Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimpongeze sana Waziri wa Fedha na Mipango na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kwa kuwasilisha vizuri sana hotuba ya Bajeti Kuu ya Serikali na maoni ya Kamati.

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii imeelezea mapato na matumizi ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2021/2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti iliyowasilishwa ni nzuri na inalenga kulipeleka Taifa letu hatua moja mbele. Kwa mantiki hiyo, ninaiunga mkono.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kiasi kikubwa bajeti hii imeheshimu mawazo ya Wabunge katika michango yao toka Bunge la Kumi na Mbili lianze, isipokuwa kilio cha kuongeza bajeti ya kilimo na mifugo hakikuzingatiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti hii, Serikali imebainisha maeneo muhimu ya kipaumbele kwa mwaka 2021/2022. Kwa upande wa wafanyakazi, ninaipongeza Serikali kwa kupunguza kodi ya mapato ya ajira (PAYE) kwa wafanyakazi kutoka asilimia tisa hadi asilimia nane. Hatua hii kwa kiasi imewapunguzia wafanyakazi mzigo mkubwa wa kodi na kuboresha maslahi yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kuipongeze Serikali kwa kuboresha mazingira ya kazi kwa Madiwani na Watendaji wetu wa Kata. Serikali imeonesha nia njema sana ya kuzijali kada hizi zinazofanya kazi na wananchi katika ngazi ya vitongoji na vijiji.

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze pia Serikali kwa kutenga shilingi bilioni 328.2 kwa ajili ya kugharamia Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022. Zoezi hili ni muhimu sana kwenye kupanga maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika michango mbalimbali, tuliwasikia Wabunge wengi wakilalamikia tozo mbalimbali zilizokuwa zinawaumiza vijana wa Kitanzania waliokopa Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu. Naipongeza Serikali kwa kufuta tozo ya asilimia sita iliyokuwa ikitozwa kwa ajili ya kulinda thamani ya mkopo wa elimu ya juu kwa wanufaika.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine lililolalamikiwa na Wabunge ni watumishi kutokupandishwa madaraja kwa kipindi cha miaka mitano na zaidi iliyopita. Ninaipongeza Serikali kwa kutenga jumla ya shilingi bilioni 449 kwa ajili ya kuwapandisha vyeo watumishi 92,619. Hatua hii itawapa motisha na kuboresha maisha ya wafanyakazi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa muda mrefu kumekuwepo na changamoto za muda mrefu za ulipaji wa mafao kwa wastaafu kutokana na ufanisi mdogo wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii katika kuhudumia wastaafu wetu. Ninaipongeza Serikali kwa kuja na mkakati wa kulipa madeni yanayodaiwa na mifuko kwa kutenga fedha kwenye bajeti na kutumia utaratibu wa kutoa hatifungani maalum isiyo taslimu zitakazoiva kwa nyakati tofauti.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maelezo ya Waziri hatua hii inakwenda kumaliza kabisa tatizo hilo la wazee wetu kudai haki yao. Katika bajeti hii Serikali imependekeza kuwa kuanzia sasa wanataka kuanza kulipa michango hiyo moja kwa moja kutokea Hazina kwa taasisi zote ambazo watumishi wanalipwa na Hazina.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niipongeze Wizara kwa nia njema ya kufanya mabadiliko katika Kanuni ya 21 ya Sheria ya Bajeti ili kuondoa changamoto iliyopo ya fedha ambazo hazijatumika hadi tarehe 30 Juni ya kila mwaka kurejeshwa Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali. Mabadiliko haya yamekuja wakati muafaka na yatasaidia sana kwenye utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika idara mbalimbali za Serikali nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Waziri kwa kuja na mapendekezo ya vyanzo vipya vya mapato. Mimi naunga mkono mapendekezo yake na niwaombe Watanzania wote waelewe kwamba Taifa letu litajengwa na sisi wenyewe. Pendekezo la kulipia kodi ya majengo kupitia matumizi ya umeme (LUKU), tozo za simu na tozo za kutumia miamala ya fedha ni ubunifu mzuri. Hapa Serikali itaongeza idadi ya walipa kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika tathmini ya utekelezaji wa Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa ilithibitika kuwa kulikuwa na ushiriki kidogo wa sekta binafsi katika utekelezaji wa Mpango wa Pili. Kwa kiasi kikubwa utekelezaji ulifanywa na taasisi za Serikali. Hii ilitokana na tabia mbaya iliyokuwa imejengeka kwenye sekta binafsi ya kuuza huduma kwa bei kubwa. Kazi hiyo hiyo ilifanyika kwa bei ya chini sana na kwa kiwango kizuri kwa kuzitumia taasisi za Serikali. Katika Mpango wa Tatu, ninaishauri Serikali ishirikishe sekta binafsi kwenye utekelezaji wa Mpango wa Tatu wa Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, ninaishauri Serikali katika maeneo machache yafuatayo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, ninaishauri Serikali ishirikishe sekta binafsi kwenye utekelezaji wa miradi ya Serikali iliyopo kwenye Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa. Katika hili, sekta binafsi wahamasishwe na kuelekezwa wawe waaminifu kwenye kutoa gharama halisia za utekelezaji kwani wameshajifunza makosa waliyofanya siku za nyuma. Wakishirikishwa kikamilifu, watazalisha ajira, wigo wa walipa kodi utapanuka na mapato yataongezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, katika Bajeti Kuu ya Serikali ya shilingi trilioni 36.33; asilimia 29.3 (trilioni 10.66) zitatumika kulipia Deni la Taifa. Kiasi hiki ni kikubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaishauri Serikali ibuni vyanzo vipya vya mapato kwani wigo wa kukusanya bado ni finyu sana. Napendekeza ianzishwe tozo mpya kupitia malipo kwenye mita za maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, biashara ndogo ndogo zimepanuka sana na wengi huwa hawalipi kodi. Ninaishauri Serikali ibuni mikakati madhubuti ya kukusanya kodi kutoka kwa wafanyabiashara wadogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nne, ninaishauri Serikali iendelee na kuboresha mazingira kwa wawekezaji wa ndani na nje. Tukipata wawekezaji wengi, ajira, wigo wa kulipa kodi na mapato ya nchi vitaongezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, tano, Serikali inategemea kukopa shilingi trilioni 7.34 kutekeleza miradi ya maendeleo. Kati ya hizo, shilingi trilioni 4.99 zitakopwa ndani na shilingi trilioni 2.35 zitakopwa nje. Katika hili Serikali inapochukua mikopo mikubwa kutoka ndani (mabenki yetu), itakuwa inaminya sekta binafsi kukopa na kuziyumbisha. Sekta binafsi zikiyumba, ajira zitakosekana na wigo wa kulipa kodi na mapato kuathirika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sita, Wabunge wengi waliotoa mawazo katika michango yao, walishauri ufanyike uwekezaji wa kutosha katika sekta za uzalishaji (kilimo, mifugo, uvuvi, viwanda) na walipendekeza bajeti ya sekta hizi ziangaliwe kwa jicho la pili. Bahati mbaya, Serikali haikuzingatia maoni ya Wabunge wengi. Ninaishauri Serikali kwenye bajeti itakayofuata ya mwaka 2022/2023 iongeze Bajeti ya Kilimo na Mifugo kwani inaajiri asilimia 65 ya Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, saba, Serikali imelimbikiza madeni mbalimbali ambayo wazabuni wameshatoa huduma. Ninaishauri Serikali ilipe madeni ambayo uhakiki umekamilika. Kwa mfano, Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NMAIST) iliyoko Arusha ina deni (shilingi 6,007,562,000) lililohakikiwa muda mrefu, lakini malipo hayajafanyika. Ninaiomba Serikali isaidie kwenye hili ili shughuli za kukuza hii taasisi zisikwame.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo na ushauri wangu, naunga mkono hoja.