Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante nashukuru. Awali ya yote napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu; kwanza kabisa kwa kuniona wa maana kwa kunipa nafasi ya leo adimu. Zimebaki siku tisa turudi majimboni. Kwa kuwa umenipa msaada mkubwa wa kuweza kuishauri Serikali ninaomba nijikite kuishauri Serikali maana muda hautoshi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali kwa jinsi tulivyopanga hapa bajeti vizuri, kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu Nchemba pamoja na Naibu Waziri kweli bajeti imekaa vizuri sana. Nimeisoma, ina page 98 na nimesikiliza michango mingi ya Wabunge karibia yote inafanana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilikuwa na mawazo tofauti. Kwanza nianze na suala la milioni 500 zilizotolewa na Mheshimiwa Rais kwa ajili ya kila jimbo. Neno la Mungu linasema “Watu wangu wanaangamia kwa kukosa maarifa.” Hii milioni 100 ni kilometa moja, milioni 500 ni kilometa moja. Nimeuliza kwenye makampuni yanayouza makatapila; kuna catepillar excavator zinazouzwa na Wachina mpaka milioni
350. Mimi nilikuwa naona kwa mawazo yangu kwenye jimbo langu, kwa kuwa lina matatizo makubwa ya barabara; mngeturuhusu kila Mbunge tukatoa mawazo nikapata excavator la milioni 400 au 350 nikabaki na milioni 150 kwa ajili ya kuweka mafuta ningeweza kutengeneza barabara zaidi ya kilometa 50 na kuendelea na caterpillar likabaki. Halafu hilo caterpillar si kwamba ni la kwangu, ikiwezekana liandikwe Mama Samia Hassan Suluhu, Rais wetu, ni mtu mwema sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine naishauri Serikali, Waheshimiwa Wabunge watu wanataka mabadiliko wako serious. Na mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano Mungu amuweke mahali pema peponi; alitunadi kwa nguvu kubwa, na wengine tulishinda hatukuwa na sifa za kushinda; na kuna wengine walishindwa kwenye uchaguzi hawakuongoza katika kura za maoni. Lakini sasa hivi niseme tu nasikitika sana, kuona nchi tena inataka kurudi kwenye upigaji. Kuna watu ndani ya Serikali hawana mapenzi mema na wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamshauri Mheshimiwa Rais awe na maamuzi magumu kabisa katika hilo, wala asione huruma. Leo nimeshuhudia akiwaapisha Wakuu wa Wilaya na wengine kuwahamisha vituo, kama alivyofanya kwa Mawaziri. Lakini ukweli utabaki kuwa ukweli, watu wale ambao wanatuhumiwa na CAG pamoja na halmashauri zingine ambao wanaonekana kabisa wamekula pesa Serikali ichukue maamuzi magumu, na kwa kufanya hivyo itakuwa na sisi inatusaidia Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye upande wa bodaboda Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba bodaboda takriban nchi nzima wanakupongeza sana. Lakini kuna sehemu ya wenyeviti wa vijiji pamoja na vitongoji; Wabunge wengi wameongea na mimi naomba nikazie hapo. Haiingii akilini mtu aliyekuwa ananifungulia mikutano yangu ya Kampeni hana hata shilingi elfu 10 kwenye Taifa ya Tanzania. Mtu huyu ambaye mimi nasimama kumuongoza Kikatiba, kwamba inatakiwa kuwasomea mapato na matumizi wananchi katika michango ya kawaida, hana hata senti 100. Ni suala la kujiuliza haraka haraka bila hata degree, unalijua kabisa suala hili si zuri. Kwa maana hiyo ukija hapa ninakuomba ujaribu kuwaingiza hawa watu ili na wao waweze kupata posho. Tunaposema Tanzania ina mali nyingi angalau na wao at least kwa mwezi wawe na hata 100,000. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la MSD. Wabunge wengi wanazungumzia suala la afya, na mimi nimekuwa msumbufu sana hapa Bungeni. Nikiangalia takwimu za mwaka 2018 kwenye halmashauri yangu Mbogwe zilitengwa milioni 600 na zilikwenda; lakini cha ajabu nawauliza waliokuwa kwenye system hizi fedha hazikufika ilhali Serikali mpo na wasaidizi wa Rais mpo.

Mheshimiwa Naibu Spika lakini nimshukuru kaka yangu ambaye ni Naibu Waziri alifanya ziara kwenye hospitali zangu na akaona changamoto zilizopo. Nikuombe radhi sana Mheshimiwa Naibu Waziri juzi kwa kumuuliza swali la kushtukiza Mheshimiwa Waziri Mkuu na ukaelekeza mamlaka kwamba watanijibu TAMISEMI lakini ninahitaji hilo zoezi kwa sababu wananchi wa Mbogwe bado wanaendelea kupata shida, akina mama wanakufa katika harakati za kujifungua, bodaboda wamekuwa wakipata ajali wanakosa vipimo kama X-ray pamoja na mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niwaombe watu walio ndani ya Serikali, bajeti hii ni nzuri sana; lakini usiwe mchezo kama wa sarakasi, kama Kanumba na Ray. Tunaweza tukawa tumepitisha bajeti ya kila Idara, na uzuri nimechangia sekta nyingi sana; nimechangia kilimo, bajeti ya madini, na kila ukisoma jinsi Mawaziri mlivyo-introduce, kwamba mtafanya nini, iwe hiyo kweli. Lakini isiwe tu kwamba mmetukaririsha kwamba mtawasaidia kwa mfano wachimbaji wadogo halafu kusiwe na kitu, mtawasaidia wakulima kuwe hakuna kila kitu, tutaonekana watu wa ajabu sana. tukiangalia humu ndani tumo wa Chama kimoja; Mheshimiwa Marehemu aliliona hili baada ya Bunge la Mwaka 2015 kuwa na mivutano ambayo haikuwa na sababu; akaona achague watu wa kumsaidia ambao…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Maganga, hebu twende vizuri kidogo. Hili Bunge halina chama kimoja vipo vyama vingine humu ndani.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante naomba kurekebisha tupo vyama vingi pamoja na mchanganyiko lakini wengi wetu tupo Chama Tawala. Kwa maana hiyo mimi nawashauri Waheshimiwa Wabunge, tusije tukamsaliti Marehemu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho naomba nizungumzie kuhusu manung’uniko ya Waheshimiwa Wabunge. Maslahi ya Wabunge yapo kidogo sana; na mimi wakati bado sijaingia humu nilikuwa nafikiria kwamba kuna posho za kutosha. Nimeangalia mabunge mengine kama vile Afrika Kusini pamoja na Kenya na mabunge mengine wanalipa kwa dola. Tusiwaogope wananchi lazima tuwe wakweli tuwaambieni wananchi huku kwenye Ubunge hakuna kitu. Tumekuwa tukitukanwa kwenye mitandao; tumekuwa tukitukwanwa kwenye mitandao, na mimi hii kazi niliiomba kabisa kwa roho yangu moja; na mimi nitasema ukweli daima fitna kwangu mwiko. Fedha inayolipwa posho hapa haitoshi, mishahara haitoshi, mimi ninayeishi na wananchi hakuna kitu kinachoendelea.

Kwa hiyo hilo Serikali iliangalie upya ili nasi tufananane na mabunge mengine, tusiwe wajanja wajanja. Ninaujua utapeli wa kila aina lakini sitaki niwe tapeli kwa wananchi, wananchi wajue kwamba wana Mbunge mwenye fedha kumbe hakuna kila kitu. (Makofi/vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo bado siku tisa, nirudi jimboni…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana mheshimiwa…

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA:…wananchi wanajua Mbunge wao anarudi na fedha. (Makofi)

NAIBU SPIKA:…kengele imeshagonga.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi/Kicheko)