Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii ya kuchangia katika bajeti yetu nzuri ya Serikali ambayo kwa kweli ni bajeti imeakisi mahitaji halisi ya Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijazungumza sana naomba nianze kwa kuunga mkono bajeti hii nzuri inayotia matumaini. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri na Naibu wake Kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu, kaka yangu Mheshimiwa Engineer Masauni, lakini na Katibu Mkuu kaka yangu Tutuba kwa kazi nzuri mliyofanya ya kutuandalia kitu ambacho hata tukikipeleka site kinakubalika. Hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nitumie nafasi hii kumpongeza sana, sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. Tumetoka Mwanza Wabunge wa Mwanza tulikuwa na ziara na Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Rais na sisi tulikuwa tuna jambo letu Mwanza, amefanya kazi kubwa nadhani watu wote mmeiona. Ameionesha dunia kwamba Tanzania kazi inaendelea, ametia saini ujenzi wa meli tano mpya hii ni historia kubwa kwenye maendeleo ya nchi yetu, kwa hiyo tunampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti hii yapo mambo ambayo nafikiria niishauri na mimi kwa Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi. Suala la kwanza niipongeze Serikali kwa juhudi ilizozifanya katika kuimarisha utendaji kwenye Serikali za Mitaa juhudi hizi zimeonekana bayana kwa Serikali kuamua kuanza kuwalipa Madiwani kutoka Serikali kuu, hiyo ni hatua muhimu sana kwenye kuimarisha utendaji kwenye Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Serikali hiyo haijawaangalia Madiwani tu imewaangalia na Watendaji ikawawekea posho za kuwaongeza morali kufanya kazi ni jambo jema sana linahitaji pongezi, lakini na mimi ninayo maboresho ambayo nataka nishauri. Madiwani tumeamua kuwalipa kutoka Serikali Kuu, mimi pia nimewahi kuwa Diwani wa Kata, kazi za Diwani wakati mwingine kwenye Kata zinakuwa ni kazi za moja kwa moja za kushughulika na wapiga kura kwa sababu ndiyo mtu anayeishi nao muda wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali yangu ya CCM itoke kwenye kuhakikisha Madiwani inawalipa posho kutoka Serikali Kuu lakini na posho hizi ziongezwe zifanane na majukumu ya Madiwani. Madiwani bado wanachokichukua ni kidogo kulingana na majukumu yao, tumeongeza kwa Watendaji tukasahau Madiwani, kuwalipa kutoka Serikali Kuu ni hatua mojawapo nzuri, lakini ni lazima tuwaongeze kipato chao ili wakasimamie vizuri shughuli za maendeleo. Nikuambie kumuongeza posho Diwani ni kuiongeza posho jamii anayotoka Diwani, kwa sababu yeye ndiye anayeshughulika na shughuli za kwenye lile eneo muda wote, kwa hiyo hilo naomba niishauri Serikali iliangalie kwa jicho la pili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nimetoka kwenye Jimbo la Sumve, Jimbo la Sumve ni jimbo la wakulima na wafugaji, nilizungumza hapa kuhusu mazao ya chakula kama choroko na dengu kuwekwa kwenye stakabadhi ghalani, kiti kilielekeza wakati wa kujadili Wizara ya Kilimo, kwamba Wizara ya Kilimo sasa kutokana na yale waliyoyakubali kwamba wanayaondoa choroko na dengu na ufuta kwenye stakabadhi ghalani waandike barua kwenda chini kuelekeza waliokuwa wamewaandikia barua kuyaweka mazao hayo kuyatoa, lakini mpaka sasa hiyo waraka haujaandikwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, huko bado kuna usumbufu wa stakabadhi ghalani ninaomba sasa Serikali kwa sababu tunataka bajeti yetu hii iakisi mahitaji ya wananchi iende ikaondoe migogoro na vikwazo vya ukusanyaji wa kodi kwa sababu moja ya kitu ambacho kilipoteza mapato ya Halmashauri ikiwepo Halmashauri ya Kwimba ni kuyaweka mazao haya kwenye stakabadhi ghalani. Jambo hili lichukuliwe kipaumbe ili barua ile itoke iende ikabadilishe hili jambo ili tuweze kukusanya mapato tuweze kutekeleza hii mipango. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaishukuru Serikali sana imeleta pesa kwenye TARURA sasa hivi matatizo hayajaisha lakini walau yamepungua, hata sisi kwenye jimbo la Sumve kuna barabara ambazo zilikuwa hazipitiki sasa kupitia hii milioni 500 tuliyopewa tumeanza kuzitengeneza zinapitika sasa hii ni jambo jema lakini ili tuongeze mapato lazima vikwazo hivi tuvishughulikie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine la watu wa Sumve nimekuwa nikilisema kila mara na nilipata matumaini makubwa Mheshimiwa Rais akiwa Mwanza alielekeza kwamba Serikali sasa inapanga kuijenga kwa lami barabara yetu inayotokea Magu kupitia Bukwimba, Ngudu mpaka Hungumarwa kwa kiwango cha lami. Nilipata matumaini makubwa sana na wakati tunajadili bajeti ya Wizara ya Ujenzi na wenyewe walikuwa wamesha tupangia pesa na kusema wanaanza kujenga kilometa 10, sasa jambo hili naomba nisisitize kupitia mchango huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahadi hii tumekuwa tukiaahidiwa muda mrefu na imekuwepo hii vote muda mrefu, sasa nadhani kupitia bajeti hii imefika sasa wakati huu mpango ambao tumekuwa tukipangiwa kwa muda mrefu sasa na sisi watu wa Kwimba tuonewe huruma tujengewe barabara yetu hii kwa kiwango cha lami kwa mujibu wa ahadi iliyotolewa ili na sisi tufanane na maeneo mengine. Kwa sababu katika bajeti nzuri kama hii, itakuwa si vema kama bajeti hii itaisha itafika kikomo hatujapata jambo hili nasi walau tuweze kusimama kifua mbele tukisema bajeti ya 2021/2022 ilituangalia kwa jicho la tatu watu wa Sumve tukapata barabara hii. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, sijui ni kengele ya ngapi?...

NAIBU SPIKA: Muda wetu umeisha Mheshimiwa malizia.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, muda wangu umeisha. Nakushukuru sana kama nilivyosema tangu awali naunga mkono hoja na naomba yale yaliyoahidiwa kwenye bajeti hii yakatekelezwe nasi tutakuwa pamoja na ninyi kwenye kutenda kazi. Ahsante sana. (Makofi)