Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. PROF. MAKAME MNYAA MBARAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa ninaomba kuchukua nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kuniwezesha na mimi kutoa mchango wangu kwa maandishi kwenye hoja hii iliyopo mbele yetu ya Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2021/2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaipongeza sana Serikali yetu kwa kuondoa Kodi ya Ongezeko kwenye maeneo mbalimbali kwenye simu janja za mkononi (smart phones) HS Code 8517.12.00, vishikwambi (Tablets) HS Code 8471.30.00 au 8517.12.00 na modemu (modems) HS Code 8517.62.00 au 8517.69.00.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango alivyosema kwenye kitabu chake cha hotuba ya bajeti (ukurasa wa 29 mpaka 30) lengo kubwa la hatua hii ni kuhamasisha matumizi ya huduma za mawasiliano ili kufikia lengo la asilimia 80 ya watumiaji wa intaneti ifikapo mwaka 2025 kutoka asilimia 46 iliyopo sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, upenyaji (penetration) mkubwa wa simu janja, vishikwambi na modem ni muhimu sana kwa sababu zifuatazo; kwanza, wastani wa mapato kwa mtumiaji (avarage revenue per user (ARPU)) huongezeka kutokana na matumizi ya data kupitia vifaa tajwa hapo juu. Motokeo yake mapato ya makampuni ya simu huongezeka zaidi kutokana na utumiaji mkubwa wa data. Makampuni hayo yanaweza kupata faida zaidi na kulipa ushuru zaidi kwa Serikali. Aidha, simu janja na vifaa vingine tajwa hapo juu kwa ujumla hufanya maisha ya watumiaji katika Taifa lolote duniani iwe rahisi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, upenyaji mkubwa wa simu janja, vishikwambi, na modem huhamasisha uanzishwaji biashara mtando, huongeza utoaji wa huduma za jamii kama vile elimu mtandao, matibabu mtando na kadhalika. Kuongezeka biashara mbalimbali kupitia mtandao huongeza ushuru na mapato kwa Serikali. Aidha kuimarika kwa huduma za jamii kutapunguza umaskini nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, tafiti mbalimbali duniani zinaonesha ya kuwa ongezeko la matumizi ya simu janja na matumizi ya Mkongo wa Mawasiliano kwa asilimia 10 hukuza Pato la Taifa kwa asilimia 1.2, huongeza ubunifu, tija katika maeneo ya kazi na ajira. Kwa hiyo hatua hii ya Serikali ya kuondoa kodi ya ongezeko kwenye vifaa hivyo ni ya kupongezwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiopingika kuwa Serikali yetu kwa miaka mingi imekuwa ikifanya jitihada za makusudi kupunguza bei ya bando (gigabit kwa sekunde (GB)) kwa dhamira ya ujumuishaji wa kidijiti na kukuza uchumi wa kidijiti nchini. Kwa bahati mbaya matokeo chanya hasa wananchi wa kipato cha chini na wananchi wa vijijini hayajafikiwa. Ninaendelea kuishauri Serikali yetu sikivu iendelee kupunguza bei ya bundle ili wananchi wote wa mijini na vijijini na wenye vipato vya chini waweze kufaidika na TEHAMA na uchumi wa kidijiti. Aidha, Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali iendelee kuwekeza kwenye mindombinu hasa maeneo ya vijijini ambako ndio kwenye Watanzania wenye kipato cha chini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuchangia. Mwisho ninaunga mkono hoja hii iliopo mbele yetu.