Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hoja hii ya Serikali ambayo ni bajeti ya Serikali. Kwanza nianze kwa kusema naunga mkono hoja hii, kwa sababu bajeti hii ya Serikali, ni bajeti ambayo inakwenda kuimarisha Sekta ya Elimu, ni bajeti ambayo inakwenda kutatua changamoto zilizopo katika Sekta ya Elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimefurahishwa sana na hatua ya Serikali kuongeza vyanzo vya kuboresha barabara vijijini, kwa sababu barabara zinapokuwa mbovu hata Wizara ya Elimu tunapata shida kupeleka mitihani. Kwa hiyo barabara zikiwa nzuri hata Walimu wanapokuwa wanakwenda kwenye shughuli za kufanya kazi mjini kama wana shida au wanaenda kikazi itawarahishia ili kurudi mapema kufundisha. Pia suala la maji na umeme, ni muhimu ili elimu iende vizuri. Kwa hiyo naunga mkono hoja kwa asilimia mia kwa sababu mambo haya yamekwenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja hii pia kwa sababu kwanza imeimarisha hata mikopo, naona hata vijana wangu wapo hapa, mikopo kwa fedha zilizotengwa mwaka 2020/2021ilikuwa ni shilingi bilioni 464, lakini katika bajeti ya Wizara yangu iliyopita zipo bilioni 500, zilizopita zilikuwa bilioni 464 na mwaka unaokuja ni bilioni 500.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge wakipitisha mapendekezo haya ambayo Mheshimiwa Waziri wa Fedha ameyaleta, tutaweza pia kupata fedha nyingine za nyongeza katika Bodi ya Mikopo. Haya ndiyo yamenifanya niweze kuunga mkono hoja hii na nawasihi Waheshimiwa Wabunge waiunge mkono ili vijana wetu waendelee kusoma. Pia kwa wale ambao hawana uwezo wa kujikimu, basi Serikali iweze kuongeza wigo na tupunguze zile kelele za wanafunzi ambao wanakuwa na sifa wanadahiliwa na wakati mwingine wanakuwa wanakosa mikopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitapenda kuchangia baadhi tu ya maeneo machache ambayo yamezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge katika hoja hii. Kwanza niongelee suala la ujuzi, Waheshimiwa Wabunge wameendelea kusisitiza kwamba elimu yetu iwe kwa vitendo zaidi, ijenge ujuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nikwambie kwamba suala hilo tayari, hata kwenye hotuba ya bajeti yangu nimeshaliweka, lakini ni maelekezo ya Mheshimiwa Rais wetu wa Awamu ya Sita, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, ameshatoa maelekezo kwa Wizara ya Elimu na tayari tumeanza mapitio, mlituona Mlimani City tarehe 18 Juni, tulikaribisha wadau wa elimu ambao wametupa maoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunapokea maoni kwa kupitia njia ya kimtandao google drive ambayo mpaka jana mchana tulikuwa na wananchi 1,152 ambao walikuwa wametoa maoni kwa njia ya mtandao. Kwa hiyo tutaendelea maoni na niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba, tutafanyia kazi na wasikose kuendelea kutupatia maoni na tutapanga muda mahsusi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa tumepanga tuwe na mjadala Dodoma tarehe 26 Jumamosi, lakini Wizara ya Uwekezaji na Ofisi ya Waziri Mkuu tayari wana jambo lao, Kongamano la Vijana. Kwa hiyo tutaangalia kwa sababu yote ni mambo Serikali, hatuwezi tukaweka mambo mawili kwa wakati mmoja ili kuweza kuruhusu ushiriki kikamilifu kwa sababu masuala yote ni muhimu, lakini niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba tutaendelea kuwashirikisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo lingine ambalo limezungumziwa kuhusiana na suala la watoto kubaki shuleni wakati wa likizo. Huwa ni msikivu sana na huwa najizuia kumpa Mheshimiwa Mbunge mwenzangu taarifa anapoongea, lakini leo kidogo jinsi lilivyoletwa na nikasikia kama mama, nasikia hata kauchungu fulani, Mheshimiwa anavyosema kwamba kuna baadhi ya shule wanawacha watoto shuleni, hakuna mabweni, wanafunzi wanalazwa kwenye sakafu kwenye majani. Hiyo hapana, hiyo sio sawa na Serikali haiwezi kuruhusu jambo kama hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeweka mfumo wa kwenda likizo kwa sababu tunaamini kwamba akili ya binadamu inachoka. Wanafunzi wanahitaji kupumzika, kukaa na familia zao na kufanya shughuli za nyumbani, maana akikaa shuleni tu kila wakati, mazingira pia mengine wanakuwa hawawezi kuyafanya. Nikitoa mfano wa wanafunzi wa kidato cha nne, wamefungua shule January, 13. Wataanza mitihani yao ya kumaliza kidato cha nne, tarehe 14 mwezi Novemba. Sasa mtoto yupo tangu January unamwambia mwezi Juni asiende nyumbani akae shuleni mpaka Disemba ndio anamaliza mitihani tarehe 13 Desemba.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kama Serikali tunaona kwamba likizo kwa wanafunzi ni muhimu. Kwa sababu suala la mjadala wa elimu lipo mezani, tumeshafungua pazia, tunapokea maoni ya wadau na hili suala la likizo ya wanafunzi ambao wapo kwenye mitihani, tulipitie ili tuone kama kweli tumefika mahali ambapo tunaona kwamba Serikali itoe waraka ili ifute hizo likizo. Kwa sasa tunatekeleza nyaraka ambazo zipo na nyaraka ambazo zipo ndio zinavyoelekeza, wanafunzi wapate na muda wa kupumzika.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba, utaratibu pia unaowekwa na shule ambazo zinawabakiza watoto shuleni unakuwa pia mwingine siyo sawa, kwa sababu inakuwa kama ni dharura, wazazi inakuwa kamata kamata, lazima walete hela na mzazi asipoleta mtoto inakuwa ni shida. Sasa kipindi cha likizo ni kipindi cha kupumzika, isiwe ni lazima kwa mzazi ambaye labda anaenda likizo anataka mtoto wake aende naye, anaambiwa lazima abaki shuleni.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kuzikumbusha shule za Serikali, Serikali inatoa elimu bila malipo, sasa hili la kuwabakisha wanafunzi wakati wa likizo limekuwa ni uchochoro wa kuongeza gharama. Gharama zinazotozwa wakati wa likizo zinaanzia Sh.5,000 mpaka Sh.250,000 kwa mwezi mmoja. Kwa hiyo sasa ni namna ambavyo gharama za elimu zinarudishwa kwa njia nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwakumbushe Maafisa Elimu wa Mikoa wote na Maafisa Elimu Wilaya kuzingatia waraka wa elimu namba tatu wa mwaka 2016, ambapo umeelekeza bayana kwamba Serikali inatoa elimu bila malipo na kama kuna ulazima wa kuwachangisha wanafunzi michango ya aina yoyote, Waraka Na.3 wa mwaka 2016 unaelekeza utaratibu unaopaswa kufuatwa. Kwa hiyo wazingatie utaratibu huo, vinginevyo Maafisa Elimu, kwa sababu sehemu tumefuatilia sehemu nyingi shule zinafungwa kwa maelekezo ya Afisa Elimu, Waziri wa TAMISEMI ambaye ndiye anasimamia shule hana taarifa, Waziri wa Elimu hana taarifa, kwa hivyo Maafisa Elimu acheni kupoka mamlaka ya kuweka sera.

Mheshimiwa Naibu Spika, shule nyingi za Serikali zimeanza huu mtindo, hata madarasa mengine yasiyokuwa ya mitihani wanaambiwa wasiende shule. Leo nimepata malalamiko kwa mfano Kagera, kuna shule moja, mpaka wanafunzi wa elimu ya awali wanaambiwa wasiende likizo. Hiyo hapana, inakuwa too much sio tu masuala ya mitihani, yaani wanasema mafunzo rekebishi na kila mwanafunzi anayekwenda shule hata huyo mwanafunzi wa elimu wa awali, anatakiwa alipe. Kwa hiyo ukilitafakari kwa undani, kuna baadhi ya shule, Serikali inatoa elimu bila malipo, lakini wao wameamua kurudisha gharama kwa kivuli cha kwamba wanaandaa wanafunzi. Tumetunga mtaala wetu, tunaamini kwamba siku 194 za masomo zinatosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, halafu ng’ombe hanenepeshwi siku ya mnada, mwanafunzi amekuwa shuleni miaka saba, darasa la kwanza, la pili kwa nini nguvu anayotumia mwanafunzi akiwa kwenye darasa la mitihani wasitumie miaka yote mwanafunzi anapokuwa shuleni? Kama hakuandaliwa vizuri kwa miaka saba jinsi mitaala yetu ilivyoandaliwa, haiwezekani kwa mwaka mmoja ukamshindilia mtoto, mambo ambayo alipaswa kusoma kwa miaka saba, huyu mtoto akaweza kuelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kitendo cha kuwashindilia watoto mwaka wa mwisho, unataka mambo ambayo walitakiwa kuwafundisha miaka saba, ayasome kwa mwaka mmoja, wengine ndio maana wakiingia kwenye vyumba vya mitihani wanwakuwa wamechanganikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kwa heshima na unyenyekevu mkubwa, naomba sana Waheshimiwa Wabunge, Serikali imelipokea suala hili na kwa sababu linaonekana ni tatizo tuna malalamiko mengi sana kutoka kwa wazazi. Shule binafsi nyingine zina utaratibu mzuri tangu kwenye joining instruction wanakuwa wameonesha na inakuwa ni sehemu ya ada zao, lakini kuna shule nyingine zinakuwa zinawashtukiza wazazi tu dakika ya mwisho mwanafunzi anatakiwa kuja, inakuwa kama dharura kwamba hawatakuja.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nadhani suala hili kama Serikali kwa sababu tumeshaiona hiyo changamoto, Waheshimiwa Wabunge tunapokea maoni kuhusiana na mitaala. Hata hivyo, suala hili lenyewe, tutalichukua na kwenda kulifanyia kazi na hasa hizi shule za Serikali, tutakwenda kufanya ukaguzi kwa sababu kuna shule za msingi kwenda mwanafunzi kusoma wiki tatu anatakiwa alipe Sh. 85,000/= shule ya Serikali. Hii sio sawa, msimamo wa Serikali kutoa elimu bila malipo upo pale pale, tutaendelea kutoa elimu bila malipo bila ya kuingiza gharama kwa kutumia kivuli kingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa elimu ya juu, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba bajeti hii inakwenda kuimarisha miundombinu katika elimu ya juu, inakwenda kuhakikisha kwamba tunaongeza idadi ya wanafunzi ambao wanajiunga na elimu ya juu kwa sababu kutokana na elimu bila malipo, ongezeko la wanafunzi Shule za Msingi na Sekondari ni kubwa. Kwa hiyo, tunaandaa mazingira sasa ya kuwapokea watakapokwenda Vyuo Vikuu. Kwa hiyo, tutakuwa na ujenzi wa miundombinu, kutakuwa na kutoa ufadhili wa wahadhiri wetu ili waweze kupata shahada za uzamivu na tuweze kuandaa walimu wengi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, tutaimarisha sana mafunzo kwa vitendo. Hapa niendelee kuwasishi Wakuu wa Vyuo, Taasisi za Elimu ya Juu kuweka ushirikiano mzuri na sekta binafsi pamoja na viwanda ili kuweza kupata sehemu za kufanya mafunzo kwa wanafunzi wetu wa elimu ya juu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja hii kwa sababu hakika inakwenda kuimarisha elimu yetu. Nashukuru sana kwa nafasi. (Makofi)