Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti nashukuru kwa kunipa fursa hii. Kwa kuanza nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai na kunifanya nisimame mbele ya Bunge lako Tukufu. Pia nitume nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya na anayoendelea kuifanya.

Vile vile nimpongeze Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na Serikali nzima kwa ujumla, wanafanya kazi kubwa sana. Mwisho, nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Naibu na Watendaji wote chini ya Katibu Mkuu ndugu yangu Tutuba. Nafahamu umahiri wake, naamini tutaenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti tunayoijadili ni bajeti nzuri sana na nitumie nafasi hii kuwaomba sana Watanzania na hasa wa eneo la Ukerewe waipokee bajeti hii kwa sababu ni bajeti nzuri, inagusa mambo mengi ya msingi yanayogusa maisha ya waanchi wa ujumla wake. Pia bajeti hii inaonesha uelekeo mzuri na zaidi na inatia matumaini, kwa hiyo niwaombe Watanzania waipokee kwa moyo ya dhati kabisa kwa mikono miwili kwa sababu ni bajeti inayotuonesha tunapoelekea ni pazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kushauri kwenye maeneo machache sana. La kwanza, bajeti hii kama nilivyosema ni bajeti nzuri, imegusa mambo mengi sana ya msingi na imezingatia ushauri ambao Wabunge tumeutoa katika mijadala mbalimbali. Bajeti hii ili tuweze kuitekeleza vizuri na yale manufaa tunayotarajia tuweze kuyaona, ni lazima tu-maintain walipakodi tulionao, lakini tutengeneze walipakodi wengine ili tuweze kupata nguvu ya kutekeleza haya tuliyoyapanga kwenye bajeti, kwenye mpango, mwisho wa siku yale tunayotarajia yaweze kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia kwenye Mpango wa Pili wa Maendeleo katika mambo yaliyosaidia sana kuchochea kukua kwa uchumi mpaka tukafikia uchumi wa kati ni pamoja na kusambaa kwa umeme, jitihadi zilizofanywa na Serikali kusambaza nishati ya umeme, kuboresha miundombinu ya utoaji wa huduma za afya, maji na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia eneo hilo hilo, ningependa kuongelea kwenye eneo la nishati ya umeme. Umeme ni injini kubwa sana ya kuchochea maendeleo ya wananchi kwa ujumla wake na nimefarijika kwenye bajeti hii, bajeti kuu lakini hata bajeti ya Wizara ya Nishati, Serikali imeonesha dhamira yake ya kuendelea na program ya usambazaji wa umeme kwenye vijiji ambavyo havikufikiwa na umeme lakini mpaka kwenye vitongoji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni jambo jema sana na likifanyika hili itasaidia sana kuchochea uchumi wa watu wetu na litasaidia kuongeza wigo wa walipa kodi kwasababu tuna vijana wengi ambao wana mawazo, wangependa kujiajiri, lakini wanaweza kujiajiri kama watakuwa na nishati ya umeme ili kuweza kuanzisha shughuli zao ndogo ndogo. Kama hili litafanyika litakuwa ni jambo jema sana. Kwa hiyo niiombe Serikali iweke mkazo na iweze ku-finance fully kwenye eneo hili la usambazaji wa umeme. Tusisahau kwenye bajeti ya Wizara ya Nishati ilionekana katika mipango waliyonayo ni pamoja na kusambaza umeme kwenye maeneo ya visiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Jimbo la Ukerewe kwa mfano, ambalo linaundwa na visiwa 38, katika wakazi zaidi ya 400,000 tulionao karibu asilimia 40 ya wakazi wanaishi katika visiwa vidogo vidogo ambavyo bado havina umeme. Kwa hiyo kutofikiwa na umeme kunadumaza maendeleo ya watu hawa na kwa maana hiyo kunadumaza vile vile jitihada za kuongeza walipakodi wengine kupitia shughuli mbalimbali ambazo wangezifanya kupitia ujasirimali. Kwa hiyo niiombe Serikali tuhakikishe kwamba kupitia bajeti hii tunaweza ku- finace kwa kiwango kikubwa ili kuhakikisha kwamba program tuliyonayo ya upelekaji umeme vijijini na hasa visiwani tunaikamilisha kwa asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Mpango wa Pili wa Maendeleo vile vile unaonesha kwamba Sekta ya Kilimo hasa kwenye eneo la uvuvi iliongezeka na ndio maana utaangalia hata kwenye uchakataji wa minofu ya samaki kwa kipindi kilichopita tani zaidi ya 26,000 zilisafirishwa ukilinganisha na tani 23,000 zilizosafirishwa miaka minne, mitano kabla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ni jema sana na shabaha ya Mpango wa Tatu ni kuchochea maendeleo ya watu. Katika kuchochea maendeleo ya watu ni pamoja na kukuza uchumi wa watu wetu hasa kwenye maeneo ambako shughuli mbalimbali za uzalishaji zinafanyika. Sasa niombe, Kanda za Ziwa ambao wanazunguza ziwa Victori kuna uzalishaji mkubwa wa Samaki. Kama nilivyoonesha hapa kumekuwa na ongezeko kubwa sana na ufanisi kwenye sekta ya uvuvi. Katika samaki wanaozalishwa katika ukanda ule karibu asilimia 30 ya samaki wale wanapatikana kwenye Visiwa vya Ukerewe, lakini bahati mbaya sana Ukerewe hakuna Kiwanda cha Kuchakata Samaki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Serikali ilione hili, ili kuweza kuchochea maendeleo ya watu wa eneo lile na kwa sababu ndio shabaha ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo, basi Wizara ya Fedha, Mheshimiwa Mwigulu aangalie uwezekano wa kuwa na Kiwanda cha Kuchakata Samaki kwenye eneo la Ukerewe pale. Kwa sababu samaki wanazalishwa pale na wakichakatwa pale, shughuli za ujasiriamali zitakuwepo na kwa maana hiyo kuongeza wigo wa walipakodi na wananchi wengi watashiriki kwenye kuchangia pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe Wizara iweze kuliangalia jambo hili. Eneo lingine ambalo napenda kushauri ni kwenye eneo la Madiwani. Niipongeze sana Serikali kwa kufanya uamuzi wa kuchukua jukumu la kuwalipa Madiwani kutoka Mfuko Mkuu wa Serikali. Sasa pamoja na kuchukua jukumu hili kumekuwa na kilio kikubwa sana cha Madiwani wetu kuomba posho hizi wanazozipata ziweze kuongezwa. wamesema Wabunge wenzangu ni jambo jema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile pamoja na kuchukua jukumu la kulipa posho za Madiwani kuna kundi kubwa sana la viongozi wetu wa vijiji na vitongoji na mitaa; Wenyeviti wa Vijiji, Wenyeviti wa Vitongoji na Wenyeviti wa Mitaa. Niiombe Seirkali itoe mwongozo kupitia TAMISEMI, basi lile eneo ambalo Halmashauri zilitumia kulipa Madiwani zihakikishe mafao ya Wenyeviti wa Vijiji, Vitongoji na Mitaa yaweze kulipwa effectively ili kuweza kuhamasisha shughuli za maendeleo kwenye maeneo yetu. Nakushukuru sana. (Makofi)