Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema aliyetujalia uzima, lakini kipekee nitumie nafasi hii kumpongeza sana Waziri wa Fedha kwa hotuba yake nzuri lakini kwa ujumla nimpongeze Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hotuba hii inatoa mwelekeo mzuri sana wa Serikali ya Chama cha Mapinduzi na inaonyesha namna gani kama alivyosema Kaka yangu Mheshimiwa Nape Serikali yetu inakwenda kuangaika na shida na matatizo ya watu wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti hii kuweka kipaumbele kwenye miundombinu ya barabara, kwenye masuala ya maji, kweye kukamilisha umeme vijijini lakini pia kwenye masuala ya afya na elimu hayo ndiyo mambo ambayo wanahangaika nayo Watanzania. Kama fedha zitakazokusanywa zikitumika vizuri kwenye mambo haya hata huu wasiwasi uliopo kwenye baadhi ya kodi na tozo tulizoongeza utaondoka na niwaombe tu watanzania hatuna namna nyingine ya kuijenga nchi yetu zaidi ya kutafuta na kutengeneza kodi na kukusanya kodi, lazima tulipe kodi tuweze kutengeneza na kuijenga nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri kipekee nipongeze kuongeza ushuru wa forodha kutoka asilimia 25 mpaka 35 kwenye magunia ya kitani yale ya duty lakini pia kuongeza ushuru wa forodha asilimia 10 kwa nyuzi za plastiki itatusaidia sana wakulima wa mkonge tunakwenda kuongeza soko na kulinda Mkonge wa Tanzania wa nchi hii. Ni jambo ambalo tunalipigia kelele muda mrefu tunashukuru Serikali, imelisikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende tu moja kwa moja kwenye jambo moja ambalo jana Kaka yangu Mheshimiwa Kitandula alisema wameniachia kulizungumza mimi mdogo wao watu wa Tanga na watu wa Morogoro tunataka tuishauri Serikali haswa kwenye kuongeza mapato na hapa nazungumzia sana mapato kwenye mamlaka za Serikali za Mitaa. Niombe sana Waziri wa Fedha niombe sana watu wa TAMISEMI, watu wa Wizara ya Kilimo na watu wa Kamati ya Bajeti kama wako hapa watusikilize vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yako kwenye ukurasa wa 53 moja ya maeneo yanayokwenda kufanya marekebisho tunakwenda kuirekebisha sheria ya fedha ya Serikali za Mitaa sura ya 290 na kwenye hotuba yako umesema, tunakwenda kufanya marekebisho, moja ili kubainisha mazingira ambayo kampuni iliyolipa tozo ya huduma haitawajibika kulipa tozo ya uzalishaji na ukasema marekebisho hayo yanalenga kutatua mgongano uliojitokeza kwenye kutafsiri kifungu husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimeingia humu 2018 miaka mitano iliyopita tumekuwa na changamoto sana kwenye jambo hili, lakini Waziri wa Fedha nikuhakikishie hatukuwa na mgongano wowote wa tafsiri kwenye sheria hii, Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa Kifungu cha Kumi na Sita inasema corporate entity inayolipa service levy haitalipa produce cess iukienda kwenye sheria yenyewe ya fedha inasema kwa mazao ya biashara mnunuzi anapaswa kulipa asilimia tatu ya farm gate price kama ushuru wa mazao kwa maana ya produce cess hakukuwa na mgongano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa tafsiri ya kisheria mgongano uliokuwepo ulikuwa ni mgongano wa kimaslahi nani afanye nini nani alipe nini tukasumbuana miaka mitano hapa na watu wa Wizara ya Kilimo ni mashahidi tumefanya vikao vingi leo limekuja kujitokeza, niliposoma kwenye hotuba yako na kukusikiliza nimerudi kwenda kuangalia Finance Bill ambayo inakuja, yanakuja marekebisho ya kurekebisha kifungu hichi kwenye Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekwenda kuongeza specifically tunasema corporate entity ambayo inazalisha mazao ya kilimo haitalipa ushuru wa mazao kwa mazao yanayozalisha labda kwa mazao ambayo yanatoka kwa mtu mwingine. Tumesema tunataka kuongeza mapato na mwaka wa fedha tulionao Halmashauri zimekusanya kwa asilimia 88 na tumeongeza makadirio na moja ya vyanzo muhimu vinavyotegemewa ni huu ushuru wa mazao sasa haya mabadiliko yaliyofanyika tafsiri yake ni nini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafsiri yake ni kwamba yale makampuni wazalishaji wakubwa wa mazao tukichukuwa mfano wa zao la mkonge hawatalipa ushuru wa mazao kwa maana produce cess labda kama wamechukua mazao hayo kutoka kwa mkulima mwingine ambaye hapo sasa tunamzungumzia mkulima mdogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya jambo hili ni kubwa inakwenda kutupunguzia fedha na mapato kwenye Halmashauri zetu na sisi ambao tunalima tunapata shida kidogo ukienda leo Handeni DC...

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Chumi.

T A A R I F A

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa mzungumzaji, kwamba jambo hilo halitaenda kuathiri tu Korogwe hata Halmashauri ya Mji wa Mafinga, hata Halmashauri ya Wilaya Mufindi hata Halmashauri ya Njombe ambayo tunategemea misitu kwa sababu kwa mfano sisi asilimia 50 ya mapato yetu yanatokana na hiyo ambayo inataka ije ifutwe. (Makofi)

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa naomba tu muda wangu ulindwe vizuri. Nina takwimu hapa za Halmashauri nyingi lakini nichukue Halmashauri moja tu ya Korogwe, huko nyuma baada ya kutokea hii mivutano tukaenda mpaka kwenye Kamati ya Bajeti na Mheshimiwa Simbachawene akiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti, wakasema mgongano wa kisheria hapa nendeni mkatekeleze sheria, sisi wa Mkoa wa Tanga tukaenda kutengeneza By Laws kwamba huyu mkulima mkubwa kabla hajatoa mzigo wake usiondoke mpaka awe amepata ushuru wetu wa mazao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ni kwamba Sheria ya Fedha inataka mnunuzi ndiyo alipe, wakulima wakubwa wa mkonge wakimaliza kulima wanachukua wanapeleka nje, Halmashauri hatumjui mnunuzi ni nani hatujui ananunua shilingi ngapi tukawa na changamoto, tukaweka sheria kwa mabadiliko haya mnayoyaleta hata ile By Laws haitaweza kutekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, chukua mfano wa Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe asilimia 70 ya eneo letu ni mashamba makubwa ya mkonge kwa hiyo mkonge ndio madini yetu, mkonge ndiyo kila kitu na ukitaka kuona hilo mwaka wa fedha tulionao kwenye bilioni moja na milioni tisa na kidogo mapato yanayotokana na ushuru wa mazao kwenye mkonge peke yake ni milioni 425 sawa na asilimia 39 ya mapato yetu. Leo ukiondo produce cess tunapata wapi mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo tu kupunguza mapato lakini pia mnatuletea mkanganyiko, huyu mkulima mkubwa ambaye anaambiwa asilipe produce cess kwa tabia ilivyo pia wananunua kwa wakulima wadogo, tunatofautishaje kati ya mkulima mkubwa na mkulima mdogo mazao yapi yametoka wapi hatuwezi kutofautisha, lakini shida ya pili kama mkulima mkubwa halipi produce cess maana yake mazao ambayo yana uhakika wa kulipiwa ushuru wa mazao ni mazao anayolima mkulima mdogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafsiri yake nini ukiwa na mnunuzi independent aliyekuja kutoka nje kwenda kununua mazao kwa wakulima wadogo ni lazima atafuata hiyo tozo tunayotaka tuichukue Halmashauri, kwa hiyo atapunguza bei kwa mkulima wetu ili aweze kupata nguvu ya kulipa ushuru na kununua yale mazao. Wakati huyu mwingine anachukuwa mazao yake anapeleka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ilitokea mwaka 2019 mwishoni alikuja mnunuzi kampuni ya Kichina kununua mkonge akakuta kuna ushuru wa mazao kwa wakulima wadogo ukinunua, akatakiwa kulipa, akaona kuliko kulipa ule ushuru ni bora aache, ilitumika busara ya Mkuu wa Mkoa kuwaomba halmashauri wasamehe ili ule ushuru wa mazao hili mnunuzi huyo anunue wakulima wasiumie. Maana yake ni kwamba mazao ya wakulima wadogo yanakwenda kushindanishwa na wakulima wakubwa, akikosekana mnunuzi independent kwa sababu ya hii kodi, wakati hawa makampuni makubwa hawalipi, wakulima wetu watakuwa hawana option zaidi ya kuwauzia hawa wakulima wakubwa ambao wana makampuni na mashamba kule kwenye maeneo yetu, wakienda kuwauzia bei ya mkonge itaporomoka, bei ya mkonge wataipanga wanavyojisikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha na ….

T A A R I F A

MWENYEKITI: Nimemwona Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge, Mtendaji wetu wa CCM Mstaafu anayejenga hoja kwa umakini mkubwa sana, amewakilisha Halmashauri nyingi tu, nilitaka nikiombe Kiti chako, Mheshimiwa Mbunge pamoja na mwingine aliyetoa hoja, tukiahirisha Bunge hapa tukakae na timu yangu ya wataalam wanaoandaa Finance Bill tulipitie hili jambo ili tulirekebishe ili tunavyo print document ya mwisho iwe imekaa sawa kwa maslahi mapana ya nchi yetu. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mnzava unaipokea taarifa?

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hiyo kwa mikono miwili na nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa uungwana huu mkubwa uliounyesha. Kwenye hili Mheshimiwa Waziri wa Fedha nataka niendelee kusema mengine lakini kwa uungwana uliouonyesha kwenye hili naishia hapa tutaonana tuliweke vizuri Mheshimiwa Waziri wa Fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nimalizie na moja tu maana Mheshimiwa Waziri wa Fedha nimefurahi sina haja ya kuendelea sana nimalizie na moja dogo. Tusaidieni tumeanzisha tozo kwenye zile skimu za umwagiliaji kwa maeneo ambayo yanakuwa yanasimamiwa na Vyama vya Ushirika na skimu za umwagiliaji kwa ujumla, hii iwe chachu ya kutufanya tuongeze fedha zaidi kuwa na miradi mingi, watu wa Korogwe kwa mfano, wanaangaika kwa zaidi ya 20 na Bwawa la Mkomazi bilioni sita inahitajika. Ukienda kilimo wanasema tumepeleka Hazina, ukienda Hazina na tungeweza kupata mapato mengi kwenye maeneo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)