Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuchangia hii bajeti muhimu. Nianzie pale walipoishia wenzangu kumpongeza hasa hasa, Mheshimiwa Rais wetu mpendwa kwa jinsi alivyokuwa mbunifu na bajeti yake hii ambayo ni ya kwanza katika utawala wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli hii bajeti imetushangaza wengi katika ubunifu ambao wameuonyesha, lakini pia najua pamoja na yeye na timu yake, timu ya Makamu wa Rais Dkt. Mpango, Mheshimiwa Waziri Mkuu, mpendwa wetu, naye kuna mchango katika bajeti hii, lakini kuna Wizara ya Fedha pamoja na wataalam wote wa Wizara ya Fedha pamoja na Serikali nzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, wewe pia kwenye bajeti hii mchango wako ni mkubwa mno. Nilikuwa najaribu kufanya analysis ya bajeti hii, zaidi ya asilimia 70 ya michango ya Wabunge, nimeangalia kwenye Hansard katika miaka 15 iliyopita, ile michango mizuri yote ya Wabunge imechukuliwa na Serikali safari hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hicho kinaonyesha namna gani sisi kama Wabunge ni muhimu katika utayarishaji wa bajeti. Kwa hiyo lile jukumu letu la msingi la utayarishaji wa bajeti, nafikiri kwa safari hii limefanyika vizuri sana. Kwa hiyo pongezi kwa Bunge lako vile vile pamoja na Wabunge wote kwa bajeti hii nzuri. Nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napongeza hivyo, nikiangalia bajeti hii imezingatia tija kwenye kilimo, imezingatia ushindani kwenye masoko yetu. Vile vile, ukiangalia ni kiasi gani ambapo karibu majimbo yote yameweza kunufaika kwa milioni mia tano ambazo amezitoa Mheshimiwa Rais kwa ajili ya kuziboresha barabara zetu za vijijini, lakini tumeshangazwa vile vile na nyongeza ya milioni 600 kwa ajili ya shule zetu za sekondari katika kata ambazo hazina shule.

Mheshimiwa Naibu Spika, napongeza zaidi hasa kwenye bajeti hii ambayo imeonyesha vile vile kuwa kutakuwa na barabara yetu ya TANZAM, kipande kile cha Igawa mpaka Tunduma ambayo imezingatia vile vile kuwa na njia nne katika kipande cha Uyole mpaka uwanja wetu wa ndege wa Songwe, nafikiri hiyo ni hatua muhimu sana. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa ku-consider hiyo lakini nashukuru kwa ujenzi vile vile wa barabara ya Isyonje kwenda mpaka Kikondo Makete.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru vile vile kwa Barabara ya Mbalizi kwenda Makongorosi. Pia nashukuru kwa kuwemo kwenye bajeti Barabara ya Mbalizi Shigamba ambayo hii ina matawi yake ya kwenda Isongole mpakani na Malawi. Kwa kweli nashukuru sana. Vile vile nashukuru kwa miradi ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilipoiangalia hii bajeti imelenga kwenye kilimo, lakini imelenga zaidi kwenye maandishi. Ukiangalia bajeti hii, hakuna mahali utaona kuna uwekezaji kwenye kilimo, hakuna. Kama kuna uwekezaji ni kidogo mno, wala hata huwezi kuuona, lakini nimeshangazwa badala ya uwekezaji, nimeona bajeti inaonyesha ongezeko la kodi kwa wakulima, ongezeko la kodi ya asilimia mbili kwa kilimo chetu ambacho hakina tija. Kwa kweli Mheshimiwa Waziri aende akaliangalie hilo, pamoja kwenye hotuba yake ya Kiswahili ameonyesha kwamba hiyo kodi haitamgusa mkulima mdogo. Hii kodi haijabagua, kwenye sheria ambayo imeandikwa Kiingereza hii kodi ni kwa mkulima yeyote, hata mtu anayekwenda kuuza kuku, anaenda kuuza mayai kwenye hoteli itabidi akatwe hiyo kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ukiangalia dhima ya kwetu ni kumjenga mkulima, kuwawezesha wananchi wetu ambao ni wengi. Sasa ukianzisha hii kodi ina maana hao wakulima kwa kiasi kikubwa unawaongezea mzigo, kwa vile mfanyabiashara yeye atataka faida, lakini mzigo wa hii kodi utaenda kwa mkulima. Mkulima wa Tanzania leo hii ukimlinganisha na mkulima wa nchi jirani yetu hata kwa kiasi tu cha mahindi, mkulima wa mahindi anazalisha mahindi kwa gharama ya zaidi ya 300,000, lakini mapato yake ya mahindi ni 100,000 na tena hayo mahindi akiyauza NFRA. Sasa huyo mkulima unamtoza kodi kutokana na nini na hii kodi ni ya mapato, mtu apate faida, huyu mkulima hana faida, kwa nini umtoze hii kodi?

Mheshimiwa Naibu Spika, huu uchumi wetu tunaoongelea uchumi shindani, inabidi tujilinganishe na wenzetu. Kwenye kahawa, uzalishaji wa Tanzania kwa mti mmoja ni gram 350 lakini mzalishaji wa jirani yetu Kenya kwa kahawa ya arabika ni karibu gram 400, mzalishaji wa Brazil ni gram zaidi ya 1,200. Sasa wote tunaingia sokoni, tufanye nini ili tumsaidie mkulima wetu aweze kuingia kwenye ushindani kwa vile bei haichagui kwamba hii ni kahawa ya Tanzania, Kenya au Brazil.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nategemea Mheshimiwa Waziri atakapokwenda kuiangalia hiyo bajeti tumsaidie vipi mkulima. Ili uzalishe vizuri unahitaji mbolea. Kwa hiyo tupeleke fedha isiyopungua bilioni 40 kuwasaidia wakulima kwenye ruzuku ya pembejeo, lakini pia tupeleke pesa kwa ajili ya utafiti ili wakulima wetu waweze kuzalisha kwa tija. Kwa hiyo, bado kuna haja ya kuongeza bajeti ya kilimo kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumzia suala la utafiti, nitatoa mfano mdogo tu. Tuna kilimo cha pareto ambayo inatumika kwa ajili ya kuhifadhi mazao. Pale kwenye halmashauri ya kwangu, wakulima wameshaanza kutumia maua ya pareto kwa ajili ya kuhifadhi mazao na imeonyesha kuwa inatumika vizuri zaidi, ina hifadhi kuliko viatilifu vingine. Kwa hiyo ningeomba fedha zipelekwe kwenye Taasisi yetu ya Utafiti ili pareto iingie sasa hivi kwenye uzalishaji wa viatilifu kwa ajili ya kuhifadhi mazao yetu na kupunguza post harvest loses.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naangalia leo kwenye taarifa ya habari kuhusu ushindani na majirani zetu, ushindani na nchi Jirani, wameanzisha sasa hivi sheria ya kuzuia malori ya Tanzania kuingia na kusafirisha mizigo kwenye nchi zao. Sasa tusipojitahidi katika hilo tutajikuta Tanzania tumekuwa kisiwa, bandari yetu itatumika vipi kama hawa wasafirishaji watazuiwa na ukichukulia kwamba hata uboreshaji wa reli yetu nao vile vile una changamoto ambazo zinatokana na majirani hao hao. Namwomba Mheshimiwa Waziri aangalie ni namna gani tuboreshe ushindani katika suala la usafirishaji, likiwemo la kuboresha bandari; la kuboresha reli yetu ya TAZARA, lakini vilevile tuangalie kupeleka meli kwenye Ziwa letu la Tanganyika ili zisafirishe mizigo kwenda Zaire.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli pendekezo langu kubwa ambalo naliona katika bajeti hii, iende ikae chini iangalie ni namna gani ya kumsaidia mkulima. Leo hii mkulima hasaidiwi kwa aina yoyote na hiyo kodi ya asilimia mbili, naomba iondolewe ilikuwepo kwa NFRA, inawezekana labda ni kwa ajili ya kuisaidia NFRA. Naiomba hata kule NFRA na kuondoke ili mkulima aweze kupata bei nzuri na hiyo sio kwa ajili ya mahindi tu, lakini hii asilimia mbili ni kwa mazao yote, kwa hiyo utakuwa ni mzigo mkubwa kwa wakulima wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja nashukuru sana. (Makofi)