Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii nami niweze kutoa mchango wangu katika Wizara hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja naomba nianze na pongezi kwa Mheshimiwa Makamu wa Rais kwa kuendesha zoezi zima la uchangiaji wa damu. Katika ukurasa wa 57 wa kitabu cha hotuba ya Waziri imeonesha ni kwa jinsi gani Tanzania inahitaji damu salama kwa ajili ya wanawake wanaojifungua, lakini siyo tu wanawake wanaojifungua, pia na watu wote wanaokuwa na uhitaji wa damu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya hii Wizara, Naibu Waziri pamoja na timu nzima ya Wizara kwa hotuba nzuri ambayo wameiandaa na kuiwasilisha hapa, lakini pia kwa kazi nzuri ambayo inafanywa na Wizara hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la bajeti la Wizara hii. Kutokana na maelezo ya hotuba hii inaonesha kwamba, mpaka kufikia Machi mwaka huu ni asilimia 31 ambayo tayari Wizara hii ilikuwa imeshapelekewa. Pia kwa upande wa mishahara, inaonesha kwamba ni 4.1 billion ambayo ilikuwa imeshapelekwa kufikia mwezi Machi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa namwomba Mheshimiwa Waziri, atakapokuja atoe ufafanuzi kwamba hii mishahara kama imetolewa asilimia ndogo hivi, amesema kwamba ni asilimia 37, hawa wafanyakazi ni kwamba wanakopwa ama hawapo labda walipunguzwa ama labda bajeti ya fungu la mishahara lilikuwa kubwa ukilinganisha na wafanyakazi waliopo? Kwa hiyo, naomba ufafanuzi katika eneo hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nizungumzie suala la huduma ya saratani. Naipongeza Wizara kwa mipango yake mizuri kwa mwaka ujao wa fedha. Naomba niishauri Serikali kwamba huduma hii ni muhimu sana, lakini katika hii hotuba tunaona kwamba, kipaumbele kimepewa kwa Hospitali moja ya Ocean Road.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na uhalisia wa nchi yetu ya Tanzania ni kwamba, watu wengi ambao wanatoka pembezoni, hawana uwezo. Kwa hiyo, utakuta mtu anafariki kwa kukosa tu ile nauli ya kumtoa huko mahali alipo na kumpeleka Dar es Salaam kupata hii huduma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu anapokuwa mgonjwa anahitaji mtu wa kumsaidia, kwa hiyo, hapo inabidi mtu atafute nauli yake yeye mwenyewe mgonjwa na nauli ya mtu ya kwenda kumsaidia kule Dar es Salaam anapokwenda kupatiwa huduma hii. Kwa hiyo, naiomba Serikali kwamba hii huduma iboreshwe katika maeneo yote ya Tanzania ili watu wasiwe wanakufa kwa kukosa hata nauli ya kuwafikisha hospitali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niishukuru Serikali kwa ajili ya lotion kwa ajili ya watu wenye albinism. Huduma hii inapatikana KCMC. Naiomba Serikali ifanye mikakati ya kuwezesha upatikanaji wa lotion hizi kwa sababu imekuwa ikipatikana kikanda. Kuna baadhi ya maeneo lotion hizi hazifiki. Serikali ishirikiane na wadau mbalimbali kuhakikisha kwamba huduma hii inapatikana all over the country. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie pia huduma ya Mifuko ya Bima ya Afya. Sijui nitumie lugha gani rahisi, lakini niseme tu kwamba, Mifuko hii inabagua baadhi ya huduma, yaani baadhi ya gharama. Utakuta mtu ndiyo ameshamwona Daktari vizuri, anapokwenda kuchukua dawa, anaambiwa kwamba hii dawa haigharamiwi na Mfuko huu; ama kuna hili suala zima la vifaa saidizi kwa watu wenye ulemavu. Mifuko hii haigharamii vifaa saidizi kwa ajili ya watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, siwezi nikailaumu mifuko hii, nadhani ni zile sera na sheria ambazo zipo. Kwa hiyo, naiomba Serikali iangalie ni jinsi gani ya kubadilisha hizi sera na sheria ambazo zinatekelezwa na Mifuko hii ambayo inasababisha baadhi ya huduma kushindwa kutolewa na Mifuko hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niongelee suala zima la wazee. Kwenye hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri, imeongelea huduma bure kwa wazee. Tunaishukuru Serikali kwa huu mpango na huduma hii ambayo inaendelea, lakini naiomba Serikali iboreshe sana huduma hii, kwa sababu kuna kilio kikubwa cha wazee kwamba wanapofika pale hospitali, kuna baadhi ya huduma ambazo ni nyingi ikiwemo dawa, baadhi ya vipimo kwamba havipatikani kwa sababu tu kwamba, huduma ile inakuwa haipatikani mahali pale. Kwa hiyo, naiomba Serikali iboreshe na iangalie kwa jicho la pekee huduma bure kwa wazee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia, naomba niongelee suala zima la ukatili wa kijinsia. Katika ukurasa wa 89 wa hii hotuba inaelezea takwimu zilizopo, kwa kweli zinasikitisha. Naomba nitumie Bunge lako Tukufu kulaani vitendo vya ukatili kwa watoto pamoja na wanawake. Matukio ni mengi ambayo yameendelea kuripotiwa ya watoto kubakwa, kulawitiwa, lakini pia vipigo ambavyo vinawasababishia watoto hawa na wanawake ulemavu wa maisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisema namalizia, lakini bado points mbili. Pia naomba Serikali iangalie suala zima la Bima ya Afya kwa watu wenye ulemavu. Kuna msemaji ambaye ametoka kuongea hapa, alikuwa ameshanifilisi lakini naomba nami nitilie mkazo. Kundi hili kiukweli linahitaji Bima ya Afya. Ukiangalia ni kwamba hata mlo wa siku moja inakuwa ni tatizo. Kwa sababu katika kitabu hiki inaonesha kwamba Serikali itahamasisha watu wenye uwezo wa kuchangia Mifuko hii waweze kuchangia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukiangalia mtu mwenye ulemavu, anakuwa hana uwezo hata kupata mlo mmoja kwa siku. Kwa hiyo, naiomba Serikali huduma hii ipatikane bure kwa kundi hili la watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya machache, naunga mkono hoja na naomba kuwasilisha.