Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Innocent Edward Kalogeris

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ambayo ipo mbele yetu, lakini kubwa zaidi nikupongeze wewe binafsi kwa kazi kubwa ambayo unaifanya hapo katika kiti katika kutuongoza. Hakika wewe ni mtoto wa nyoka na kama sio wa nyoka basi ni mjukuu wa nyoka, maana yake damu ya ukoo wa Adam Sapi Mkwawa inaonekana inafanya kazi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri wetu wa Fedha ndugu yangu Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, Naibu wake na timu nzima ya wataalam kwa kutuletea bajeti ambayo kiuhakika imebeba dhana ya maelekezo ya mama yetu Samia Suluhu Hassan, lakini kubwa zaidi Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi katika kumsaidia Mtanzania kusonga mbele kutoka hapa tulipo na kwenda mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni uthibitisho tosha umeona kila Mbunge aliyesimama anapongeza, lakini sio Mbunge kwa sababu sisi Wabunge tulichangia katika bajeti katika Wizara mbalimbali, tukieleza zile kero za wananchi wetu na wananchi wetu huko nje vile vile wamepata faraja kubwa na wanaendelea kuipongeza Serikali ya Chama Cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa hongera sana kwa mdogo wangu Mheshimiwa Mwigulu na timu yake kwa kufuata maelekezo ya mama, lakini kwa kufuata maelekezo ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama Chetu Cha Mapinduzi. Ni imani yangu kabisa tukienda hivi ndani ya miaka mitano hii tutafanya mambo makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitumie nafasi hii kumpongeza Mama yetu Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jemedari mkuu katika nchi yetu, kwa kazi kubwa ambayo ameifanya ndani ya kipindi cha siku 100 anakoelekea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakika mama huyu ni Mama shujaa, mama shupavu ambaye kwa uhakika niwaambie Watanzania na naendelea kusema mama huyu anatosha, anatosha na atatuvusha salama Watanzania kule tunapotarajia kwenda. Hata hivyo, nitumie nafasi hii…

T A A R I F A

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa.

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa tu ndugu mzungumzaji kwamba mama huyu sio tu anatosha bali anatosha na chenji inabaki. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kalogeris, endelea na kuchangia.

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru nimeipokea taarifa. Ni kweli chenji bado inabaki na itatosha kufanyia mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii vile vile kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu, ndugu yetu kwa kazi kubwa ambayo anaifanya ndani na nje ya Bunge katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi, lakini kuwa kama kiungo kati ya Mama Baraza la Mawaziri lakini na sisi Wabunge katika kuona kipi kifanyike. Ni imani yangu kwamba hata haya yaliyokuja kuna majumuisho makubwa ambayo yamefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii vile vile kutoa pongeza za dhati kwa Serikali yangu. Hakika kauli yake Mama, anatusalimu kwa jina la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, sisi tunatakiwa kujibu kazi iendelee, kazi inaendelea tena kwa kasi kubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona tumepata milioni 500 kila Jimbo kwa ajili ya TARURA. Wabunge tumepiga kelele kwamba barabara mbaya, barabara mbovu, lakini mama ametusikia ametupa. Pia nimpongeze ndugu yangu Mheshimiwa Mwigulu na naamini hayo ni maelekezo ya Mama kwa kubuni vyanzo mbalimbali ambavyo tunaamini kwa mwaka huu wa fedha tutakwenda kutengeneza bilioni 300 ambayo inaonekana inakwenda TARURA. Ombi langu kwa Serikali, Halmashauri, Majiji na Manispaa tumetengwa katika fedha za Mfuko wa Barabara, wamependelewa wenzetu wa Majiji na Manispaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu fedha hizi katika mgao wake uende kwa majimbo bila kujali la Manispaa au la Jiji na kadhalika ili na sisi Halmashauri twende tukajenge barabara ambayo ukitilia maanani mtandao wa barabara kwenye halmashauri ni mkubwa kuliko kwenye majiji au manispaa. Kwa hivyo niwaombe Wabunge wenzangu katika hili tuwe pamoja na Mheshimiwa Waziri wa Fedha TAMISEMI mgao wa fedha hizi bilioni 300, zigawiwe katika majimbo, nikiamini kila Jimbo litapata karibu millioni 800 na tutaenda kufanya kazi kubwa ya barabara. Ndani ya miaka mitano nataka nithibitishe katika Bunge hili kwamba suala la barabara litakuwa ni historia katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii vile vile kutoa pongezi za dhati kwa Serikali yangu ya Chama Cha Mapinduzi tuliahidi na bahati nzuri nilikuwa ni Mwenyekiti wa CCM wa Mkoa mpaka naingia hapa Bungeni. Nilipita Mkoa mzima wa Morogoro tukiahidi kila kitu tutafanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la REA, walipotuambia umeme tulisema mpaka kufikia 2023 tutakuwa tumekamilisha kabisa. Nataka nitoe taarifa na shukrani za dhati kwa wananchi wa Jimbo la Morogoro Kusini na Mkoa wa Morogoro. Jana Mkoa wa Morogoro tumezindua rasmi REA III mzunguko wa II, vijiji vyote vinapata umeme. Hongera sana kwa Serikali yangu ya Chama Cha Mpinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru leo asubuhi katika kuuliza swali imeonekana vijiji vile ambavyo vimepungua, Wizara imesema kwamba navyo vitaingia hata kama havipo. Kwangu vimebaki vijiji vitano tu, ahsanteni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile niishukuru Serikali yangu ya Chama Cha Mapinduzi kwa kazi kubwa ambayo imeifanya, aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati Dkt. John Joseph Pombe Magufuli alipokuwa katika ziara yake katika siku zake za mwisho katika dunia hii, alisimama Morogoro na akasema atatoa kilometa 40 kujengwa kwa lami kutoka Mjini Morogoro mpaka tutakapoishia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru katika bajeti hii tumetengewa kilometa 15 na tayari imeshatangazwa maana yake kazi inaenda kufanywa, nina kila sababu ya kuipongeza Serikali, lakini niiombe Serikali barabara hii inakwenda mpaka kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere inakwenda mpaka kwenye Hifadhi ya Mwalimu Nyerere tuendelee kutenga fedha ili tufike huko, utalii ukaendelee kuwepo kwenye Hifadhi, lakini vile vile katika hilo bwawa la Mwalimu Nyerere. Naamini bwawa hili likikamilika utakuwa ni utalii mkubwa ambao utaingiza fedha nyingi kwenye Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukrani hizo, naomba nichangie kwenye maeneo mawili. Eneo la kwanza ni kwenye kodi; ni imani yangu hakuna Mtanzania ambaye hataki kulipa kodi, ila lipo jambo ambalo Serikali inatakiwa kufanya kupitia TRA kwamba kodi inayokadiriwa iwe na uhalisia na inayolipika. Katika maeneo mengi wafanyabiashara wanalia na ukweli usiofichika wanalia, kuna kama dhuluma ambayo inatendeka. Sasa katika hili, Mama yetu amesema hataki dhuluma, anataka watu walipe kodi kwa hiyari, naomba Mheshimiwa Waziri akasimamie hili TRA, kodi ikawe ya uwazi na iwe inayolipika kulingana na mwananchi alivyopata kipato chake, failure to that, ni kwamba watu watakwepa au tunatengeneza mianya ya rushwa kati ya watu wa TRA na walipakodi, mwisho wake kodi itakuwa haiwezi kulipika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine la mwisho ambalo ningependa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja ili kazi iendelee, haya yote niliyosema yakamilike. Ahsante sana. (Makofi)