Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Francis Leonard Mtega

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbarali

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ili niweze kuchangia katika bajeti hii. Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu anayetujalia uhai na anayezidi kulinda Taifa letu na ustawi wa wananchi wake. Pili, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anazofanya, nimshukuru sana Makamu wa Rais, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu na Baraza lote la Mawaziri kwa kazi nzuri wanazofanya. Hii imetuletea bajeti nzuri, bajeti ambayo imegusa kila eneo, kila kundi kwa kweli ni bajeti ambayo inaenda kuinua hali za Watanzania wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba mchango wangu ujikite katika kilimo; kwa vile asilimia 65 ya Watanzania wanajihusisha na kilimo, lakini pia vijana wetu ambao hawana ajira wanaweza wakajiunga na kilimo. Vile vile Bunge lako Tukufu hili Bunge la Kumi na Mbili limebainisha kwamba linaenda kujikita zaidi katika kufanya mageuzi makubwa katika sekta hii ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona katika bajeti ukurasa wa tano, ukurasa wa 16 na wa 17 namna ambavyo Serikali inaenda kuboresha kilimo, namna Serikali inavyoenda kuleta tija na kutafuta masoko ya ndani na nje ya nchi. Hata hivyo, nilitarajia kuona kwamba Serikali inaweka fedha nyingi kama mtaji kuinua hii sekta; kwanza kwa kujenga na kuboresha miundombinu ya umwagiliaji, lakini pili, kwa kutafuta masoko na kuboresha ya ndani na nje na kikanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kabla ya kuanza mtaji huu naona kuna tozo mbalimbali zimewekwa pale. Kwa mfano katika ukurasa wa 33 kuna tozo ya zuio, sasa pale imefafanuliwa vizuri kwamba tozo hii inaenda kutozwa kwa NFRA kama Wakala wa Ununuzi, lakini bahati mbaya kinachotokea kule ni tofauti kabisa, ni wakulima ndio wanaotozwa tozo hii. Wakulima wale hawajafafanuliwa vizuri, tozo hii inatozwa wakati gani kwa sababu kuna ushuru wa halmashauri na wakulima wanatozwa njiani wanavyotoka shambani wakati wanarudisha mazao nyumbani, wanatozwa barabarani, lakini pia wakulima wanatozwa wanapopeleka gulioni wanatozwa mara ya pili na tatu wengine wanatozwa pale wanapouza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Mheshimiwa Waziri aje na ufafanuzi, kwamba muda sahihi wa kumtoza mkulima hasa mdogo ni wakati gani? Anaposafirisha au anapouza? Ni wakati gani atozwe na kwa kiasi gani? Tumeona nyuma huko, ilikuwa kawaida ni kwamba anayebeba chini ya tani moja hatozwi chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa ukurasa wa 33 imebainishwa kabisa, hii haitahusu wakulima wadogo wadogo magulioni, itahusu tu wakala wa ununuzi, lakini kinachotokea kule ni tofauti kabisa; wale wazabuni wanaotakiwa watoze njiani, hata wakiona gunia chini ya tani moja, wanatoza. Wanatoa visingizio mbalimbali; watasema umeweka mfuko haufai siyo wenyewe, watasema sijui sasa hivi tunatoza tu kwa vile umechelewa kurudi toka shambani, ili mradi wao wapate kodi kubwa. Wanapiga hesabu ya kutosha kupeleka Halmashauri na nyingine ibaki kwa ajili yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tungependa ufafanuzi, tujue hali halisi, inatakiwa itozwe kwa nani? Kama ni mkulima, basi ni wakati gani? Je, ni pale anapofanya biashara au wakati gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, changamoto nyingine kwa wakulima hawa ni mbolea. Mbolea ina ruzuku lakini kwa kweli ruzuku ile inafika mahali haiwezekani, bado ni bei kubwa sana. Nitoe mfano, mwaka jana 2020, Jimbo la Mbalali mbolea aina ya CAN imeadimika kabisa. Huwa bei ya kawaida uwa ni shilingi 45,000/=, imepanda mpaka shilingi 55,000 kwa mfuko mmoja wa kilo 50.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingine kwa wakulima ni skimu zile. Kwa kweli skimu zilizo nyingi zina hali mbaya sana. Kwa hiyo, wakulima wanakosa pato kwa sababu skimu zile hazijakarabatiwa kwa muda mrefu. Kule Mbarali kuna skimu moja inaitwa Mwendamtitu, imekuwa ikijaa mchanga mara kwa mara. Halmashauri kupitia mapato ya ndani imejaribu kuzibua, imeshindikana na wale wameomba mkopo kutoka TAB Bank mpaka sasa hivi hawajapata mkopo wowote na baadhi yao hawajavuna kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingine ni mtaji. Wakulima wadogo wale hawana mtaji wa kutosha. Mtaji kwa maana ya kwamba wanaenda benki wanaahidiwa kukopeshwa, lakini ukifika msimu kwamba wanaenda shambani, benki hawatoi mikopo kwa wakati na pengine hawatoi kabisa. Wamekuwa wakinilalamikia. Mwenyewe nimeenda benki kuulizia, mbona hamuwapi wakulima hawa mikopo na msimu unapita? Wananijibu kwamba mtandao haupatikani, waombaji ni wengi, tunaendelea kuchambua, tutawapa tutakapoona majina yao, lakini muda unazidi kwenda, wengi wamekosa mikopo, wachache wamebahatika kukopa na wengine wameenda kukopa kwa watu binafsi, kitu ambacho ni gharama kubwa, kwani riba ni kubwa mno. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wamehangaika, wamepata mikopo, wamepata shida zote hizo, lakini masoko hakuna. Wamevuna mipunga, imejaa ndani na soko hakuna. Kwa mwaka uliopita Mbarali tumevuna tani 275,000 uzalishaji, lakini mahitaji yetu ni tani 125,000 tu. Kwa hiyo, tuna ziada ya tani 150,000; na hizo tani zimekutana na mavuno ya mwaka huu. Kwa hiyo, wamekopa, hawajauza, wamelipa ushuru, tozo mbalimbali, mpunga umekwama ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa haraka haraka nije kwenye suala la masoko ya ndani. Naiomba Serikali iwape NFRA fedha nyingi wanunue mazao yote ya wakulima. Njia nyingine katika kuimarisha masoko ya ndani ni kuanzisha mradi wa Liganga uanze kufanya kazi, watauza mazao yao kule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna tatizo kubwa sana la Tume ya Umwagiliaji, inafanya kazi kule bila mawasiliano na Halmashauri. Wanaenda site, wanaongea na wakulima moja kwa moja; sehemu nyingine wanafukuzwa na sehemu nyingine kuna miradi ya ajabu kabisa ambayo Halmashauri haijui na mingine iko chini ya kiwango. Kwa mfano, tuna bwawa moja Rwanyo pale Igurusi la miaka mingi halifai na ni hatari kwa wananchi pale. Tuliomba Chuo Kikuu Mzumbe waje kutathmini namna ya kurekebisha, wakasema gharama ya marekebisho itazidi gharama hata ya ujenzi. Sasa fedha ya Serikali ndiyo imeisha hiyo, ni hasara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa naomba, ili tuwe na usimamizi mzuri kwa Wilaya ya Mbarali, kwa kweli jimbo lile ni kubwa mno, tunaomba ligawike yawe majimbo mawili au Halmashauri mbili, kwa sababu inapitia mikoa mitatu; imeanzia Mbeya, Njombe, hadi Iringa; na ukiwa katikati pale kwenda upande wa mashariki ni kilomita 97, kwenda magharibi ni 134, jumla ni urefu wa kilomita 231. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mtaalam kwenda kufanya supervision, akienda anarudi usiku kabisa na inabidi anywe Panadol ndiyo alale usingizi na akirudia analazwa. Sasa kwa kweli tuna hali ngumu sana. Kuna miradi mikubwa na mizuri ya ujenzi wa madarasa; mnaenda kule mnaambiwa cement tulimwazima Mwenyekiti wa Kijiji, tuliona itaganda. Mbao, kiongozi fulani tuliona azitumie, fedha hatuna. Kwa kuwa ni mbali mno, tunaomba sana igawanywe iwe Halmashauri mbili na ikiwezekana na Mji wa Lujewa iwe mamlaka kamili.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, muda wako umeisha Mheshimiwa.

MHE. FRANCIS L. MTEGA Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)