Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Kavejuru Eliadory Felix

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii adhimu kwanza kumpongeza na kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia kwa kutuletea bajeti nzuri. Nampongeza na Makamu wake Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya. Nampongeza Waziri wa Fedha, Naibu wake, Katibu na watumishi wote wa Wizara ya Fedha. Bajeti waliyoiandaa hakika inatibu kiu ya Watanzania. Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru kwa namna ya pekee Waziri Mkuu kwa Mkoa wetu wa Kigoma jinsi anavyosimamia zao la kimkakati la Mchikichi, Mungu ambariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niingie kwenye hoja ya bajeti. Nimeipitia bajeti, nikaangalia Tanzania sasa hivi inakadiriwa kuwa na idadi ya watu milioni 60. Katika milioni 60, ni 5% tu ndio ambao ni direct tax payer, wanaolipa kodi moja kwa moja. Asilimia tano katika milioni 60 ni sawa na milioni tatu. Ukitoa kwenye milioni 60 unabakiza milioni 57 ambao sio walipaji wa kodi wa moja kwa moja. Nikajiuliza swali: Je, upo uwezekano wa watu milioni tatu kulipa kodi ambazo zitatosheleza Serikali itoe huduma kwa watu milioni 57? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Waziri wa Fedha anisikilize kwa makini tuna kila haja ya kutafuta na kuangalia ni kwa namna gani tunaweza tukapanua wigo wa kodi. Wigo wa kodi ni lazima utokane na kupanua wingi wa shughuli za kiuchumi ndani ya nchi yetu, naomba nishauri, Tanzania tumejaliwa vyanzo vingi. Mungu ametujalia, lakini hatujavifanyia kazi. Mathalani Mkoa wetu wa Kigoma, Mungu ametupa ardhi nzuri, inastawi kila aina ya mazao, lakini ndani ya ardhi hiyo Mungu ametupa madini ya Dolomite ambayo ndiyo malighafi haswa ya mbolea ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Waziri atambue kwamba katika Mkoa wa Kigoma tuna madini ya Dolomite ambayo mimi mwenyewe niliwahi kuhusika kwenye kampuni iliyokuwa ya Kimarekani wakapita wa Anglo American walikuwa kwenye utafiti wa madini, walisema maeneo yafuatayo; Ilagara, Kazuramimba, Basanza, Makere na Kitagata ni maeneo ambayo yana malighafi ya kutengeneza mbolea ya kusaidia nchi hii na tunaweza tukafanya mapinduzi ya kilimo kwa kupata mbolea ambayo inaweza ikatengenezwa ndani ya nchi yetu. Naomba Mheshimiwa Waziri aliangalie kwa jicho la pekee. Wakati wale wa Ngara wanasaidiwa kile kiwanda cha Nikeli na Liganga tuangalie uwezekano wa kuwa na kiwanda cha kutengeneza mbolea katika Mkoa wa Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikijiuliza, kwa nini tunaagiza chumvi kutoka nje wakati sisi kwenye ukanda wa ziwa wa bahari tuna vyanzo vingi vya kutengeneza chumvi? Ukienda kule kwenye Ziwa Eyasi upande Meatu Mkoa wa Simiyu, tuna deposit kubwa ya chumvi. Ukija Kigoma, ile miamba yote ya Uvinza ni chumvi. Kwa nini tusiweke uwekezaji mkubwa na tukazalisha ya kutosheleza na ile fedha ambayo tunaagiza bidhaa ya chumvi nje tukaitumia kwa mahitaji mengine na badala yake tukauza sisi wenyewe?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tuangalie mahali hapo kama sehemu mpya ambapo itakuwa ni chanzo cha mapato ya fedha ya Serikali na chanzo cha ajira kwa waliokosa ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kuendelea, ni lazima tufunge mkanda kwa kufanya mapinduzi katika kilimo chetu. Hata Ulaya waliendelea baada ya kufanya mapinduzi katika kilimo. Tunahitaji sekta ya umwagiliaji ipewe fedha. Zaidi ya hapo kwenye tafiti papewe kipaumbele. Hatuwezi tukasonga mbele kama hatuna tafiti. Tunaomba tafiti kwenye kilimo zipewe kipaumbele, kwenye madini zipewe kipaumbele na kwenye uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kwenye uvuvi nayo ni sehemu ambapo tunaweza tukapata fedha.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante kwa mchango mzuri, mengine unaweza ukamwandikia Waziri, umechangia vizuri sana.

MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono hoja. (Makofi)