Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Mbulu Mjini nachukua nafasi hii kuungana na Watanzania wenzangu kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kulijaalia Taifa letu ustawi katika nyanja mbalimbali za kijamii, kiuchumi, kisiasa, kidiplomasia, hali inayotufanya kuwa kelelezo mbele ya mataifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naungana na Watanzania wote kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu wa Awamu ya Sita mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kupokea uongozi wa Taifa letu, hakika tumekuwa kielelezo mbele ya mataifa, nawaasa Watanzania wenzangu tumpe ushirikiano wa dhati na kumwombea kwa Mwenyezi Mungu amjalie ulinzi, baraka na mafanikio katika kuliongoza Taifa letu Eeh Mungu mjalie baraka zako za milele.

Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Jemadari wa Afrika na Mwana Mapinduzi na Mzalendo wa kweli, Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, viongozi na watendaji wote kwa jinsi tulivyotekeleza Ilani ya CCM ya mwaka 2015-2020 kwa kiasi kikubwa. Hakika tumwombee Hayati Mheshimiwa John Pombe Magufuli aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama Taifa mchango wake tuukumbuke daima, pamoja na viongozi na Watanzania wote waliotangulia mbele za haki.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba kutoa mchango wangu kwa Wizara hii ya Fedha kupitia Taarifa ya Hali ya Uchumi yam waka 2021/2022; kwanza Serikali itazame upya mfumo wa kukusanya kodi ya mapato kwenye taasisi za fedha hususan mabenki na mawakala wao kwani mara nyingi unapotoa hela kwenye ATM mbalimbali utaona ujumbe wa maneno kuwa hakuna huduma kwa sasa kwani mfumo huu utaikosesha Serikali kupata mapato yenye uhalisia. Sote tufahamu kuwa upatikanaji wa tozo na kodi kwenye miamala ya fedha ukidhibitiwa vizuri na Serikali tutapata mapato mazuri kwa kuwa kiwango cha riba na tozo ni mkubwa katika taasisi hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia TAMISEMI itazame mpango wa kutoa mafunzo ya Waheshimiwa Madiwani kufahamu majukumu yao katika kusimamia Halmashauri zetu nchini, kukusanya mapato ya ndani na matumizi ya mapato hayo, kushauri na kuhamasisha shughuli za maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaipongeza sana Serikali Kuu kwa azma yake ya kulipa posho za Madiwani kupitia mapato ya Hazina hivyo basi kuna sababu mahususi za kutazama fedha zilizopangwa awali kupata miongozo yake kwa Waraka kutoka TAMISEMI ili mchanganuo wake uwasilishwe kwenye kikao cha Kamati ya Fedha ya mwezi Julai kwa waraka badala ya maelekezo kwa fedha zile nyingi ili sehemu itakayobaki isaidie kuchangia miradi ya maendeleo kwenye kata na vijiji.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha Serikali iangalie kiwango cha posho ya vikao kwa Waheshimiwa Madiwani kwani kiasi cha shilingi 40,000 kwa Diwani wa Kata kuhudhuria kwa robo mwaka kwa kikao kimoja tu ni kidogo sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga hoja mkono kwa asilimia 100 na naomba kuwasilisha.