Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Grace Victor Tendega

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyikiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia katika Bunge hili. Kwa sababu ni mara ya kwanza na mimi kuchangia katika bajeti napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha kuweza kuja humu kuwakilisha akina mama wa Mkoa wa Iringa. Napenda pia kushukuru chama changu ambacho pia kimeniwezesha kuwa Mbunge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nichangie kwa kuanza na kitabu cha Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 89, ukatili wa kijinsia. Kumekuwa na matatizo mengi, kumekuwa na ukatili wa kijinsia ambao unafanyika katika nchi yetu na hasa waathirika wa tatizo hilo ni wanawake na watoto. Tumeona wanawake wengi wanafanyiwa ukatili wa kinyama, tumeona watoto wetu wanafanyiwa ukatili wa kinyama, tumeona watoto wanachomwa moto, tumeona watoto wanamwagiwa maji ya moto, tumeona madhara mengi kwa watoto wetu wa nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri ameeleza katika hotuba yake kwamba wataendelea kusimamia sheria, sheria zipo Mheshimiwa. Kama zipo na matukio yanaendelea kuna tatizo kubwa katika nchi hii la usimamizi wa sheria. Nikuombe Waziri unapokuja kuhitimisha hoja zako uweze kutueleza usimamizi huo utakuwaje tofauti na mazoea ya siku za nyuma ambayo yalikuwa yakiendelea ambapo akina mama wengi wananyanyasika, watoto wengi wananyanyasika, watoto wamekosa kabisa wa kuwasemea, tumeona watoto wanafichwa kabisa ndani kwa miaka kadhaa. Inatia uchungu kwa sisi wazazi ukiona matukio yale yanaendelea katika nchi hii ambayo tunasema ina amani na utulivu. Mheshimiwa Waziri tunaomba uweze kulisimamia na kwa sababu ni mwanamke mwenzetu basi uchungu huu najua unao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende katika masuala ya afya kwa ujumla. Tukiangalia bajeti ambayo imetengwa kwa Wizara hii, asilimia ambazo waliomba 100 wao wamepewa asilimia 11, hivi tutatekeleza kweli haya yote? Ndiyo maana wenzangu waliotangulia wanasema wanamuonea huruma Waziri kwa sababu matatizo ni mengi, mahitaji ya afya ni mengi huko kwenye Wilaya na majimbo yetu kuna matatizo lukuki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nikizungumzia katika Wilaya ya Iringa, Jimbo la Kalenga, tumekuwa na shida kubwa ya huduma za afya. Zahanati wananchi wamejenga, ukienda Wasa wamejenga zahanati lakini hakuna madaktari na manesi wananchi wanatoka kule kuja hospitali huku Ipamba ambapo ni mbali. Watu wanatoka Kata ya Magulilwa na kata mbalimbali kwa sababu hakuna hospitali za kuwahudumia na wakifika pale wanapata shida kwa sababu dawa lazima wanunue na dawa ni gharama na wakati mwingine hazipo. Kwa hiyo, kumekuwa na changamoto kubwa sana katika hospitali zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Mheshimiwa Waziri aweze kutupa majibu hizi changamoto zitatatuliwa lini, huu upungufu wa madaktari na wataalam katika maeneo yetu utakwisha lini? Hawa wananchi wameweza kujitolea kujenga majengo lakini mengine yamekaa kama magofu hakuna madaktari wala dawa. Serikali hii mnasema ni sikivu lakini watu wanapotea na tunasema afya ndiyo mtaji wa kwanza kwa jamii yetu. Sasa kama Serikali hii ambayo mnasema ni ya viwanda kwa sasa hivi, je, hivyo viwanda vitaendeshwa na watu wasio na afya bora. Tunahitaji kuwekeza kwenye afya ili tupate Watanzania wenye fikra bunifu za kuweza kuwekeza huko kwenye viwanda. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri uweze kuja na majibu ya masuala hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwa upande wa wazee, huko ndiyo kabisa. Tunashuhudia wazee wetu wakipata shida hospitalini. Hii Sera ya Wazee kupata huduma ya afya bure haitekelezeki, hawapati dawa. Wazee wanakwenda hospitalini wale wahudumu wetu madaktari na manesi wanatoa maneno ya kashfa kwa wazee wetu, inatia uchungu. Wazee hawa wameifanyia kazi kubwa nchi hii, wameweza kufanya mambo mengi kwa nchi hii lakini sisi hatuwalipi hata fadhila ya kupata dawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, unakuta ni rahisi kwa nchi yetu na Serikali hii ya CCM kuitisha mkutano wa wazee Dar es Salaam, lakini mara nyingi haiwezi ikawatimizia ahadi zao. Ni rahisi sana wakawa wamewekwa sehemu wazee wasikilize lakini kutimiza ahadi zao inakuwa ni ngumu. Tukuombe Mheshimiwa Waziri uweze kutuambia hawa wazee matibabu bure yatapatikana lini? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwa huduma za afya kwa watu wenye ulemavu. Mara nyingi tupo nao, tukiwa kwenye foleni hospitalini mnawaona hawa watu hawapewi kipaumbele kama inavyotakiwa. Hawa watu wanahitaji kuhudumiwa kwa ukaribu. Mimi nikuombe tu Mheshimiwa Waziri kwenye hitimisho lako hawa watu ikiwezekana wapewe bima ya afya ili waweze kutibiwa kwa bima ya afya. Kwa sababu wanapata shida sana, wengine hata hawajiwezi, hawajui wapate wapi pesa ya matibabu, hawajui wataendaje hospitalini lakini hawahudumiwi! Tunaomba wapate bima ya afya kwani itawaokoa wao kuweza kutibiwa na kuweza kuwa kama watu wengine kwa sababu na sisi ni walemavu wa kesho, hakuna ambaye sio mlemavu, ikitokea itakuwa ni bahati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende sasa katika Mfuko wa Bima ya Afya. Mfuko wa Bima ya Afya huko ndio kabisa, ukimgusa mwananchi huko kijijini ukamuelimisha anakuelewa lakini anakuja na swali tukienda hospitalini watu wenye kadi za bima ya afya wanatengwa, hawapati huduma haraka, wananyanyapaliwa sana, hii adha itaisha lini? Unakuta mtu ana bima ya afya lakini akienda pale wanasema tunahudumia kwanza wanaolipa cash wengine mtasubiri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie na WAVIU wale Watu Wanaoishi na Virusi vya UKIMWI …
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante sana.