoja aweze kwenda nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na tutakapoenda kwa mwaka hadi mwaka tunakwenda kuyamaliza na yenyewe na hapo yatakwenda juu zaidi kufuatana na mchanganuo wa gharama halisi utakavyoonekana kwenye fedha hizi ambazo tumeweka za nyongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye maboma ya afya; tuna maboma tulikuwa tumetengeneza, kuna zahanati na kuna zahanati zile zilizoko kwenye kata. Tuna zahanati ziko kwenye kila kijiji na tuna zingine tumeziweka kwenye kata, hii ni tofauti na vile vituo vikubwa ambavyo tunaviweka vina facilities nyingi. Vilishajengwa vingine vina miaka kumi, vingine 15 na hii ilikuwa nguvu ya wananchi. Tunapendekeza tupeleke shilingi bilioni 100 kwa ajili ya eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye haya maboma ya afya tunapendekeza tuyafanyie kazi kwa sababu hiki tunachoendea mbele cha bima ya afya kwa wote, hiyo bima ya afya kwa wote siyo ile kadi, ni facilities (vitendea kazi) ambapo inaanza na hospitali zenyewe, lakini pia dawa pamoja na vifaa tiba ambavyo vinatakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ni lazima tukamilishe kwanza haya yapatikane kila eneo na tunaendelea kufanya tathmini, wenzetu wa TAMISEMI wanaendelea kufanya tathmini na maeneo yale ambayo ni ya tarafa ama maeneo ya kimkakati ambayo hayajapata vituo vya aina hiyo. Lakini sambamba na yale ambayo yanahitaji ukamilishwaji ambayo tayari kazi inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais wetu aliposema kazi iendelee na kazi inaendelea, alikuwa anamaanisha hivyo. Hapatakuwepo na sehemu pana gap ya kazi inayotakiwa kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo hilo hilo la afya kwenye bima ya afya kwa wote na hospitali hizi ambazo zinaangukia Wizara ya Afya, tunapendekeza tupeleke shilingi bilioni 50 kwa ajili ya vifaa tiba pamoja na dawa, na hii ni nyongeza ya fedha ambazo zilishatolewa kwenye bajeti mama ya sekta ambayo tuliipitisha hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye hoja za Wabunge, jambo moja ambalo lilisemewa kwa sauti kubwa sana na kwa msisitizo sana, lilikuwa jambo la ring fencing ya fedha hizi. Waheshimiwa Wabunge walikuwa wanataka kujiridhisha kwamba fedha hizi zitatumika kwa matumizi yaliyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja, niwahakikishie Wabunge kwamba Mheshimiwa Rais yuko makini sana kwenye masuala haya ya fedha, sana. Sisi tulioko kwenye Wizara ya Fedha anatuelekeza kila wakati kuhakikisha fedha zinakwenda kwenye maeneo yaliyokusudiwa na maeneo yenye tija kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tutaifafanua zaidi tutakapokuwa tunaongelea masuala ya siku 100; lakini niwaelezee tu kwamba Serikali iko makini kwenye jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kwenye hili ambalo Waheshimiwa Wabunge mmelisema kwa nguvu sana, nilikuwa nawaona Mheshimiwa Munde, Mheshimiwa Lucy, Mheshimiwa Jesca, Mheshimiwa Matiko, Mheshimiwa Nape pamoja Wabunge wengine wengi, ni vile tu siwezi kumtaja kila mmoja, mlisema sana tuwahakikishie kwamba fedha hizi zitakuwa ring fenced. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na mimi niseme mbele yako, kwa sababu sekta hizi tunazozipelekea fedha nyingi zina mfuko, wala hatukuona sababu ya kuanzisha mfuko kwa sababu tumekitaja chanzo na tukataja zinapokwenda. Maana yake zinatoka kwenye chanzo, zinakwenda moja kwa moja kwenye mfuko ule ambao upo.

Mheshimiwa Spika, nimeshaeleza maeneo mengine, nilikuwa bado sijaelezea upande wa maji. Maji tulishapeleka bajeti. Muda huu ambapo tumeweka nyongeza hii tuliyoomba kwa Bunge lako Tukufu, tunapendekeza tuwapelekee Wizara ya Maji shilingi bilioni 207 za nyongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kama alivyosema Mheshimiwa Maganga jana, kwamba yeye ile fedha ya TARURA anatamani anunue greda; na mimi naendelea kuungana naye na ninamshauri Waziri wa Maji, fedha nyingine wanunue magari ya kuchimba visima, nyingine wanunue magreda ya kuchimba mabwawa, halafu fedha nyingine twende kwenye utaratibu wa kisima kila kijiji. Kama umeme upo kila kijiji tunakosaje kisima kila kijiji? Hili ni jambo ambalo litaweza kutekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo Mfuko wa TARURA upo kisheria, hivi tunavyoongea, na chanzo tumekitaja. Maana yake fedha itatoka kwenye chanzo inakwenda kwenye Mfuko wa TARURA kama ambavyo fedha zile zilizokuwa zinakwenda kwenye TARURA zimetumika zilivyokusudiwa kwa sababu kuna Mfuko wa TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna Mfuko wa Maji; fedha tulizotaja kutoka kwenye chanzo zinakwenda kwenye Mfuko wa Maji. Tuna Mfuko wa Elimu ya Juu, Bodi ya Mikopo, fedha iliyotajwa inakwenda moja kwa moja kwenye Mfuko wa Elimu ya Juu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa bima ya afya kwa wote sheria inakuja siyo siku nyingi, kwa hiyo, hatukuona kutengeneza sheria inayohusu tu huo mfuko wakati kuna jambo linakuja kubwa linalohusisha bima ya afya kwa wote. Kwa maana hiyo na mfuko wake utatajwa na sheria ambayo itakuja kufuatana na mpangilio unavyopangwa wa shughuli zetu za Kibunge (Makofi)

Mheshimiwa Spika, upande wa maboma, hiyo kwa sababu ni maboma, ni kitu endelevu, tumeona yenyewe itakuwa fedha ambayo inakwenda kwenye Wizara husika kufanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, SGR pamoja na reli, Mfuko wa Reli upo, kwenye SGR ni mradi wa kimkakati ambao wote tunautolea macho kwamba ni lazima ukamilike. Kwa hiyo, tumeona kwa kweli Wabunge pamoja na Watanzania mtuamini kwenye hili, tunakwenda kulifanyia kazi ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa TARURA tunarekebisha kipengele kile ambacho kilikuwa kinazuia Halmashauri, Majiji na Manispaa kutengeneza barabara. Kama tumeshachukua baadhi ya mzigo wa kuwalipa Madiwani kwenye makusanyo yao ya ndani tunafungulia kanuni ile na wenyewe waweze kufanya periodic maintenance ya barabara zao. Kwa hiyo hilo tutalifanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na ninaamini tuna majiji ambayo wana uwezo mkubwa kabisa wa kuweza kuzitengeneza barabara zao na tukaunganisha nguvu hii ambayo tumeisema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo lilichangiwa kwa hisia na Waheshimiwa Wabunge na kule kwa wananchi wetu lilikuwa na hisia, ni jambo la kodi ya majengo kwa kutumia LUKU. Kati ya maswali yaliyokuwa yanaulizwa ni inakuaje mpangaji ndio awe mlipaji? Je, nyumba zenye mita nyingi? Nyumba kubwa zenye mita moja? Itakuaje kwa nyumba ya nyasi? Itakuaje kwa nyumba za vijijini; itakuaje kwa nyumba zisizo na umeme; taasisi pamoja na rika lililosamehewa itakuaje?

Mheshimiwa Spika, moja niwaombe Watanzania tusiigope teknolojia, teknolojia imekuja ili itusaidie, duniani kote teknolojia imeletwa ili kurahisha ufanyaji wa mambo, ndiyo kazi moja kubwa ambayo unaweza ukaitaja kwa sentensi ya ujumla, imekuja kurahisisha kazi. Sasa wenzetu ambao wanashughulika na masuala ya umeme pamoja na wale wanaoshughulika na IT wametuhakikisha kwamba mambo haya yote yanakwenda kwa programming.

Mheshimiwa Spika, leo hii hata tulivyoongea na Waziri wa Nishati walituhakikishia kwamba wanao uwezo wa kuitisha LUKU zote, wanao uwezo wa kuitisha mita zote, wakajua na mtumiaji anatumia kiwango gani, wanajua, wanajua hata trend ya matumizi wanajua, wanajua na nyumba zenye mita zaidi ya moja, hazikujibandika zile mita zimeenda kuwekwa.

Mheshimiwa Spika, takwimu zake zote zipo na zipo namna ya kuitisha, tulivyohakikishiwa hayo tukaona ni jambo ambalo tutafanya programming na wenzetu hivi wapo busy wanafanya programming. Watafanya programming tunaitoa sheria nzima ile iliyokuwa inatumika kukusanya manually tunaipeleka tukusanye kiteknolojia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatuendi kuvunja Torati, tunaenda kuimarisha Torati, vilevile ilivyokuwa inafanyika manually tunaipeleka tunaikusanya kiteknolojia, kwa mfano, kama jengo moja ambalo linastahili kuwa la mita moja lina mita 12 tunaenda kuzi-program kwamba zipo 12; kwa hiyo, kwenye 12,000 tunagawanya kwa 12 tunazi-program kwa hiyo kwa mwezi atakuwa analipa mia, mia badala ya 1000 ni 12 gawanya kwa watu 12. Tunagawanya kwa idadi ya mita tupate ka kiwango ambacho kwenye kila kijimita tutapata.

Mheshimiwa Spika, wengine walikuwa wanasema je, wale ambao hawatumiagi hata shilingi 1,000 hiyo kwa mwezi, wenzetu kimtandao unaitisha wale ambao hawatumiagi hata hiyo maana yake unawatoa kiurahisi kuliko kutembea siku nzima unawatafuta. Unaitisha tu au una blacklist hawapo na wale waliosamehewa hivyo hivyo una program unawatoa, hivyo hivyo na kwenye nyumba ambayo ina mita zaidi ya moja na kwenye eneo lilitakiwa kuwa na mita zaidi moja mathalani ghorofa lilitakiwa kuwa na malipo yanayoendana na flats zile ilivyokuwa imebainishwa kwenye sheria tuna program hivyo hivyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo sisi tuliona hii imerahisisha utaratibu kwa wananchi wetu ni wao tu kukubaliana na hali hiyo na waweze kujua kwamba teknolojia imekuja iturahisishie. Hebu fikiria uwezekano katika karne hii eti watu wanatangaziwa deadline ya kulipa mita unakuta wamepangana mstari kama hapa na Dodoma Sekondari kule, wanaenda kulipa shilingi 10,000; mwingine ametoka sijui wapi anapanda gari, mwingine anatumia nauli, mwingine anaendesha gari, mwingine anapoteza na muda anaenda kulipa shilingi 10,000, anaenda kulipa shilingi 50,000 tumezigawanya kama tulivyozigawanya, tuna program, zitakuwa programmed hivyo ndivyo ambavyo itafanyika, hivi vitu vinawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa wale waliokuwa wanapata msamaha kama ni wazee, kama ni Taasisi za Kidini tunaenda kufanya hivyo hivyo, tuna program kwenye vitendea kazi vyetu hawatakuwepo na tunaenda kutekeleza sheria vilevile. (Makofi)

Kwa nyumba zile ambazo zipo vijijini wengine walikuwa wanabandika tu kanyumba kapo kijijini hapana, hii hatutaenda kutoza kwenye kila mwenye umeme na wala hatutaenda kutoza kwa matumizi ya umeme kwa sababu tukitoza kwa matumizi ya umeme tutaongeza gharama za uzalishaji, tunaenda ku-program kodi inayotakiwa kutozwa ya jengo kwenye eneo husika.

Mheshimiwa Spika, nchi zote zilizoendelea hawatozi kwa kupanga mistari, wanatoza kieletroniki hiyo ndiyo faida ya teknolojia. Hata hapa Afrika, Namibia kuanzia kodi ya ardhi wanatoza kwa utaratibu wa LUKU, kodi ya jengo wanatoza kwa utaratibu wa LUKU, kwa hiyo mtu anakuwa anajua kwamba nina commitment zangu hizi hapa anazitoa kwa kutumia simu yake akiwa yupo nyumbani kwake, akiwa yupo ofisini kwake bila kusumbuana kupanga foleni kwa njia zile za kienyeji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hata maeneo ambayo yatatozwa ni yaleyale yaliyoanishwa yenye sifa siyo kila kijiji, siyo kila nyasi, siyo kila mwenye umeme ni yule ambaye anaangukia kwenye sifa zile ambazo tulishakubaliana kisheria. (Makofi)

Kwa wale wachache ambao wanatumia solar hili eneo tumesema ni wachache wale wataendelea ku- graduate kuungana na wale wenye umeme, tumewaachia TAMISEMI watafanya hiyo na kitakuwa moja ya chanzo ambacho na wenyewe watatumia kwenye haya maeneo mengine ambayo tunawakabidhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine lilikuwa linasemwa kwamba sasa je, kwa nini itozwe kwa mpangaji? Nasema na nasisitiza kodi hii si ya mpangaji, hii ni kodi ya mmiliki, hii si kodi ya mpangaji ni kodi ya mmiliki, utaratibu huu tunaotumia ni utaratibu ambao hata kwa karatasi alikuwa akikutwa yule ambaye anaishi kwenye ile nyumba anasaini kwa niaba ya mwenye nyumba, wakionana kwa taratibu wanazozijua wana-offset hiyo difference hata kwa karatasi ndivyo walivyokuwa wanafanya, ndiyo utaratibu uliokuwa unafanyika, hakuna nyumba ambayo ina mita ambayo haihusiani kabisa na mwenye nyumba na hakuna nyumba ambayo mtu anaishi hausiani kabisa yaani hawajuani wala hawajahi kuwasiliana hata kwa kutumia mtu wa kati kama dalali kwamba wewe basi kaa hapa, hakuna mtu anayeenda kuingia tu kwenye nyumba isimekane kwamba hata muona wala hawatakuwepo na hata third ya part wa kuonesha huyu anakutana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hoja ya kwamba akitokea mwenye nyumba asiye na busara au akatokea aliyemkorofi, niwatangazie wenye nyumba wote hili si jambo la mahusiano, hili si jambo la mahusiano ya mpangaji na mwenye nyumba wala hili si jambo la kirafiki hili ni jambo la nchi, jambo la sheria, akitokea mkorofi nchi hii haijawahi kushindwa kushughulika na wakorofi, akitokea asiye na busara pia na yenyewe tutafundishana busara hili ni jambo la nchi ni jambo la sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo wapangaji wala wasipate shida, kama una mwenye nyumba ambaye atakiuka sheria za nchi zinazohusu masuala ya kodi sheria zetu zipo wazi kwa watu wa aina hiyo ni kitu gani kinafanyika kwa maana hiyo hatua za kisheria kwa watu wa aina hiyo zitafuata tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niliona hili na lenyewe nilisisitize na niwaombe Watanzania tusiogope teknolojia, tutumie teknolojia itusaidie kuendesha mambo yetu kwa urahisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapa hapa kwenye hilo la upande wa kukusanya; watu wameanza kuchanganya hii habari ya kulipa kodi. Tunaposema kulipa kodi kwa hiari watu wameanza kuchanganya wanadhania kodi ni hiari, tunaposema tutoe elimu watu walipe kodi kwa hiari watu wameshaanza kuchanganya wakidhani kodi ni hiari na wengine wanachanganya halali na hiari, kana kwamba sasa mtu atakuwa na uamuzi wa kulipa ama kutokulipa kwamba anaweza kupanga tu kwamba yaani anaambiwa kabisa kodi yake stahiki ni hii ila anapanga kama alipe au asilipe, that is a gross mistake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kodi yoyote anayostahili mtu kulipa ni kitu cha lazima, lazima alipe. Tunachosema kwa hiari tunasema usisubiri kusukumwa, tunaongelea wajibu kwamba watu wawajibike kulipa, watu wanataka kuchanganya hiari aone kama vile anaweza akawa na uamuzi wa kulipa ama kutokulipa. Si jambo la kuamua ama ulipe ama kutokulipa, kodi stahiki kwa mtu yeyote kodi stahiki lazima alipe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunachosema tutatoa elimu tunasema usisubiri kusukumwa na wala usiingie kwenye mitego ya kukwepa kulipa unatafuta matatizo, hivi tunavyoongea tunapoanza Julai, tutafuatilia utaratibu wa matumizi ya EFD, tutayafuatlia sana lakini pia tutafuatilia watu walipe kodi stahiki, tutafuatilia sana watu walipe kodi stahiki, tutalifuatilia hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa wale ambao wanapenda kuamua kwamba nipewe bei isiyo na risiti au yenye risiti twendeni tutoke kwenye kupeana bei yenye risiti au isiyo na risiti twendeni bei ni moja yenye risiti lipa kodi ya Serikali. Tutaelimishana kwenye hili na wakati ule nilimteua unajua kuteua ni kuzuri, nilimteua Subira natamani kulirudia hili neno nilimteua Balozi wa Kutoa Elimu ya Kulipa Kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nafanya na teuzi zingine namteua na Zulfa Omary kutoka Pemba na yeye atatusaidia…(Makofi)

SPIKA: Yupo wapi Mheshimiwa Zulfa. (Kicheko)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, namteua na Ndugu yangu Ameir Abdalla Ameir yule shabiki mpya wa Yanga ambaye aliguswa na bajeti hii, haukuwepo siku ile kwenye kiti, Mheshimiwa Ameir alisema tangu ujana wake, tangu mtoto kwa takribani zaidi ya miaka 12 iliyopita alikuwa shabiki wa Simba ila anasema kwa bajeti hii ameamua kuingia Yanga. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, hii elimu pia ya mlipa kodi, si elimu ya darasani tu, kule tunapata elimu ya darasani, lakini pia tunataka tufanye elimu ya hamasa ya kuhamasishana, taasisi yangu ya Mamlaka ya Mapato watafundisha kitaalamu technical issues pamoja na faida zile, wataonesha na kinachofanikiwa.

Mheshimiwa Spika, lakini, vijana wetu pia wana lugha wanazoelewana wao wenyewe, kwa hiyo na kule nateua kwenye kundi hilo, nateua mabalozi wa kuhamasisha kulipa kodi kwa hiari, namteua mwana kabumbu mashuhuri Mbwana Samatta na yeye awepo kwenye Mabalozi ya Kulipa Kodi, namteua Ndugu Edo Kumwembe na yeye awepo kwenye Mabalozi ya Kulipa Kodi na kwa wanawake namteua Ndugu Hamisa Mobetto na yeye atatusaidia kuhamasisha kwenye walipa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo tulikuwa tunapata shida nalo ambalo na lenyewe tunalifanyia kazi kama Serikali na kama Wizara, tuna tatizo kwenye masuala ya ukadiriaji, tunashida kubwa kwenye masuala ya ukadiriaji, ndiyo maana tuna mrundikano mkubwa sana wa kesi kwenye vyombo vyetu.

Mheshimiwa Spika, wanauliza huku hamna balozi? Subirini nimemteua Matiko kuwa Balozi wa Usemaji upande wa Magereza. (Kicheko/Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Waziri bado sijaisikia vizuri hii. (Kicheko)

WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Spika, nimemteua Esther Matiko Msemaji wa upande wa Magereza. (Kicheko)

SPIKA: Ana uzoefu wa kutosha. (Kicheko)

WAZIRI WA FEDHA NA MAPINGO: Mheshimiwa Spika, na nimemteua Mheshimiwa Ester Bulaya upande wa masuala ya wastaafu, amelisemea sana hilo pamoja na wenzake na Mheshimiwa Cecilia upande wa mfumuko wa bei, hizo hoja zilikuwa zinakuja huku mbele. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, Kwa hiyo, kwenye upande wa ukadiriaji kuna shida moja tu sisi kama Serikali tumeiona. Moja; ukadiriaji ile ya kwamba mimi nakukadiria, usiporidhika kesho uje tuongee na mimi mwenyewe na usiporidhika nenda kwenye hatua nyingine, lakini ili usikilizwe huko unapokwenda ulipe kwanza theluthi moja ya kile ambacho umekikataa.

Mheshimiwa Spika, hivi theluthi moja ya bilioni 150 ni ngapi? Theluthi moja ya bilioni 90 ni ngapi? Sasa tunapendekeza tunapokwenda tutaanzisha chombo cha Msuluhishi wa Masuala ya Kikodi ili kuwatengenezea watu wetu badala ya kutumia njia moja ya kupeleka kwenye Mahakama ya Kikodi pamoja na bureau za kikodi wawe na fursa ya kusemea mambo yao, lakini pia tunaendelea kuimarisha ile mifumo ya ndani ili pasiwe na uonevu kwenye ukadiriaji wa kodi mtu akadiriwe kodi anayostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuanzia tarehe 1 Julai hili na lenyewe tutalifuatilia kwa karibu sana. Kwa mfano nilipata kesi moja hivi juzi, kuna mtu mmoja alienda akakadiriwa shilingi milioni 400, alivyokadiriwa shilingi milioni 400 yule aliyemkadiria akamwambia alete shilingi milioni 200 za kwao wale wakadiriaji, akakataa, alivyokataa hiyo ilikuwa tarehe 23 Novemba, akakataa kutoa shilingi milioni 200 hiyo alivyokataa, tarehe 23 Novemba alivyokadiriwa kwa barua kwamba makadirio yako ni shilingi milioni 400, lakini akaambiwa lete shilingi milioni 200 alivyosumbuka sumbuka akaambiwa wewe unajifanya mjanja. Tarehe 27 kutoka tarehe 23 Novemba siku nne baadaye akakadiriwa shilingi bilioni 2.5, hiyo ni tarehe 27 Novemba 2020, alivyokadiriwa hii sasa kaenda akaongea nao kwamba ule mpango basi nimeshakubali akatanguliza shilingi milioni 100, alivyotanguliza shilingi milioni 100 tarehe 3 Disemba ikashushwa ile kutoka shilingi bilioni 2.5 ikarudi shilingi milioni 320. Maana yake nini? Maana yake hii ni rushwa, haya hayawezi yakawa makosa ya kawaida. Nimepeleka kumbukumbu hii vyombo vya dola vitachukua kazi yake na wale watu nimemuelekeza Kamshina achukue hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, dakika zangu zimekwenda, nilipokea jambo lile alilisemea Mheshimiwa Nape la kule TIPER, nimeelekeza zoezi lile liendelee, waendelee na utaratibu, kulikuwepo na shida ya taratibu zetu za kindani ya kiofisi nimeshaelekeza waendelee hizo hatua zingine ambazo zilikuwa zinakwamisha zitakuta wale kule wanaendelea pasiwe na gap pale.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Wenyeviti wa Vijiji pamoja na Ma-VEO, pamoja na posho mlizotaka za Madiwani ziongezeke za Watendaji niwaombe mridhie tumeanza na hatua hii, na kama ambavyo Mheshimiwa Rais alisema kwa wafanyakazi wote, alisema tunaanza na hatua hizi mwaka kesho tutaangalia zaidi na mimi nitumie kauli ile ile aliyoisema Mheshimiwa Rais tuanze na hatua hizo halafu mwaka kesho tutaangalia zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa mifugo, kilimo na uvuvi, tumeshaongea na Wizara zinazohusika na mimi natoa ridhaa ya yale maeneo ambayo yanataka kufanya financing za kisasa wafanye hivyo kwa upande wa mifugo, kilimo na uvuvi na sisi kama Wizara tutafanya nao karibu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata kwa upande wa Zimamoto, upande wa Zimamoto tumeongea na Waziri anayehusika natoa ridhaa arekebishe kanuni kwenye upande wa makato yale ya tozo zile ambazo zinakuwa ngumu kukusanyika kwa upande wa Zimamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Askari Magereza pamoja na wa Zimamoto na yenyewe tunaoanisha, tumeongea na Waziri mwenye sekta, Mheshimiwa Simbachawene, tumeoanisha na wenyewe kwenda miaka sita kama tulivyosema kwa polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye mambo ya sensa ya mwaka huu inayokuja tunapanga tuimarishe na kile kipengele cha makazi, tulikuwa tunaangalia zaidi upande wa idadi ya watu, tutaweka mkazo kwenye upande wa makazi ili hivi vitu vingine ambavyo vinahusiana na mambo ya makazi na vyenyewe viweze kuzingatiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa miradi ya kimikakati, Mheshimiwa Asenga amesema sana kule kwake, nimemuelekeza Katibu Mkuu ashungulikie yale maoni yako, asimamishe lile jambo ambalo lililokuwa linafanyika ambalo umelisema kwa nguvu sana ili waweze kuingia kwenye mkataba ambao utakuwa na manufaa kwa wananchi siyo ule ambao unaleta fedha, unatumia fedha nyingi kuliko maeneo mengine yote ambayo yaliwahi kutumika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa Covid tunaenda na utaratibu ambao Mheshimiwa Rais aliunda Kamati na kamati ile ilishatoa taarifa na sisi tutaendelea kufanya kama ambavyo imefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mengine tutaendelea kufafanua tunapokuja kwenye Finance Bill, lakini nililisikia jambo la Mheshimiwa Festo Sanga la nyasi wamesema na Wabunge wengine wengi ambao wamesema kwa kweli isiishie tu majiji na sisi tunakubaliana, tutaenda mpaka Manispaa na kwa maeneo mahususi ambayo hayako Manispaa wala hayako, lakini yanauwitaji huo tutaweka kipengele ambacho itahiji ruhusa maalumu mbali na ile ya BMT ambayo mlipendekeza tuipeleke ya kutolea ridhaa ili iweze kuombewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tutaenda mpaka Manispaa, lakini kama kuna eneo mahususi litaombewa tutaweka kwenye kipengele tunavyokuja kwenye Finance Bill kwa yale ambayo hayako pale, tumeona tuanze na hivyo kwa ajili ya control, hilo lilikuwa na nyasi bandia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeona kengele imeshagongwa kwa kumalizia, tumeongelea hii sekta ya michezo, lakini lazima kwenye michezo mimi ninavyoangalia hii naongea tu kiuanamichezo, siyo kama shabiki na uniazime dakika zingine mbili za nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwenye michezo bado tunakosea kwenye mipangilio/mipango yetu, vitu vyetu vingi bado vinakuja kwa dharura. Ninaposema haya kwanza niipongeze kabisa Simba imefanya hatua kubwa sana mwaka huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini mimi nilivyokuwa naiangalia Simba ya mwaka huu, Simba ya mwaka huu ilikuwa ya kwenda kuchukua ubingwa. Kuna mahali tumekosea na tunakosea pale ambapo hatuweki vipaumbele, yaani sisi kwetu mambo yote yako sawa tu, kwamba mtu anaenda kucheza mchezo ambao unaweza kuleta kombe Tanzania kwa mara ya kwanza, anaenda kucheza nusu fainali, maana yake ili ucheze fainali lazima ucheze nusu fainali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, anaenda kucheza mchezo mkubwa wa kuleta kombe mathalani, ukishinda nusu fainali na kiwango nilichokuwa nakiona wangeweza kuleta kombe. Huku una mchezo wa nusu fainali wa muhimu kwenye historia, katikati yake unaweka mechi ya watani. (Kicheko)

Sasa mimi nilivyoona Simba walivyofungwa kule Afrika Kusini, wao na wengine wanaaminishwa kama wamehujumiwa na nani yule/anaitwa nani yule, Senzo, wengine wanaaminishwa kwamba wamehujumiwa na watani mnawalaumu watani bure. Kiuanamichezo kabisa tunakosa mpango, Simba imeenda kucheza South Africa bila game plan, yenyewe ilijiandaa na mechi ya mtani na mimi niwapongeze Yanga, walivyoenda uwanjani wakakaa dakika kadhaa wakaona Simba hawapo, wakajua wanajiandaa na mchezo hawa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, on a serious note timu zinazokwenda kwenye mashindano ya Kimataifa, zinaleta sifa ya Taifa. Lazima bodi hizi zinazosimamia wawe wanawapa kakipaumbele wawape, waangalie wangeweza kupeleka mchezo huko. Kwa sababu leo hii, kwenye timu zetu hata kama ni fainali ukiweka mtani hapa akili zote na miundombinu yote inaelekea hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Simba hii ilivyokuwa imempiga Al- Ahly ingehujumiwa na Senzo kweli! Eti ihujumiwe na mashabiki! Hapa walienda bila game plan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, la mwisho niwapongeze sana wana Yanga ambao wamewaunga mkono Simba. Wamewaunga mkono Simba, wana Yanga wamewaunga mkono Simba kwa kuwapa Morrison, licha ya wana Simba kuwa na mashabiki wenye heshima wengine tunao humu humu, hawakuwahi kurudisha hata tiketi tu ambayo Yanga walimletea Morrison hapa. (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, nakukumbusha baada ya hapa kuna kura zinapigwa! (Makofi/Kicheko)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, wana Yanga muendelee na upendo huo huo na wala waachieni tu Morrison anakuja Makambo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuwa nimewasilisha na kufafanua baadhi ya hoja, msingi wa Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2021/2022, 2025/2026, wenye dhima ya kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu, kwa mara nyingine tena nitoe rai kwa Waheshimiwa Wabunge wote, wananchi na wadau wote kwa kuendelea kushirikiana pamoja katika kutekeleza mpango huo. Na niwaombe Watanzania wote tujitoe tumuunge mkono Rais wetu katika kutekeleza dira hii twende naye bega kwa bega nchi hii itajengwa na Watanzania wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawashukuru tena, Waheshimiwa Wabunge tuendelee kuiunga mkono Serikali na kabla sijahitimisha maelezo yangu, nichukue fursa hii pia niwashukuru watumishi wote wa Wizara ya Fedha na Mipango, nikianza na Naibu Waziri - Mheshimiwa Mhandisi Hamad Masauni, Mbunge na Naibu Waziri pamoja na Katibu Mkuu Emmanuel Mpawe Tutuba, Naibu Makatibu Wakuu - Ndugu Amina Shaban, Dkt. Hatibu Kazungu na Ndugu yangu Adolf Ndunguru kwa kutupa ushirikiano mkubwa katika kuandaa na kutekeleza majukumu yetu. (Makofi)

Niishukuru tena Kamati yako ya Bajeti nimeenda mle hii Kamati inafanya mambo very professional, tulifanya uchambuzi ulio bora sana na ndio maana kazi yetu inakuwa rahisi. Naamini tutatekeleza pakubwa zaidi na hata zile hoja walizotoa za kutengeneza utaratibu wa monitoring and evaluation, unaweza pia ukaendelea kuzitumia Kamati hizi. Kamati ya Bajeti, ya LAAC pamoja na ya TAMISEMI kwenye haya maeneo ambayo tunaelekeza fedha nyingi wakaweza kufanya ufuatiliaji sambamba na taasisi zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuwa nimetoa ufafanuzi huu naomba sasa, Bunge lako liridhie bajeti hii na nawaomba Wabunge wote na naamini Halima Mdee kwa mara ya kwanza utapiga kura ya ndiyo. Wote tuipigie bajeti hii kura ya ndio kwa sababu inakwenda kufanya mapinduzi. Wote na wenzako, hii ni bajeti yetu, tumeshiriki kuitengeneza na angalieni vitita tunavyoondoka navyo kwa ajili ya miradi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, waheshimiwa wananchi nifafanue tu hilo sio kila Mbunge atabeba kwenye pickup hizo fedha, bali zitakwenda kwenye Halmashauri zetu Wabunge wenu wameziomba tu, ila wasije wakafika kule wakasema Waziri aliwaambia mtakuja na hizo fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba sasa kutoa hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naafiki.