Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Bupe Nelson Mwakang'ata

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika bajeti hii muhimu. Kwanza kabisa namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uzima na afya Wabunge wote tuliopo humu ndani ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nimpongeze Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu kwa kazi nzuri. Bajeti aliyotuletea kwa kweli, imekidhi viwango, imegusa sehemu zote na matatizo yote ya Watanzania kwa kweli, imeweza kugusa kila nyanja. Tunakushukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze pia Waziri na Naibu wake kaka yangu Mheshimiwa Masauni kwa kazi nzuri na bajeti nzuri waliyotuletea. Kwa kweli, bajeti imekidhi viwango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuwapongeza kwa suala zima la kuwajali bodaboda. Bodaboda kwa kweli lilikuwa ni tatizo kubwa sana, tulikuwa na vijana wetu ambao walikuwa wanavuta bangi, wanajiunga kwenye makundi mbalimbali ambayo sio ya kimaadili, lakini sasa hivi bodaboda wameweza kujiajiri wenyewe. Shida yao ilikuwa ni changamoto hizo za barabarani, za kukamatwa hovyohovyo bila mpangilio. Tunashukuru sana Serikali imeweza kuwajali kwa kuwapunguzia fine kutoka shilingi 30,000 mpaka shilingi 10,000. Hata hivyo, Serikali isiishie hapo tu iendelee kuwalinda hawa bodaboda maana unaweza ukampunguzia bodaboda kwamba, asilipe shilingi 30,000 lakini akaweza kukamatwa mara tano, mara tatu, ikarudi palepale shilingi 30,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Serikali ikimkamata bodaboda kosa moja, basi kosa hilo liendelee mpaka siku nzima iishe. Sio leo asubuhi unamkamata, mchana unamkamata, jioni unamkamata, kwa hiyo, ile shilingi 30,000 itakuwa tena imerudi palepale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningeweza kuishauri Serikali kwamba, hawa bodaboda wangeanzishiwa mafunzo. Bodaboda wengi wanajifunza wenyewe huko mtaani, anajifunza siku tatu, baada ya hapo anaingia barabarani. Hajajifunza kokote, hajajua sheria anaingia barabarani. Naiomba Serikali sasa kwa sababu imewatambua bodaboda na imewapunguzia adhabu basi iwaandalie tena na mafunzo kwa ajili ya kuzijua sheria za barabarani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze tena Serikali kwa kuwakumbuka Madiwani. Madiwani kwa kweli wamekuwa wakifanya kazi kubwa sana huko waliko, lakini naishukuru Serikali imeweza kuwakumbuka. Naiomba Serikali pamoja na kwamba, imewakumbuka kuwalipa posho zao kupitia Serikali Kuu, pia iwakumbuke kwa kuwaongezea posho, lakini pia kwa kuwakopesha angalau hata usafiri wa kuwafikia Watanzania popote pale walipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niipongeze Serikali kwa kuwakumbuka watumishi kuwapandisha madaraja. Hiki kilikuwa ni kilio kikubwa sana kwa watumishi Watanzania, hasa Walimu. Walimu walikuwa kwa muda mrefu hawajapandishwa madaraja na wale waliopandishwa madaraja walikuwa hawajalipwa na wala walikuwa hawapatiwi hata semina zozote za kuongezewa ujuzi, lakini kwa utaratibu huu wa Serikali kuwapandisha madaraja kwa kweli, wamefuta kilio cha Watanzania, wamewaongezea tija Walimu watakwenda klufanya kazi vizuri na watumishi wote kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze pia Serikali kwa kutenga bajeti ya maji. Kwa kweli bajeti hii imekwenda kukidhi matatizo ya wananchi, kwa sababu ukimkumbuka mama kumtua ndoo kichwani, basi unakuwa umelikumbuka Taifa lote kwa ujumla, kwa sababu, hakuna kama mama. Sisi wanawake tulikuwa tunapata tabu sana wakati wa kutafuta maji, tulikuwa tunakwenda mwendo mrefu sana, ndoa zetu zilikuwa ziko hatarini, ndoa zetu zilikuwa zinavunjika, lakini bajeti hii inakwenda kutibu ugonjwa huu. Tunaishukuru sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizi, sasa niingie kwenye hoja zangu za msingi. Nilihudhuria semina moja ya takwimu, Mkoa wa Rukwa uliongelewa kwamba, ndio wa kwanza kwa umaskini. Nilijiuliza kwamba, Mkoa wa Rukwa unakuwaje maskini wakati sisi Mkoa wa Rukwa tuunaweza kulisha hata Tanzania nzima kwa kilimo tunacholima Wanarukwa, lakini inakuwaje tunaambiwa sisi ndio wa kwanza kwa umaskini? Nikajiuliza ni kwa nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipata jibu kwamba, ni kwa sababu ya miundombinu hafifu, barabara zetu hazijakaa vizuri, hasa barabara inayotoka Mkoa wa Songwe, Tunduma kuelekea Sumbawanga Mjini. Barabara ile imejengwa kwa kiwango cha lami vizuri kabisa, lakini tatizo la barabara ile ni matuta. Barabara ile ina kilometa 300, lakini matuta makubwa sana; matuta ni takribani 270, matuta hayo yametuletea matatizo makubwa sana hasa kwa wanaume wengi wanaoendesha magari Mkoa wa Rukwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukipita mara tatu ile barabara kiuno chako kinakosa ushirikiano. Ukiwapima wanaume wanaoendesha magari Mkoa wa Rukwa na hasa wale wanaosafiri mwendo mrefu, mabasi na magari madogo, ukiwapima viuno havina ushirikiano kabisa. Tunaomba sana Serikali katika bajeti hii angalau itupunguzie yale matuta, matuta ni makubwa sana. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata sisi wanawake tunaposafiri ukiwa mjamzito, ujauzito huwezi kufika Mbeya, unaharibika ndani ya gari. Tunaomba barabara hii ipunguzwe matuta yale, matuta yamekuwa ni mengi sana, yamezidi hata kilometa za barabara. Kilometa ni 300 matuta 270 na matuta ni makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, Mkoa wa Rukwa wanasema ni maskini, lakini sisi tuna bandari, bandari ziko tatu; tuna Maziwa mawili, kuna Ziwa Tanganyika halafu na Ziwa Rukwa. Ziwa Tanganyika tuna bandari tatu, bandari hizo hazijaanza kufanya kazi mpaka sasa, naomba katika bajeti hii bandari zile zikifunguliwa tutapata usafiri wa kuvuka kwenda nchi za nje kama Kongo, Zambia, tutasafirisha mazao yetu ambayo yanakosa soko. Kwa mfano mahindi, pale Kongo mahindi wanahitaji sana, lakini tukiwa na bandari inafanya kazi, basi tutaweza kupata soko ambalo linaweza kukidhi mahitaji ya Wanarukwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni uwanja wa ndege. Uwanja wa ndege wa Mkoa wa Rukwa umezungumziwa muda mrefu, lakini naiomba Serikali kwenye bajeti hii basi angalau iikumbuke mikoa hii ambayo inaitwa maskini iikumbuke kwa kujenga miundombinu kama uwanja wa ndege, kufungua hizo barabara, nadhani na sisi tutawafikia wenzetu ambao wamefikia kiwango cha juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)