Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi hii na mimi kuwa mmoja wa wachangiaji kwenye bajeti ya Serikali. Nitajielekeza sana kwenye namna ya kuonesha mikakati ya upatikanaji wa fedha, lakini pia nitatoa ushauri kwenye namna bora ya kuweka matumizi yaliyo sahihi, ili walipa kodi waweze kujiona wanachokifanya kina tija katika maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kabla sijaanza kwenda katika maeneo hayo nitumie nafasi hii kuipongeza Serikali kwa bajeti hii nzuri na kubwa ambayo wametuletea. Na ninafurahi sana kuwa miongoni kwenye bajeti inayosifiwa kwa sababu, hata Wabunge wazoefu waliosimama wanakiri kwa maneno yao hii ni bajeti ya kwanza yenye faraja kubwa kwa wananchi. Hivyo, najisikia faraja sana mimi, kama Mbunge mgeni jimboni kwenye Bunge hili, kuwa sehemu ya mtu ambaye nasifiwa kupokea bajeti yenye tija ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini baada ya maneno hayo niitumie nafasi hii kuieleza Serikali, kwenye michango yangu ya awali nilipokuwa natoa nilizungumza sana suala la namna bora ya kuwapanga watumiaji wa ardhi, kwa maana ya wakulima na wafugaji katika maeneo mazuri ili kuweza kuongeza vipato vyao waweze kuweza kuisaidia Serikali yao kupata mapato.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa masikitiko makubwa naomba nitumie kidogo muda mfupi kuifahamisha Serikali jimboni kwangu juzi kumetokea tukio la Afisa Kilimo kushambuliwa na mfugaji eti kwa sababu, Afisa Kilimo huyu alikuwa anakwenda kuangalia maeneo ambayo wakulima wameliwa mazao yao, imesikitisha sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nitumie nafasi hii kumpa pole Afisa Kilimo huyu na kumtia moyo huko aliko aendelee kuchapa kazi kwani Watanzania wana lengo la kuzalisha. Lakini pamoja na hayo niwaombe viongozi wa Kata ile ya Ruvu kwenye kijiji kile cha Ruvu Station, waendelee kuwaasa Watanzania wananchi wa eneo lao wawe na amani kwani Serikali yao itachukua hatua stahili kwa wakosaji na wala wasiji-organise kufanya mambo ambayo yatavunja sheria ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo mchango wangu wa kwanza nataka nijielekeze kwenye mapato ya ndani, hasa yanayohusiana na masuala ya halmashauri, halmashauri zetu zimekuwa na vyanzo vingi vya mapato na ni mjumbe wa Kamati ya Utawala wa Serikali za Mitaa. Tulipokuwa tunapitia bajeti zao Halmashauri nyingi nchini hawana vyanzo vipya, vyanzo vyao ni vile walivyozowea siku zote, inaonekana kuna tatizo labda kwenye ubunifu wa vyanzo vipya.

Niiombe Serikali ifike sehemu ikiwezekana iwe inafanya vikao na timu za halmashauri wawasaidie kuwaonesha njia na mipango mbalimbali ya kuanzisha vyanzo vipya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nimegundu kwenye zile taarifa zao mapato mengi ambayo wanayakusanya hawafikii malengo. Na hawafikii malengo nikiangalia inawezekana ni kutokana na kukosa wataalam wanaofahamu ukusanyaji wa mapato. mapato mengi wameyakabidhi kwa watendaji wa vijiji, mapato mengi wameyakabidhi kwa watendaji wa kata, watu ambao tunaamini wana majukumu mengine makubwa wanayoyafanya kwenye maeneo yao. kwa hiyo, ningeiomba Serikali ifanye utaratibu ikiwezekana, ili iweze kusaidia kukuza mapato ya halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, na ukikuza mapato ya halmashauri maana yake unakuza pia pato la uchumi wa nchi hii. Kwa hiyo, ni vizuri zaidi ikiwezekana tunapoitazama TRA kwenye level ya kitaifa tufikirie namna bora ya kuangalia chombo kitakachosimamia mapato ya halmashauri. Kwa sababu, mapato yale yanakusanywa katika mazingira ambayo unaona kabisa kwamba, wakusanyaji inawezekana wanakosa skills za ukusanyaji. Sasa ningeshauri sana Serikali iangalie eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na hapa tukumbuke tu kwenye miaka kdhaa ya nyuma kwenye level za chini za Serikali za Vijiji na Kata kulikuwa na watu wanaitwa ma- Revenue Collectors. Watu ambao walikuwa anafanya kazi ya ukusanyaji wa mapato na takwimu ya mapato yale ilikuwa inatunzwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisemi kwamba, hawa watendaji wa vijiji na kata wanashindwa kufanya au hawana uwezo wa kufanya, lakini najaribu kuyaangalia majukumu yao, wana majukumu ya kusimamia migogoro ya ardhi, wana majukumu ya kuhakikisha wanasimamia majengo, wana kazi ya kuhakikisha kwamba, wageni wanapokuja, Wabunge wanapofanya ziara na wao wapo. Ni muda gani mzuri watapata wa kusimamia mapato katika muda wao wote? Kwa hiyo, ni vizuri Serikali ikajielekeza kuangalia mapato mengi ya halmashauri inawezekana yanapotea kwa sababu chombo kinachokusanya mapato hayo kinakosa uwezo wa kukaa muda wote kusimamia mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine ambalo ningependa kulizungumza ni suala zima kwa wawekezaji. Tukiangalia utaratibu wa nchi yetu na sheria zetu wawekezaji wengi ambao tunawategemea labda wanaweza kuja ku- boost maisha yetu au kipato chetu cha nchi tunatazama sana watu wa kutoka nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaamini kukiwekwa sera nzuri, kukiwa na utaratibu mzuri wa kuhamasisha wananchi wa ndani, ili waweze kuwekeza kwenye maeneo haya ambayo wanawekeza wenzetu kuna uwezekano kukawa na kiwango kikubwa sana cha upatikanaji. Cha msingi hapa Serikali itengeneze mazingira rafiki ya kuwafanya watu waweze kuwekeza na wanapowekeza ndipo watakapoweza kusababisha Serikali ipate fedha kwa sababu watalipa kodi na watafanya shughuli nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sambamba na hilo nizungumzie jambo moja la mfano katika maeneo haya; tumeona Serikali imeweza kuanzisha, TAMISEMI, wameanzisha miradi ya kimkakati. Tangu ianzishwe hii miradi ya kimkakati kwenye nchi hii ni miradi 38 tu ambayo ndio imetimiza sifa, lakini katika miradi hiyo ni miradi sita tu ndio imetekelezwa imekamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo nizungumzie jambo moja la mfano katika maeneo hayo tumeona Serikali - TAMISEMI imeweza kuanzisha miradi ya kimkakati, tangu waanzie hii miradi ya kimkakati kwenye nchi hii ni miradi 38 tu ambayo ndiyo imetimiza sifa, lakini katika miradi hiyo ni miradi sita tu ndiyo imetekelezwa imekamilika. Kwa maana nyingine ni nini pamoja na Serikali ilikuwa ina wazo jema la kuhakikisha kwamba Halmashauri inakuwa na miradi ya kimkakati kuongeza mapato lakini inaonekana fungu la Serikali kwenye kuifanya miradi iliyopitishwa kutekelezwa ni dogo, ningeishauri Serikali ikae chini na mabenki badala ya Serikali wao kupeleka fedha kwenye ile miradi ya kimkakati wawaunganishe na Halmashauri zile, wao Serikali kuu wawe madhamana wa hizo Halmashauri, hayo mabenki waziwezeshe hizo Halmashauri ambazo miradi yao imepitishwa iweze kutekelezwa kwa sababu inavyotekelezwa ni kweli kwamba kipato kitaongezeka na watu wale wataendelea kuhakikisha kwamba wanaingiza mapato ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo langu la pili ninalotaka kuchangia kwa leo ni namna bora ya kutunza matumizi, na matumizi haya yatumike kwa ubora wake ili fedha ziende na ninazungumza hapa kwa kupitia document moja tu ya Mkaguzi wa Serikali. Mkaguzi wa Serikali alipokuwa anafanya ukaguzi kwenye mradi wetu wa mwendo kasi kipande cha kutoka Dara es Salaam mpaka Morogoro inaonesha tu kwa kushindwa kuwalipa wakandarasi kwa wakati Serikali imetumia sio chini ya milioni 11.2 kuwalipa kama adhabu ya kuchelewesha kuwalipa wakandarasi kwa wakati, sasa niwaombe Serikali ni vizuri tukawalipa wakandarasi hawa kwa wakati ili tukaepusha fedha ambazo tunalipa kama adhabu ili hizo fedha zifanya shughuli nyingine, tukifanya hivi hata hii mikakati mikubwa iliyowekwa hapa ya ukusanyaji wa kodi fedha hizo zinaweza zikaenda kwa wakati kwenye maeneo yanayokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Sambamba na hilo kwa maana hiyo sasa ni vizuri sana tukatengeneza utaratibu mzuri na tukaisimamia sheria yetu vizuri wenyewe tukaji-control kwenye matumizi. Wabunge wengi hapa wamepongeza juu ya uanzishwaji wa kodi ya kwenye simu lakini wamesema pia ni vizuri zaidi Serikali ikajielekeza kuhakikisha kwamba fedha hizo zinaelekezwa kwenye jambo ambalo limekusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maana yake ni nini, kama kweli Watanzania hawa ninahakika kabisa kwa bajeti hii ya kwanza wakiona fedha zinazokatwa kwenye simu zao zimefanya kazi kwenye Majimbo yao kwenye barabara zao nina hakika hata mwakani tunaweza tukawaeleza tofauti na tulivyowaeleza mwaka huu na wakaridhika kutoa michango hiyo pasipo tatizo lolote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili nilieleze ndugu zangu, tulitazame kwenye imani zetu za dini, nani anamlazimisha mtu kutoa sadaka, wanatoa sadaka kwa moyo kwasababu wanaamini wanachokifanya wanakifanya kwa sababu ya uwezo wa Mwenyezi Mungu anataka wafanya hivyo, na wanafanya wanaona yale majukumu na ukiangalia kwenye zile sadaka zinazotolewa Makanisani na Misikitini wala hakuna auditor anayekagua kule na watu wanaridhika na wanaendelea kutoa siku zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa serikali watafurahi sana Watanzania hawa wakiona barabara zinajengwa kweli watafurahi wakiona shule zinajengwa kweli, watafurahi wakiona maji yanatoka kwa uhakika, kwa hiyo na mimi naungana na wabunge wenzangu kuiomba Serikali fedha hizi fungeni mikanda na ninyi msizielekeze kwenye matumizi mengine, zielekezeni kwenye matumizi ambayo mmewatamanisha Watanzania waone kwamba ndiyo kitu kinachokwenda kufanyika na ninahakika Watanzania hawa wapo watu ambao wanaweza kutoa kodi hizi pasipo lawama yoyote kama wataona yanayofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi kwa sababu mara baada ya bajeti ile kusomwa nimepokea meseji, nimepokea simu nyingi kutoka kwenye Jimbo langu watu wakipongeza na wananishauri wananiambia hebu sisitiza Serikali tuzione barabara zikitengenezwa kweli, wanasema hebu sisitiza Serikali tukiona huduma ya afya inatolewa kweli tutaweza kutoka kodi zaidi ya hivi na salamu hizi niseme zimetolewa kwa makundi tofauti na wengine ambao wamenitumia salamu hizo na kunipigia simu kunieleza wakitoa pongezi hizo katika hali ya kawaida kwa maisha tunayoishi kule sikutegemea kama wangekuwa sehemu ya watu wanaopongeza, kwa mazingira yetu tunayojua lakini wamepongeza kwa sababu wanaiamini Serikali yao na wana uhakika kinachokwenda kufanyika kitakuwa kikubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)