Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Na mimi nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kukubali bajeti nzuri namna hii ije hapa Bungeni. Pia niwapongeze wapishi, Mheshimiwa Waziri, Dkt. Mwigulu Nchemba na Eng. Hamad Masauni kwa namna ambavyo walipika na hatimaye kutuletea hapa. Lakini pia nichukue nafasi hii kuwashukuru sana Kamati ya Bajeti ambao walitoa maoni mazuri sana kuhusiana na bajeti hii; uchambuzi wao kwa kweli umejitosheleza nami nawashukuru sana. Lakini niwashukuru pia Wabunge wote waliochangia hata wale ambao hawakuchangia lakini wametoa mawazo yao kwa namna moja ama nyingine, lakini hasa wale ambao walichangia sekta ya mifugo na uvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na hoja za Kamati, mojawapo ilikuwa ni Serikali iweke mazingira bora na kuhamasisha wananchi kufuga samaki. Suala hili la ufugaji wa samaki ni suala jipya. Tunakubali kwamba tutaendelea kufanya kazi hilo na Serikali tumejiandaa vizuri. Moja, tumeandaa miongozo mbalimbali inayoongoza suala lenyewe la ufugaji wa samaki, tuna miongozo ya namna ya kufuga au kutunza vifaranga; tuna miongozo ya namna ya kufuga samaki kwenye mabwawa; tunamiongozo ya namna ya kufuga samaki kwenye vizimba; na miongozo mbali mbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunajitayarisha vizuri kwa sababu wavuvi wetu hasa wanaotaka kufuga samaki kwenye vizimba wanapata shida hasa kwenye suala la environmental impact assessment Pamoja na NEMC. Sasa sisi tumesema tutagharamia na tutafanya kama Wizara, strategic environmental assessment kwenye maeneo ya upande hasa wa ziwa na bahari na maeneo yanayokubalika, halafu tutawajulisha wanaotaka kufuga samaki ili waweze kufuga samaki kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala hili la kufuga samaki pia tumesema tuanzishe vituo vipya viwili, vitakavyowezesha wananchi wetu kujifunza. Tuna vituo vipya vitano viko kule Lindi, Ruvuma, Mwamapuli pale Igunga, Kingorwila Morogoro na kule Chato na tumesema tunaongeza vituo vyangine viwili kule Mtwara na Dar es Salaam. Hivi vituo viwili vitakuwa ni special kwa ajili ya watu wa mwambao, kwa sababu mfugaji wa samaki kwa vizimba vya mwambao na kule ziwani tofauti kidogo, kwa hiyo tumeona tuanzishe vituo viwili. Mwaka wa fedha unaokuja vituo hivyo vitafanya kazi na wananchi walioko kwenye maeneo hayo watakwenda kwenye vituo hivyo ili waweze kujifunza namna ya ufugaji bora wa samaki jinsi ulivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumesema vile vile tutaendelea kutoa mafunzo mbalimbali kwa wafugaji wa samaki wa mabwawa na vizimba na maeneo mengine. Wataalam wetu wapo tayari kwenda na kutoa utaalam, mafunzo ili kwamba suala hili liweze kueleweka vizuri na wananchi waweze kuchukua hii kama fursa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu, suala la kufuga samaki ni suala rahisi sana na vijana ambao wako huko wanajaribu kuangalia wafanye kazi gani, wanaweza kuanza na hili kwa sababu hili ni eneo oevu sana na linaweza kuwapa kipato kizuri cha kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala lingine ambalo Kamati walitushauri walisema Serikali iweke mazingira yatakayowezesha usafirishaji wa mazao ya uvuvi. Tumejitahidi sana kwenye eneo hili, moja ya jitihada tulizofanya ni kupunguza tozo. Tulisema kwenye bajeti yetu tulipokuwa tunasoma hapa, tumepunguza tozo za aina mbalimbali ambazo tulizitaja kwenye bajeti yetu, sipendi kuzirudia hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo tulilizungumza na Kamati, ni Serikali iendeleze mapambano dhidi ya uvuvi haramu na kudhibiti utoroshaji wa mazao ya uvuvi, suala hili ni suala endelevu. Naomba Waheshimiwa Wabunge waelewe na wananchi ewelewe kwamba, uvuvi haramu haukubaliki kwa namna yoyote ile. Tunaendelea nalo lakini kwa namna ambayo itakuwa ni shirikishi zaidi. Tumezitayarisha halmashauri zetu pamoja Kamati za Ulinzi za Wilaya na za Mikoa, ili zishiriki kwenye jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili lilikuwa likichukuliwa kama ni suala la ngazi ya Wizara peke yake, lakini safari hii tunatakata twende pamoja kama Serikali moja. Kwa hiyo ndio maana mtaanza kuona Wakuu wa Wilaya wanasaka makokolo na Wakuu wa Mikoa wanatafuta wavuvi haramu na kuwapa adhabu kwa mujibu wa sheria. Sasa tunataka Serikali kwa ujumla tulivalie njuga suala hili ili ijulikane kwamba ulinzi wa rasilimali za mazao ya samaki ni wetu sisi wote. (Makofo)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niende kwenye masuala ya mifugo. Kamati walitushauri kwamba jitihada zaidi ziongezwe kupambana na magonjwa ya mifugo, hili ni suala ambalo pia ni endelevu, sisi tunaendelea kama Wizara. Moja tunajengea uwezo kituo chetu kinachozalisha chanji cha TVI kipo pale Kibaha, tumetenga kiasi cha shilingi bilioni 2.4 kwa ajili ya kuzalisha chanjo zaidi. Pia Wizara tumetenga kiasi cha shilingi bilioni 2.3 kwa ajili ya kujenga majosho katika maeneo ya wafugaji, hasa maeneo ambayo mifugo yetu mingi ipo. Kwa hiyo, tutajenga majosho kwenye maeneo ya Waheshimiwa Wabunge ili tujaribu kupunguza namna za magonjwa zinazosababishwa na kutoogesha mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tutanunua dawa za kuogesha hiyo mifugo. Tumetenga pesa kiwango fulani na tutafanya ukarabati wa clinic zetu mahali popote zilipo, tumetenga kiasi cha pesa kwenye bajeti yetu ili kwamba tuhakikishe angalau tuna clinic za mifugo kwenye maeneo yetu kuweza kutibu mifugo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo tumesema tutalifanya ni suala linalohusiana na mambo ya ugani. Kamati ilitushauri kwamba tuweke mazingira wezeshaji ya ufanyaji kazi kwa Maafisa Mifugo ili waweze kuzungukia mashamba na mifugo. Tulisema pia kwenye bajeti yetu, kwamba kwenye bajeti hii tumetenga kiasi cha pesa tutanunua pikipiki 300, kwa ajili ya Maafisa Mifugo ili waweze kutembea na kuwafikia wafugaji popote watakapokuwa. Mbali ya kuwanunulia vifaa hivi, pia tutafanya mafunzo rejea kwa ajili ya maafisa hawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mambo yaliyozungumzwa na ushauri uliotolewa ni mwingi. Niseme tu kwamba ushauri wote na hoja zilizotolewa tumezichukua tutazijibu kwa maandishi, ziko nyingi; kuna bajeti ya mifugo na uvuvi ni ndogo tumechukua, naomba tu watupe nafasi kwa bajeti hii tuliopewa waone tunafanya nini kwa mwaka ujao na si sasa hawatakuwa na sababu za kumdai Mheshimiwa Rais kutoongezea bajeti baada ya kufanya kazi ambazo tumepangiwa mwaka huu watakapotupitishia bajeti yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kusafirisha na kuuza mazao ya mifugo na samaki bado kweli ni kidogo tunakubali na tunataka tuongeze sasa uzalishaji kwenye sekta hizi zote mbili. Utagundua kwamba kazi zote tulizozitenga kuzifanya zinalenga kuogeza tija na uzalishaji kwenye masuala haya mawili.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la ulinzi na usalama kwa wavuvi na wafugaji. Suala hili linaihusu Serikali nzima na tutashirikiana na Kamati za Ulinzi za Wilaya na za Mikoa ili tuhakikishe ya kwamba wavuvi wanapokuwa baharini au wanapokuwa kule ziwani, wako salama na vifaa vyao na vyombo vyao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala lingine la miundombini ya mifugo, nimetaja baadhi. Pia lipo suala la mchango wa uvuvi kwenye pato la Taifa. Nadhani hili litaelezwa kwa kirefu sana na litaongelewa vizuri zaidi naMheshimiwa Waziri au Naibu Waziri wa Fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu zao la mwani ambalo linastawi kwenye mwambao wa pwani kuanzia Mtwara, Lindi, Dar es Salaam, Pwani kwenda mpaka Tanga. Suala hili tumelichukua vizuri na sisi kwenye bajeti ijayo tumetenga pesa mahususi kwa ajili ya zao la mwani kuhusiana na uzalishaji wake, soko lake na kuhusiana hasa akinamama wanaozalisha suala hili tuwatafutie vifaa vinavyoweza kuvuna zao hili kwa wingi. Kwa hiyo suala hili pia tumeliwekea maanani sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kuna suala la Ranchi za Taifa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushUkuru sana na naunga mkono hoja.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa nakupa dakika moja, malizia Ranchi za Taifa.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, suala la Ranchi za Taifa, tumelichukua na najua Waheshimiwa Wabunge hapo walishauri sana juu suala hili, lakini hata kwenye hoja hii limezungumzwa sana, tumelichukua na tunafanya tathmini, wategemee transformation kubwa kwenye Ranchi zetu za Taifa. Ahsante sana. (Makofi)