Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Ahmed Ally Salum

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Solwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. AHMED A. SALUM: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii adhimu kuchangia kwenye hoja ya bajeti yetu hii nzuri bajeti ya kwanza ya Mheshimiwa Rais wetu mama yetu Samia Suluhu na bajeti ya kwanza kwa Waziri wetu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Waziri wa Fedha. Naomba tu niwasalimie Waheshimiwa Wabunge kwa jina la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

WABUNGE FULANI: Kazi iendelee!

MHE. AHMED A. SALUM: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri bajeti hii inakwenda kumaliza matatizo mengi sana na hasa hasa kwenye maeneo yetu ya vijijini na hasa hasa kwa wananchi na wakulima wanaoishi maeneo ya mbali na miji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni awamu yangu hii ya tatu nakwenda ya nne nimekuwa nikisema mara nyingi sana tupate fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma bajeti hii inakwenda kukamilisha maboma. Katika Jimbo la Solwa lina mabomba zaidi ya 150 ukichukua katika zahanati nina maboma 39 sasa hivi ukienda kwenye elimu ya msingi nina maboma zaidi ya 53, ukienda kwenye Sekondari nina maboma zaidi ya 60.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naishukuru sana Serikali ya Samia kwamba kweli kabisa tunakwenda kutatua matatizo haya ya maboma yetu. Lakini vilevile inakwenda kumaliza kabisa matatizo ya barabara zetu, nina barabara zenye urefu wa kilometa 743 TARURA lakini hakuna barabara hata moja ambayo ilikuwa inanisumbua kama barabara ya kutoka Didia kuja Solwa. Fedha hizi tulizopata Mheshimiwa Dkt. Mwigulu pamoja na Mheshimiwa Rais wetu nikushukuru sana tunakwenda kumaliza matatizo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na barabara ilikuwa ni muhimu kweli kwenye kata zaidi ya sita zenye kulima mpunga zinalima mazao mengi sana mpaka watu wa Burundi na Rwanda wanakuja kununua mazao katika Jimbo la Solwa. Kwa hiyo, kwa kweli hapa sasa hivi wakulima pamoja na wafugaji wa Jimbo la Solwa wamekusikia na wamefurahi sana kwa Serikali yao hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwambie tu Mheshimiwa Waziri wa Fedha tarehe 25 Februari, tulisaini mkataba wa maji Tinde pale kwa agizo la Hayati aliyekuwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli mradi huu ulisainiwa Tinde kwa maana mradi mzima unaitwa Tinde package ni mradi wa maji wa vijiji zaidi ya 15 Jimbo la Solwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tangu tumesaini mradi huu mpaka sasa hivi mkandarasi ameshindwa kuendelea kwa sababu ya suala zima ya VAT kwa maana ya GN. Nikuombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha lishughulikie hili haraka ili mkandarasi aanze kazi aanze kazi mara moja, na mimi nimelisema hivi ili wananchi kwanza wa Jimbo la Solwa wasikie wakusikie wewe waisikie na Serikali yao kwamba tatizo hili sasa limekwisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda nikushukuru Mheshimiwa Waziri umeigusia sana blue print umeigusia sana sana na nikushukuru sana tu umeondoa ile asilimia 15 kwa suala zima la sukari nakadhalika tunakwenda vizuri sasa lakini kuna VAT refund on export hii bado inazuia export ya bidhaa zetu zinazozalishwa ndani ya nchi yetu matokeo yake nini? Biashara yoyote bidhaa yoyote inayozalishwa ndani ya nchi yetu hii unapokwenda kuuza nchi Jirani au nchi za SADC lazima ulipe VAT unapokwenda kwenda kuomba VAT hii na bidhaa tayari imeshatoka bidhaa ikishatoka unatakiwa urudishiwe ile ili uendelee kuzalisha na kwenda kuuza bidhaa nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hii sisi ni tatizo kubwa wafanyabiashara wengi wamekuwa hawafanyi hawa export na hii tatizo kubwa sana inadumaza export leo ninavyokwambia Mheshimiwa Waziri wa Fedha wafanyabiashara wanaokwenda Rwanda kuwekeza waki- target soko la Zaire. Leo wafanyabiashara wengi wanakwenda kuwekeza Uganda waki-target soko la Tanzania na nchi za Zambia kwa sababu hizo nchi ni nchi nzuri sana na ziko mstari wa mbele ku-refund VAT on export product kutokana na manufacturing. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri hili lichukue lifanyie kazi linadumaza export na ukishadumaza export maana yake unadumaza foreign currencies ndani ya nchi yetu utaona kuna tatizo kubwa sana kwenye suala hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitizama Djibouti leo wana free zone kubwa sana inaweza ikawa the second largest au third largest in Africa baada ya Afrika Kusini wamejenga bandari kubwa wamejenga eneo kubwa kweli kwa ajili ya wawekezaji wa viwanda wanaokwenda kuwekeza pale wanataka sasa kuwa katika Afrika wao wawe kama vile Hong Kong kama vile Dubai wanataka kuifanya Djibouti iwe hivyo na Serikali ya China imeisaidia 3.5 bilioni katika mradi mzima ule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tuwe makini na hapa nikushauri Mheshimiwa Waziri atenge fedha kwa ajili ya research development katika Wizara yake. Tenga fedha kwa ajili ya research and development tusiende kichwa kichwa lazima tuwajue wenzetu na nchi Jirani wa Kenya wanafanya nini, Waganda wanafanya nini, Rwanda wanafanya nini Burundi wanafanya nini, Zambia hawa nchi zote zinazotuzunguka ni wapinzani wetu na usifikiri wanafurahia maendeleo yetu kwa namna moja au nyingine wanatizama sera, wanatizama sheria zetu, wanaziweka mezani wanazifanyia kazi ili wawe advantage Zaidi ya sisi Tanzania ndiyo wanavyofanya tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Kenya hapa wanajenga bandari hapa Lamu bandari kubwa sana ambayo tayari inakuwa competitor ya bandari yetu ya Dar es Salaam na Tanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo nilitaka tu Mheshimiwa Waziri wa Fedha lichukue na ikiwezekana tufanye kama wenzetu Ethiopia wamekuwa na maeneo maalum kabisa yaani na wanavyotenga maeneo kwa ajili ya viwanda wawekezaji wa nje na wa ndani ya nchi kwa mfano wanakuwa na strategic zao tunataka kwenda kumaliza matatizo ya masoko ya pamba katika Mkoa wa Shinyanga na Simiyu tunataka kwenda kumaliza masoko kwa mfano ya mazao ya mawese Singida sijui, Singida hapo tunataka kwenda wanakuwa na strategic wanatenga maeneo, wanajenga maeneo wanaweka barabara wanaweka lami, wanaweka umeme wanandaa hili kwa ajili ya viwanda kwa wawekezaji wa viwanda tu atoke nje akija anataka kuwekeza mafuta anaambiwa bwana mafuta ya kula nenda Singida, nenda Kigoma kiwanja hiki hapa na hati hii hapa biashara imeisha nenda kawekeze ndiyo wanavyofanya wenzetu ukienda Thailand hivyo hivyo, ukienda Ethiopia hivyo hivyo yaani hupati shida kabisa kwenye uwekezaji wa nchi kama hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wa Fedha ukishakuwa na East Africa Development haya yote yataangukia kwako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine Mheshimiwa Waziri wa Fedha hii blue print ipige overall yote mnaigusa gusa hivi sawa kabisa mimi nakushukuru kwa namna ambavyo hata haya uliyoyachukua umeyafanyiakazi. Lakini ichukue ipige overall yote kabisa tuimalize ili sasa Tanzania iwe katika nafasi nzuri ya uwekezaji Tanzania tuweze kuwavutia wawekezaji wote wa ndani na nje ya nchi. Tanzania tuna jiografia nzuri bandari yetu iko katikati karibu na nchi zote za SADC Tanzania kuna amani tuna advantage nyingi mno ya watu kuja kuwekeza hapa Tanzania tuna resources nyingi tuna mali nyingi ambayo wawekezaji wanaweza wakaja kuwekeza katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hapa Shinyanga Simiyu peke yake inazalisha asilimia 60 ya pamba inayozalishwa Tanzania hii na mnajua pamba inaajiri watu Zaidi ya milioni 21 lakini hakuna kiwanda kikubwa cha nguo Tanzania hii haipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda kimoja tu India kinanunua pamba yote ya Tanzania hii, hivi tunashindwaje kuwa na Strategic Plan, TPDC, NDC tukamwambia sikiliza chukua hii bilioni 100 jenga kiwanda kikubwa cha pamba hapa, chukua hii bilioni 100 jenga kiwanda cha mafuta hapa, ukishajenga tangaza, uza watakuja wawekezaji, yaani ukishajenga kiwanda ikakaa vizuri Menejimenti kila kitu tangaza uza, chukua fedha jenga kiwanda kingine, tunakuwa na strategic tu, viwanda vikubwa 10 ndani ya nchi hii, nchi inainuka inakwenda vizuri sana katika maendeleo yetu. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Ahmed ni kengele ya pili.

MHE. AHMED A. SALUM: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru naunga mkono hoja. (Makofi)