Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Naibu Spika, Ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi nichangie hoja iliyopo mezani. Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai na wakati huo huo nawashukuru sana wananchi wa Urambo wakiwamo Ndugu zangu kwa ushirikiano wanaonipa mimi katika kutafuta maendeleo ya eneo letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali yetu ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mama yetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, akiwemo Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na Mawaziri wote kwa jitihada zao kubwa ambazo zimetuletea hii bajeti ambayo tunaijadili siku ya leo. Hongera sana Serikali kwa bajeti nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Urambo tumenufaika pia na bajeti hii tumehakikishiwa maji yatakuja, barabara zitatengenezwa, umeme utafika kwenye vijiji vyote. Ombi letu kwa siku ya leo ni kwamba lini mafundi watafika Urambo kuhakikisha kwamba ule mradi wa maji unaotoka Lake Victoria unaanza kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kilimo ni muhimu sana katika Wilaya yetu kwa sababu tunategemea sana zao la tumbaku ili lituwezeshe kumudu maisha kwa upande wa biashara. Nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwa sababu imetambua kwamba kuna umuhimu wa kufanya vikao na wanunuzi wa tumbaku. Kwa sababu kilio chetu kikubwa ni kuongeza makisio, wakulima wanapenda walime kadri wanavyoweza kwa hiyo tunapopata makisio makubwa yanatupa nguvu na sisi ya kulima zaidi. Kwa hiyo naipongeza Serikali kwa kitendo chake cha kukutana na wanunuzi mwaka jana mwezi Februari, 2020. Serikali kwa kupitia wizara ya fedha na wakati huo alikuwa Mheshimiwa Makamu wa Rais, Dkt. Philip Mpango ambaye alikutana na wanunuzi wa tumbaku.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba utaratibu wa kukutana na wanunuzi uendelee kwa sababu kikao cha mwaka jana mwezi Februari, 2020 kilizaa matunda tukaongezewa makisio kutoka tani elfu 36 hadi kufikia tani 67 elfu. Kwa hiyo vikao tunaomba viendelee vya kukutana na wanunuzi, kwanza vinawapa nguvu wale wanunuzi waliopo lakini pia kinatoa fursa ya kujadili tozo mbalimbali, changamoto wanazokutana nazo ili weendelee kununua tumbaku. Kwa hiyo, tunaomba Serikali iendelee na utaratibu wa kukutana na wanunuzi, tunategemea kwamba wanunuzi watakapokuwa wengi kwanza watatoa makisio zaidi lakini pia kutakuwa na changamoto ya kuongeza bei, kutakuwa ushindani wa bei, kwa hiyo tutanufanika zaidi. Hivyo, utatatibu wa Serikali kukutana na wanunuzi tunaomba uendelee.

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii tumeiona ina bilioni 294 zikiwepo bilioni 30 za umwagiliaji. Lakini Serikali inajua, kwamba kuna Azimio la Maputo ambalo walikuwa wamekubaliana kwamba kutenga asilimia 10 ya bajeti nzima iende kwenye kilimo. Tunajua kwa mwaka huu haiwezekani kwa sababu tayari wameshatenga bilioni 294. Ombi sasa kwa Serikali kweli kwamba zile bilioni 294 basi zipatikane ziende kwa kilimo, fedha zote zilizotengwa ziende kwenye kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii pia kuipongeza Serikali kwa kuondoa VAT kwa upande wa cold rooms vyumba vya kuhifadhi baridi ili watu wanaosafirisha mazao nje, maua na mazao mengine yanayotokana na horticulture wapeleke. Tunaipongeza Serikali kwa suala hilo lakini tunaomba basi Serikali ituambie kwamba ina vituo vingapi vya kuhifadhi baridi yaani cold rooms. Na je, ina mpango wa kuongeza, kama ina mpango wa kuongeza inaongeza vyumba vingapi ili wenzetu wanaosafirisha bidhaa nje kwa kutegemea hivyo vyumba basi na wenyewe wanufaike.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niiombe Serikali imeweka asilimia mbili ya Kodi ya Zuio. Tunaomba hii kodi asilimia mbili iondolewe kwa upande wa mazao ya wakulima ili waweze kupelekea mazao yao vizuri zaidi. Naiomba Serikali kwa kuwa ina mpango wa kuongeza zao la alizeti, sisi kama Mkoa wa Tabora nasi pia tunalima alizeti, tunaomba tuongezwe kwenye mpango wa kuongeza zao la alizeti ili na sisi tuliwe kwa sababu tunajua kwa sasa hivi zao la alizeti ni muhimu katika upande wa kuongeza mafuta kama tunavyoona sasa hivi mafuta yamepanda bei sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Serikali kwa ujumla mimi mwalimu, ningependa sana nizungumzie suala la elimu naona sintatenda haki bila kuzungumza suala la elimu. Nampongeza Mheshimiwa Prof. Ndalichako nimemuona kwenye vikao vingi sasa hivi anatafuta maoni na jinsi gani ya kuboresha elimu nchini. Ni jambo zuri sana, nakupongeza kwa sababu sisi wote tumeomba Serikali ifanyie kazi suala la elimu ili liende na wakati lijibu hoja na mahitaji ya kipindi hiki. Lakini mimi nilikuwa namuomba Mheshimiwa Prof. Ndalichako na Wizara ya Elimu kwa ujumla iangalie uboreshaji wa elimu lakini iwaanglie na Walimu. Kwa sababu huwezi kuboresha suala la elimu bila ya kuangalia Watendaji, sasa hivi tumeona walimu wana changamoto nyingi sana, wengi hawapandi madaraja kwa wakati na wengine wanapanda madaraja lakini mishahara yao hairekebishwi kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi ningeomba Serikali iwachukue wale wote ambao wana mhudumia Mwalimu kwa sababu Mwalimu hahudumiwi na mtu mmoja anahudumiwa na vyombo vingi sana. Kwa hiyo mimi ningeomba kuwe na kikao cha kuangalia wote wanaomuhudmia mwalimu wanafanyaje yaani kuwe na co-ordination ili walimu waweze kupata haki zao kwa wakati na waweze kufanya kazi kwa bidi zaidi hata baada ya kuletewa maboresho hayo. Kwa mfano nilikuwa naangalia suala la TSC ilipoundwa ilikuwa na malengo gani? Mimi nilikuwa nategemea kwamba TSC itasaidia kuleta co-ordination yaani itaunganisha vyombo kwa pamoja ili mambo ya upandaji wa madaraja, kama ni kuchukuliwa hatua za nidhamu na vitu vya namna hiyo, lakini je, najiuliza TSC ilipoundwa na ikapewa majukumu yale kweli ndiyo tunachotegemeWa. Matokeo ya utendaji kazi wa TSC ndiyo yale tuliyoyategemea baada ya kuomba iundwe? Kwa hiyo naomba TSC ifanyiwe tathmini kama kweli inafanya kazi iliyokusudiwa ya kurahisisha huduma kwa Walimu ambao ni walengwa. Wakati huo huo, pamoja tukija na maboresho ya elimu lakini pia tuangalie suala la ukaguzi. Je, ukaguzi inafanya kazi inavyopaswa kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho naomba nimalizie kwa kuzungumzia suala la posho kwa Watendaji wa Kata. Naipongeza Serikali kwa kwa Watendaji wa Kata wamefanya vizuri sana lakini niiombe pia na Watendaji wa Vijiji na Mitaa waangaliwe. Kwa sababu wao nao pia wanasaidia kuhamasisha suala la uchaguzi, sensa inakuja watatumika, masuala ya usalama, kwa hiyo naomba pia Watendaji wa VIjiji nao waangaliwe wapate posho kama walivyopata wenzao wa upande wa Kata. Itasaidia kuwapa motisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeangalia data, nikaangalia kuna vijiji 12,319, mitaa 4,263 wakichanga na wale Watendaji wa Kata 3,956 naamini Serikali inaweza, penye nia pana njia. Naipongeza sana kwa bajeti hii lakini naomba narudia tena kuomba watusaidie sana suala la kilimo kwa sababu kilimo ndiYo Uti wa Mgongo. Ahsante sana. (Makofi)