Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi uliyonipa. Kwanza kabisa naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze Serikali ya Awamu ya Sita, kwa muda mfupi ililyoanza kufanya kazi imefanya mambo mazuri sana, imewatia moja sana Watanzania. Tulifika mahala watu walikuwa na hofu totauti tofauti lakini sasa kwa awamu hii ya sita matumaini yamerudi kwa kasi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Waziri Dkt. Mwigulu Nchemba, nimpongeze engineer Masauni pamoja na wataalamu wa Wizara hii, mmefanya vizuri sana, niwapongeze sana sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishukuru Serikali kwa fedha waliyotowa. Kwa muda huu mfupi fedha nyingi imekwenda kwenye majimbo yetu. Tumepata fedha kwa ajili ya madarasa pamoja barabara na vilevile tutapata fedha za shule mpya. Kwa jimbo langu mimi niseme tu kata sita hazikuwa shule kabisa, lakini sasa tunamatumaini ya kwenda kupata shule hizi mpya. Ahsanteni sana Serikali hii ya Awamu ya Sita.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nishukuru sana kwa wazo lile la kuwalipa Madiwani moja kwa moja kutoka Serikali Kuu ilikuwa ni kilio kikubwa sana cha Madiwani, hasa Madiwani wa halmashauri yangu ambao waliniletea kero nyingi sana. Na kabla sijapeleka kwa Waziri, Waziri ameliona hilo na tayari ametoa ufumbuzi. Ombi la Waheshimiwa Madiwani, wanasema tunashukuru sana lakini wafikiriwe kuongezewa kidogo, waongeze kidogo pale. Tunafahamu Madiwani wana kazi kubwa, wakiamka asubuhi wale ndio wanaokuwa na wapiga kura wetu, muda wote wanao shida zote wanazo, lakini wanafanya hivyo kwa namna mungu anavyowasaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nishukuru sana sana Serikali kwa maamuzi haya ambayo Mheshimiwa Waziri kupitia bajeti hii alituambia hapa. Ninamatumaini makubwa sana kwamba zahanati zangu, maana tutulikuwa na maboma ya zahanati zaidi ya 34; kwa maneno aliyosema Waziri hapa sasa yanaenda kukamilika. Nilivunjiwa madaraja zaidi ya 24 wakati mvua hizi zilizopita. Sasa kupitia mpango ule wa TARURA ninauhakika yanaenda kujengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa tunashida ya kero ya hospitali sisi tulikuwa hatuna hospitali sasa hivi tumepokea milioni 500 ujenzi umeanza nina uhakikia kwa mipango hii hospitali ile inaenda kukamilika mapema iwezekanavyo; pamoja na mambo mengi mazuri, kama vile mikopo kwa wanafunzi, tulikuwa tunashida na wanafunzi, na mimi kama Mbunge nasomesha baadhi ya wanafunzi, lakini sasa najua kupitia mikopo hii aliyotuambia Mheshimiwa Waziri hapa sasa na mimi Mbunge hapa nitapumua, nitafanya mambo mengine. Niishukuru sana Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hivi naomba nishauri kidogo. Tumefanya vizuri kwa upande wa Madiwani lakini kiko kilio kikubwa kwa upande wa Wenyeviti wa Serikali za Mitaa na Wenyeviti wa vijiji. Niliona mahala fulani kwenye halmashauri zenye uwezo, ziliwahi kufanya kitu wakati fulani. Ninafahamu Serikali yetu, Serikali Sikivu, inaweza kufanya kitu kwa wenyeviti hawa wa vijiji. Kama halmashauri za manispaa ziliweza kulipa 50,000 kwa mwezi kwa wenyeviti wa mitaa ninauhakika tukipanga tukiamua tunaweza kuwalipa kitu fulani wenyeviti hawa wa vijiji, Kwa hiyo nikombe Mheshimiwa Waziri utakapohitimisha basi wape matumaini wenyeviti wetu wa vijiji nawao wapate kitu fulani, inawezekana kwa mwezi hata kwa miezi mitatu mitatu kwa kuanzia ikibidi tufanye kitu fulani kwao.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kwa upande ule wa fedha za majumuisho; tumepeleka fedha milioni 500 kwa kila halmashauri kwa kila jimbo. Hata hivyo, yapo majimbo yenye ukubwa wa kipekee. Inatakiwa majimbo haya pamoja na kuwapa hizi milioni 500 tuyafikirie Zaidi, kwa sababu hatuwezi kufanana, hata vidole hivi havifanani. Yako maeneo yamefika mahala pazuri, lakini yako yana majimbo makubwa sana. Tukisema tumetoa tu milioni 500 na tukapiga makofi kwa kweli zile fedha zinaweza zisionane kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kwa mfano ile milioni 500 naenda kuendeleza ujenzi wa barabara ya kutoka Mbiga – Litoo hadi Ngumbo kwa Mheshimiwa Stella Manyanya, ni barabara ya TARURA, tulipata msaada pale tumejengewa kilometa 34 34 kwa kiwango cha lami, lakini sasa zimebaki kilometa 14, kwa hiyo tunaenda kuendeleza kilometa moja; unaweza ukano. Na hii ni barabara yenye kilometa nyingi sana ndani ya jimbo. Kwa hiyo ombi langu kwa Serikali, pamoja na kutoa fedha hizi tuyaangalie majimbo makubwa, tuyaongezee fedha ili zikafanye vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo hivyo kwa upande wa…

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Benaya Kapinga kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Jacqueline Msongozi.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara anayozungumzia Mheshimiwa Benaya ambayo imebakiza kilometa 14 kujengwa kwa lami inayopita kwenye Ukanda wa Ziwa Nyasa ambako kuna vivutio vingi vya utalii na vivutio vingi vya asili; mimi nilikuwa tu nataka nimuongezee mchangiaji kwamba, ni vizuri sasa Serikali ikatenga pesa kwa ajili ya kumalizia kilometa 14 badala ya kutoa kilometa moja. Kwa sababu kilometa moja inakuwa haina tija labda wangetoa pesa za kilometa 14 ingeleta tija zaidi. Ahsante. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Benaya, malizia mchango wako.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naipokea taarifa yake kwa mikono miwili, nakushukuru sana dada yangu Msongozi.

Mheshimiwa Naibu Spika, na barabara hii mwezi wa kwanza tulipokwenda hata Mheshimiwa Waziri Mkuu aliitolea maelekezo, kwamba ikamilike kwa sababu ina muhimu mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nitoe ushauri upande wa kilimo. Wananchi wa nchi wamefanya vizuri sana kufikia hapa tulipofikia, kiasi kwamba kwa kiasi kikubwa Tanzania haina njaa. Wakulima wetu wamefanya kazi wenyewe kwa nguvu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukifuata taarifa za bajeti hapa upande wa huu wa kilimo hatukufanya vizuri sana, tuwe wa kweli, hatukufanya vizuri sana. Fedha zinatengwa lakini zinazokwenda ni kidogo sana, na hii ipo tofauti na nchi Jirani. Hata kwa bajeti hii tunayoijadili nchi za wenzetu kwa upande wa kilimo zimefanya vizuri zaidi kuliko sisi. Unaweza kuona Kenya wao wametenga trilioni 1.2 kwenye kilimo, Uganda wametenga almost hela ya kwao trilioni 45…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie dakika moja tu.

NAIBU SPIKA: Sekunde thelathini.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Rwanda pia wametenga fedha nyingi, sisi Tanzania tupo chini kuliko nchi za wenzetu. Kwa hiyo nikuombe sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha, kwamba bajeti inayokuja tufanye mambo makubwa, fanya, weka alama kwenye kilimo ili taifa hili likukumbuke. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, nakushukuru sana.