Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami leo niweze kuchangia bajeti ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda kuipongeza Serikali chini ya uongozi wake Mheshimiwa Rais wetu, Mama yetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuweza kuisimamia vizuri Serikali yetu kiasi kwamba imekuwa ikiendelea kutekeleza miradi ya kimkakati na miradi mikubwa kwa ufanisi mkubwa pia napenda kuwapongeza wasaidizi wake Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Baraza zima la Mawaziri, kwa namna ambavyo wanachapa kazi usiku na mchana kwa ajili ya kuleta maendeleo kwa wananachi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yetu imeonesha ukomavu, usikivu, unyenyekevu na hekima kubwa na busara kubwa kwa wananchi wake katika kuiendesha nchi yetu, naipongeza sana Serikali yetu. Suala la kutengwa kwa Milioni 500 kila Jimbo suala la kuwekwa tozo ya shilingi 100 kwenye mafuta ni mambo ambayo wananchi wengi yamewafariji sana na ni imani yangu kwamba sasa barabara nyingi zitaweza kupitika muda wote wa mwaka bila kuwa na kikwazo chochote, lakini vilevile kutenga Milioni 600 kwa ajili ya shule za Sekondari ni imani yangu kwamba sasa tunakwenda kutatua changamoto kubwa iliyokuwa inalikabili Taifa letu, changamoto ya mimba za utotoni, pamoja na utoro kwenye shule zetu kwa sababu hapo kabla watoto walikuwa wanasoma shule za mbali sana kwa sababu kwenye Kata zao kulikuwa hakuna shule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pale kwangu Somanga kulikuwa hakuna shule kwa hiyo nina imani kwa kupitia hizi Milioni 600 basi tutapata suluhisho la matatizo na changamoto ambazo zilikuwepo, walikuwa wanasoma umbali wa Kilometa 15 kwenda kwenye Kata za Jirani. Nieleze tu taarifa ya masikitiko kwenye Jimbo langu la Kilwa Kaskazini siku ya tarehe moja ya mwezi huu wa Juni, kulitokea msiba wa mwananchi wangu anaitwa Walivyo Uwiro, katika Kijiji cha Kipindimbi, mkazi wa Kijiji ya Kipindimbi kata ya Njinjo, alifariki dunia kutokana na migogoro ya wakulima na wafugaji, ninamuombea kwa Mwenyezi Mungu aiweke roho yake mahali pema peponi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na tukio hilo na matukio yanayoendelea ambayo kwa kweli hali ya usalama sio nzuri sana kule, kule katika kata za Miguruwe, za Kandawale, pamoja na kata hiyo ya Njinjo niliyoisema na Mitowe ningeomba tu Serikali sasa wakati tunaelekea kutekeleza bajeti ya mwaka 2021/2022 iweze kurekebisha mambo fulani na kutuboreshea mambo fulani ili kuhakikisha kwamba matukio ya namna hii hayajitokezi tena.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninasema hivi kwa sababu tumekuwa na tunu zetu za Taifa ambazo ni amani, utulivu, na mshikamano katika Taifa letu ambazo ni msingi imara kwa maendeleo ya Taifa letu ambazo kwa sasa zinaonekana kule Jimboni kwangu katika baadhi ya kata zimeanza kupungua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali kwa kushirikisha zile sekta ambazo zinahusika kwenye kilimo, ufugaji, pamoja na ardhi watusaidie kuharakisha kuwepo kwa mpango wa matumizi bora ya ardhi, ili kuhakikisha kwamba hii migogoro haiendelei tena. Lakini vile vile ningeomba Wizara ya Mifugo ijikite kwenye kuboresha mazingira bora ikiwemo ujenzi wa malambo, ili kuwafanya wale wafugaji ambao wamehamia katika maeneo yetu wasiwe wanahangaika hangaika sana na kuingia kwenye mashamba ya wananchi na hatimaye kuzua migogoro ya namna hii. Lakini vile vile Serikali kwa kushirikiana na vyombo vyake vya dola basi ijitahidi kufanya operations za mara kwa mara ili kuzuia wahamiaji ambao siyo rasmi ambao kwa kiasi kikubwa ndiyo wanaosumbua na kuleta hii migogoro ambayo ipo sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ninaomba nijikite kwenye sekta ya uvuvi kuna mambo matatu hapa nitayazungumza, kwanza ninaomba Serikali kupitia Wizara ya uvuvi itusaidie kujenga masoko ya kisasa katika maeneo yetu, Pwani yetu ya Bahari ya Hindi ikiwemo Jimboni kwangu Kilwa Kaskazini ni maarufu sana kwenye uvuvi ukifika pale Somanga Samaki wanavuliwa sana, wengine wanasafirishwa hadi nje ya nchi wanapelekwa hadi Spain, Portugal pamoja na Italy na China Samaki aina ya robusta pamoja na prawns pweza wamekuwa maarufu sana kule Kilwa hasa pale Somanga na Kivinje, lakini hali ya masoko kwa kweli ni mbaya lakini wataalam pia wamekuwa wachache kwenye sekta hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano mtaalam ambaye anatoa leseni ambaye yupo chini ya Wizara ya Uvuvi ni mmoja tu kwa Pwani yote ya Mkoa wa Lindi na Mtwara, kwa hiyo mtu akitaka kusafirisha bidhaa zake kama hao Samaki ambao wanauzwa hadi nje nchi wanahangaika sana wale wafanyabiashara. Vilevile ningeomba wavuvi waboreshewe miundombinu ya kuvulia Samaki, vifaa vya kisasa vipatikane lakini vilevile maelekezo kutoka kwa wataalam, wataalam wetu wawe karibu na wavuvi wetu ili kuboresha kipato chao na kipato cha Taifa kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo la utalii wa uvuvi pia kama alivyotangulia kuzungumza Mbunge mwenzangu aliyetangulia bahari ya Hindi ina visiwa vingi, Kilwa peke yake kuna Songosongo, kuna Simaya kuna Ukuza lakini vile vile kuna kisiwa cha Simaya, kwa hiyo niombe iweke mkazo Wizara yetu ya Utalii ikishirikiana na Wizara ya Uvuvi kwenye eneo hilo, hii tunaiita sports fishing iweze kufanyika nchi kama Seychelles , Maldives na Mauritius na nchi ya Mexico na Latin America zimekuwa zimepiga hatua kubwa sana zimekuwa zikiingiza fedha nyingi kila mwaka kupitia hii sport fishing au uvuvi wa utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho niombe kuzungumzia mchezo wa mpira wa miguu, nimefarijika sana kusikia kwenye bajeti yetu kwamba kutakuwa na msamaha wa kodi ya VAT kwenye kuingiza nyasi za bandia ambazo zitatumika kwenye viwanja vyetu, nimefarijika sana kusikia kwamba TFF itapewa jukumu la kusimamia, kwa sababu TFF ndiyo yenye jukumu la kusimamia mchezo wa mpira wa miguu katika nchi yetu na wanajua standards za vile viwanja zinavyotakiwa kuwa, aina ya nyasi bandia zinazotakiwa wanazijua kwa hiyo nafikiri ni jambo ambalo limekaa vizuri, isipokuwa ningeomba kushauri katika eneo moja kwa Serikali yetu niiombe isitoe ile privilege au ile exemption kwa Majiji peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu dhamira ni njema ya kukuza vipaji na kuendeleza vipaji vya vijana wetu, vipaji vimetapakaa nchi nzima kwa hiyo niombe kwenye Majiji, kwenye Manispaa kwenye Halmashauri za Wilaya kote misamaha itolewe ili wenye uwezo wa kununua hizo nyasi waweze kupata huo msamaha wa kodi ya VAT.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ningependa kuizungumzia TFF, TFF ni taasisi ambayo siyo ya kibiashara lakini katika manunuzi yake yote hata mapato ya mlangoni yalikuwa yakitozwa VAT asilimia 18, lakini kwenye mapato ya mlangoni unakuta wanakata kwenye ile gross figure, gross revenue yale mapato ghafi kabla ule mgao wa vilabu na maeneo mengine haujatolewa unakuta wanakata ile asilimia 18, hii imeleta uchungu na inasumbua sana kwa vilabu vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilabu vyetu vingi ni vichanga vinacheza mpira wa ridhaa sio profession football kwa hiyo mwisho wa siku ukikata asilimia 18 ya VAT maana yake unakuwa unavididimiza na kuvifanya vilabu visiwe na mapato ya kutosha, kwa hiyo ningeomba hii ikiwezekana ifutwe na kwa kuzingatia kwamba kama nilivyosema mpira wetu hauendeshwi kibiashara, TFF siyo taasisi ya kibiashara ningeomba ifutiwe hii kodi ya VAT. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile sasa hivi kuna mradi unaogharimu kama Bilioni 10 wa uendelezaji wa vituo vya michezo kule Kigamboni - Dar es Salaam na Tanga tayari pale inaonekana 1.8 Bilioni ambazo zile fedha zimeletwa na FIFA tayari 1.8 Bilioni zitakwenda kwenye VAT kwa hiyo zitapinguza ufanisi kwenye ile miradi ambayo inakwenda kujenga vipaji na kukuza mpira wa nchi hii, ndiyo maana ninasisitiza Mheshimiwa Waziri wa Fedha tusaidie kwanza kuiondoa kwenye legislation ya VAT TFF ili hatimaye iweze kufanya mambo yenye tija. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)