Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Michael Mwita Kembaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia katika bajeti yetu hii ya mwaka 2021/2022. Nichukue nafasi hii kumpongeza Rais wetu, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea bajeti ambayo kwa kweli imekoza kila mtu. Imegusa wafanyabiashara, wamachinga, wakulima, wafanyakazi, wafugaji na wavuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi ya yote, Mheshimiwa Rais wetu Mama yetu ameweza kufanya jambo lingine la kipekee kwa kutoa shilingi milioni 500 kwa kila Jimbo. Tayari fedha ile imeingia, nimefanya mazungumzo na Meneja wa TARURA kuongeza Kilometa moja ya lami katika Mji wetu wa Tarime Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nitakuwa sina fadhila kama sitampongeza na kumshukuru kwa shilingi milioni 600 kwa ajili ya ujenzi wa Sekondari katika Jimbo letu la Tarime Mjini ambapo tulikuwa hatuna Sekondari katika Kata ya Saba Saba, sasa inakwenda kujenga. Nampongeza na ninatoa shukrani sana kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile napenda kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu wake pamoja na watalaam wote katika Wizara ya Fedha kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya, kuhakikisha kwamba wanatuletea bajeti ambayo imeshiba. Hongera sana Mheshimiwa Dkt. Nchemba pamoja na Naibu Waziri Mheshimiwa Engineer Masauni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kutoa mchango wangu kwa upande wa tozo au ushuru kwa bidhaa zinazotoka nje. Ukienda katika nchi jirani ya Kenya unapokuwa unatoa bidhaa hapa unapeleka Kenya, kwa mfano kama sasa hivi juice hizi za Azam zinavuka sana kwenda Kenya, wewe unavusha tu hamna usumbufu wowote unaopatikana katika upande ule. Wafanyabisahara wanaovusha bidhaa zile wanapita custom kawaida, wanapita wanalipa ushuru na bidhaa zao wanafanya biashara kama kawaida.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukitolea mfano mwingine ng’ombe wanatoka Tanzania kwa wingi sana wanapita tena pale mpakani bila shida yoyote wanavuka na wanaenda wanauza bila shida yoyote. Sababu kubwa inayosababisha biashara hii iweze kufanyika vizuri ni kwa sababu ushuru wa Kenya uko chini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuchukue mfano katika Mji wetu wa Tarime nyumba zinajengwa kila siku, wakati wanajenga wanatumia simenti, mabati, misumari, na kadhalika lakini sasa tuchukulie mfano wa simenti inayozalishwa Tanzania inauzwa shilingi 22,000 mpaka shilingi 24,000 ilhali simenti ambayo inatoka Kenya inauzwa shilingi 16,000 mkapa shilingi 17,000, sasa kwa mkulima au mtu wa kawaida pale Tarime kununua simenti shilingi 22,000 na huku anajua kwamba, kuna simenti hapa inauzwa shilingi 17,000 inakuwa ni ngumu kidogo. Nini kinafanyika sasa?

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachofanyika sasa vijana wanaamka wanaanza kufanya wanapita njia panya road kupitisha ile simenti na matokeo yake Serikali inapoteza mapato makubwa sana. Mimi ningeshauri Serikali waangalie, wajifunze kutoka katika nchi ya Kenya walifanyaje ili wafanyabisahara waweze kulipa kodi kwa hiyari badala ya kufukuzana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pale kuna vifo vinatokea mara kwa mara pale na hivi vinatokana na vijana ambao wanasomba hizi bidhaa au magendo kutoka nchi ya Kenya kuanguka au kugongwa pale ambapo wanafukuzana, hii inatokana na kwamba, anapopita alipe ushuru kawaida ushuru ule unakuwa ni mkubwa zaidi kiasi kwamba, hawezi kupata faida, lakini iwapo kama ushuru huu ungekuwa wa kawaida kama nchi jirani…

MHE. ABDULLAH ALI MWINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kembaki kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Abdullah Mwinyi.

T A A R I F A

MHE. ABDULLAH ALI MWINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Ningependa tu kumpa taarifa mchangia mada taarifa ya kwamba, simenti ya Kenya kwa mujibu wa Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ikija Tanzania haitozwi kodi na simenti ya Tanzania ikienda Kenya haitozwi kodi, taarifa.

NAIBU SPIKA: Haya, ahsante sana. Mheshimiwa Kembaki unapokea taarifa hiyo?

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu mimi naona inatozwa na ndiyo maana wanafukuzana. Kwa hiyo, nikipokea na ilhali kuna kufukuzana na inakamatwa na hivi juzi punde tu TRA imegawa zaidi ya simenti 150 kwa shule za sekondari na msingi ambazo zimekamatwa kutokana na hii biashara ambayo wafanyabiashara ambao wanafanya magendo katika barabara hii ya Sirari.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, sipokei hiyo taarifa. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Sasa ili taarifa zetu rasmi za Bunge zikae vizuri, hao wamepokonywa kwa sababu ya kodi au wamepokonywa kwa sababu ya magendo?

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu wananunua simenti Kenya wanaileta Tarime. Kwa hivyo, wakati wanaleta wanakamatwa.

NAIBU SPIKA: Wanaileta kwa njia ya magendo ama wanaileta kwa njia halali?

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, wanaileta kwa njia ya magendo, kwa jina maarufu njia za panya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, kwa njia hii kumbe kuna haja ya Serikali kutoa elimu kwa wafanyabiashara elimu ambayo itasaidia wafanyabiashara kujua hizi namna ya kupitisha au namna ya kuagiza bidhaa kutoka nchi nyingine ili kuepuka ukwepaji kodi au hii bidhaa kupita kwa njia ya magendo. Ukweli ni kwamba, Serikali ikifanya hivi kwa kutoa elimu ya kutosha pia kuhakikisha kwamba, hizi tozo au ushuru unakuwa wa chini kwanza itahamasisha watu kulipa kodi wenyewe kwa hiyari, lakini pia itasababisha Serikali kupata mapato yake bila usumbufu wowote ikilinganishwa kwamba, mipaka ya nchi yetu na wafanyakazi walioko TRA hawatoshi kudhibiti haya mazingira ya ukwepaji au utoroshaji wa bidhaa ambazo zinaingia nchini. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa pia, Serikali ifanye utafiti wa kina ni kwa nini viwanda vyetu au bidhaa zinazozalishwa nchini zinauzwa kwa bei ya juu ikilinganishwa na bidhaa zinazotoka nje. Bila kufanya hivi bado ukwepaji kodi utaendelea, vilevile hatutapata suluhu ya nchi yetu kuwa tegemezi. Ningependa sana utafiti huu ufanyiwe kazi na baada ya utafiti huu kupatikana tutafute majibu namna gani tunaweza kutatua changamoto hizi ambazo zinasababisha bidhaa zinazozalishwa nchini kuuzwa kwa bei ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi. Ahsanteni sana, naunga mkono hoja. (Makofi)