Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. John Michael Sallu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Handeni Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. JOHN M. SALLU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Kwanza nianze na shukrani. Naishukuru sana Serikali yetu sikivu. Namshukuru sana mama kwa kuja na bajeti hii bajeti sikivu. Hapa nipende kumpongeza ndugu yangu Waziri, Mheshimiwa Mwigulu, Naibu wake na watendaji wote walioko chini yake kwa kuandaa bajeti hii Sikivu, iliyosikiliza mawazo mengi ya Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli namshukuru sana mama kwa jinsi ambavyo ametukumbuka kwenye barabara. Sisi wa vijijini kwa kutuongezea zile hela za TARURA zimetusaidia sana na zitasaidia sana kusisimua maendeleo ya kilimo kule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najikita zaidi kwenye kilimo kwa sababu Jimbo langu linashughulika zaidi na kilimo, kwa hiyo, katika ile asilimia 65 ya watu wanaoshughulika na kilimo na jimbo langu tumo. Kwa kweli asilimia moja ya bajeti ni ndogo sana kwa kilimo, kwa sababu kilimo kwa sababu kilimo kimebeba asilimia 65 ya wananchi. Ili tuweze kupata maendeleo kwenye nchi yetu, tunahitaji asilimia 65 ya wananchi kuisisimua ili iweze kulima kwa tija. Ili iweze kulima kwa tija tunahitaji Maafisa Ugani wa kutosha pamoja na mbinu za kuwaelimisha ili waweze kulima kwa tija kwani mazao yanayopatikana sasa hivi ndani ya heka moja yako chini sana hayana tija. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile katika kusisimua wakulima hawa soko ni muhimu sana la ndani na nje. Soko la ndani linaweza kusisimuliwa zaidi kwa kuwa na mbinu za kutengeneza viwanda vidogo vidogo ambavyo vitaleta tija ya ku-add value, kuongeza thamani mazao yetu. Kwa hiyo, taasisi husika zinatakiwa hapa Serikali iziangalie kama alivyosema mwongeaji aliyepita, kuna hizi CAMARTEC watakiwa waje na mbinu ya kuhakikisha kwamba tunapata viwanda vidogo vidogo ambavyo vitasaidia kusisimua uchumi kule vijijini. Uzuri ni kwamba ndugu zetu wa REA wamejitahidi umeme unaenda kila mahali, kwa hiyo sasa ni jukumu la viwanda hivi kusisimuliwa ili viweze kuleta tija kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, soko la nje ndugu zetu wa TANTRADE wanajitahidi, naomba na sisi wafanyabiashara tujitahidi kutafuta soko la nje kwa kadri iwezekanavyo kwa sababu ukiangalia wenzetu jirani wanauza sana nje mazao yetu sisi. Mazao yetu mengi yanapitia Kenya. Kwa hiyo hapa kuna jambo la kujifunza. Kwa mfano, kilimo cha mbogamboga na matunda ambapo kwenye jimbo langu tuna eneo kubwa sana wanalima machungwa na maembe pamoja na mbogamboga, kata takribani 14. Hapa nashauri lijengwe soko la matunda pale Segera ili liweze kurahisisha matunda haya kukusanywa na kuweka soko la Kimataifa pale ambapo litakuwa na majokofu ya baridi kwa ajili ya matunda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa napo pana kitu cha kujifunza kwa sababu baada ya kukusanya na kununua mazao haya ya matunda na mbogamboga tunatakiwa tuyapeleke nje, lakini bandari zetu bado hazijawa imara kusafirisha mazao haya. Maana ukiangalia kwa sasa hivi mazao mengi ya mbogamboga na matunda yanapitia Bandari ya Mombasa, hata yale maparachichi ya Njombe mengi yanapitia Mombasa badala ya kupitia Bandari ya Dar es Salaam au ya Tanga. Sasa hapa tuna kitu cha kujifunza. Serikali ikae na wafanyabiashara ili iweze kuona tuna upungufu gani ambao bandari zetu ya Tanga na Dar es Salaam haiwezi kusafirisha mbogamboga na matunda kwa urahisi kiasi ambacho kinawafanya wakapitie kwenye bandari nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kuongelea suala la umwagiliaji, kwa sababu umwagiliaji utaongeza sana tija kwa wakulima wetu. Sisi wa Handeni Vijijini tunapitiwa na Mto mkubwa wa Pangani ambapo tungeweza kutumia vizuri Bonde ya Masatu na Bonde la Kwamgwe ambapo maji yameshafanya kazi ya kuzalisha umeme sasa yanaenda kutupwa tu baharini. Kwa kutumia mabonde haya tungeweza kusisimua sana kilimo kwa wananchi na kuleta tija na hatimaye kuongeza kipato cha wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna mito ya msimu ambayo wakati wa mvua inaleta tafrani kubwa kwenye madaraja yetu. Sasa hii mito ya msimu tungeweza kuyakinga maji na tukayatumia kwa ajili ya umwagiliaji wa mbogamboga na matunda, tungeongeza tija kubwa kwa wananchi wetu. Mito hiyo ni kama vile Mto Msangazi na Mto Mnyuzi ambayo inakatiza katika eneo kubwa la Jimbo la Handeni Vijijini ambapo tukiitumia vizuri, basi tutatengeneza mazingira bora ya wakulima na hivyo kuongeza tija na kipato kwa ujumla na hatimaye kuongeza pato la halmashauri na nchi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nije kwenye suala la zile mashine za kukusanyia kodi. Mashine zile zinahitaji mtandao wa simu (network) na eneo kubwa la Jimbo la Handeni Vijijini hatuna network ya kutosha. Hivyo tunatumia mashine ambazo zinaweza kukusanya kodi offline lakini inabidi lazima mkusanyaji huyo wa kodi atoke aende kutafuta mtandao ili aweze ku-reconcile data zake. Sasa hicho kipindi cha kwenda kutafuta mtandao na kupanda kwenye mti kupata mtandao ina maana kuna malori ya mizigo yanapita pale, kwa hiyo kuna mapato tunakosa. Hivyo, Wizara husika naomba itusaidie, mtandao upatikane katika maeneo yote ili tuweze kukusanya mapato ya halmashauri kadri inavyotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sina budi kushukuru upatikanaji wa mbinu mbadala ya kupata hela ya kuchangia TARURA kwa sababu tukiimarisha TARURA tutaweza kutoa mazao yetu kwenda sokoni na bei itakuwa nzuri kwani sasa hivi kuna mazao yanaharibika na kuozea mashambani kwa kukosa barabara nzuri. Hivyo, nasihi ule ukusanyaji wa vyanzo ambavyo tumevipanga hapa ufanyike vizuri na Fungu lilindwe vizuri ili kweli lipelekwe kutengeneza barabara zetu za TARURA zipitike mwaka mzima ili tuweze kutoa mazao na tupate maendeleo tarajiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kupata nafasi hii na naunga mkono hoja. (Makofi)