Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Kunti Yusuph Majala

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru na mimi kunipatia nafasi ili niweze kuchangia bajeti hii ya Awamu ya Sita ambayo tunaianza mwaka 2021/ 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe kuipongeza Serikali. Tangu lilivyoingia Bunge la Kumi na Moja kilio changu kilikuwa ni malipo ya Madiwani kupelekwa Serikali Kuu, hata wakati nachangia Wizara ya TAMISEMI nilisema kwamba tunaomba Madiwani wetu wakalipwe stahiki zao na Serikali Kuu ili kuwaondolea mzigo wa kukopwa…

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, naomba tupunguze sauti tuwasikilize wachangiaji.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iweze kuwalipa Madiwani wetu kupitia Serikali Kuu ili kuwapunguzia mtihani na msalaba mzito waliokuwa wanaubeba Madiwani kwa kukopwa na Wakurugenzi kwenye halmashauri zao. Kwa hiyo niwapongeze sana, na niipongeze sana Serikali kwa kuliona hilo na kuweza kuwapelekea Madiwani kwenda kuwalipa kwenye Serikali Kuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipendekeza hapa wakati nachangia Wizara ya TAMISEMI, kwamba Serikali ikipeleka Madiwani wetu kwenda kulipwa Serikali Kuu tuna watu hawa ambao pia wao ndiyo watendaji wetu wakuu huko chini baada ya Madiwani. Wenyeviti wa vijiji tunao ambao ndio wanafanya kazi kule nikapendekeza kwamba Madiwani tuwapeleke Serikali Kuu ili zile fedha zilizokuwa zinalipa Madiwani ziende na zenyewe zikasaidie kuwalipa posho angalau ya shilingi laki moja wenyeviti wetu wa vijiji, na wao waweze kutekeleza majukumu yao na wajibu wao kwa weledi kuliko sasa wanapata posho ya shilingi 10,000 na wakati mwingine hazilipwi kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini hilo Mheshimiwa Waziri atakwenda kulichukua kama alivyoelekeza Mama, naamini watamshauri vyema, hali kadhalika na mama aweze kuona kwa jicho la kipekee kwa ajili ya kuwasaidia wenyeviti wetu wa vijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende sasa kwenye hotuba ya Waziri na ninaomba nianze na suala zima la kodi ya majengo. Wamesema Wabunge wengi, lakini na mimi naomba niseme hofu yangu kwenye suala zima la kodi ya majengo. Mheshimiwa Waziri anatuambia kwamba itakwenda kulipwa kwa mfumo wa LUKU na kila mwezi italipwa shilingi 1,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kodi ya majengo kwa kila nyumba ni shilingi 20,000. Ukilipa kila mwezi shilingi 1,000 kwa mwaka mzima utakuwa umelipa shilingi 12,000 hii shilingi 8,000 nani anaifidia? Niombe nisaidiwe ufafanuzi kwenye suala zima hili la kodi ya majengo. Lakini ukiangalia tu kwa uhalisia wa kawaida ni kitu ambacho hakiwezekani, kwamba mpangaji niende nikampe huo mzigo wa kulipa kodi ya jengo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kwenye kodi ya majengo pia ametuambia kwamba shilingi 1,000 na shilingi 5,000 kwenye nyumba yenye mita moja, na zile nyumba ambazo zina mita zaidi ya moja zinatengenezewa mfumo wao, ni lini zinakwenda kutengenezewa huo mfumo? Imekuaje watengeneze huo mfumo wa kodi ya jengo kwenye nyumba yenye mita moja wakashindwa kutengeneza huo mfumo wa nyumba yenye mita zaidi ya moja? Kwa hiyo nimuombe Mheshimiwa Waziri aende akakae na timu yake vizuri watengeneze namna bora ambayo tunaweza kwenda kukusanya kodi hii ya majengo ili tuweze kuleta tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2017/2018 nikiwa nachangia bajeti hii nilisema kwamba Serikali imekuwa haipunguzi kodi kwenye vifaa vya ujenzi, lakini inakwenda kuongeza kodi kwenye vifaa vya ujenzi huku wanataka kodi kwenye majengo. Ukiangalia hapa kwenye ongezeko la ushuru wa forodha, Mheshimiwa Waziri amekuja na mapendekezo ya kuongeza ushuru kwenye bidhaa ya mabati asilimia kumi au Dola za Kimarekani 250. Sasa tunataka wananchi wetu waweze kujenga na kuishi kwenye nyumba bora leo unakwenda kuwaongezea kodi huko kwenye hizo bati ni mwananchi gani atakayeweza kwenda kujenga nyumba kwa kwenda kupandisha kodi ya mabati?

Mheshimiwa Mwenyekiti, inaturudisha nyuma tena watu hawa watarudi nyuma, hawataweza kwenda kumudu gharama za kununua mabati na matokeo yake nyumba za mabati zitapungua tutakwenda kuanza kurudi kwenye nyumba za matope za full suit juu na chini kama enzi hizo tulizotoka huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili nalo nimuombe Mheshimiwa Waziri, kama umeamua kuchukua kodi ya majengo tunaomba basi punguza kodi kwenye vifaa vya ujenzi; na kama mnaamua kuchukua kodi kwenye majengo basi huku kwingine tuache ili watu waweze kupumua na waweze kuona ni namna gani wanaweza kuichangia Serikali yao kwenye suala zima la kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye kuzungumzia suala la barabara zetu za kimkakati za kuunganisha mikoa pamoja na wilaya. Ili tuweze kukuza uchumi wetu; na Tanzania sisi tunategemea sana suala zima, la kilimo na kilimo bila barabara hatuwezi kupata tija kwenye kilimo. Sasa sisi mikoa minne, Mkoa wa Tanga, Manyara, Dodoma na Singida tuna barabara yetu ya kutokea Kilindi. Nilisema, kwamba, barabara hii ina ahadi ya marais watatu, Rais Awamu ya Tatu, Rais Awamu ya Nne na Awamu ya Tano waliahidi kuijenga barabara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na barabara hii sisi kwenye uchumi ndiyo barabara itakayoweza kusaidia wakulima wetu kuweza kupata tija kwenye mazao yao. Lakini pili, ni juzi Mheshimiwa Waziri Mkuu amezindua zao la kimkakati kwenye mikoa mitatu, mkoa wa Dodoma, Singida pamoja na Simiyu. Kama barabara hizi hazitakwenda kupitika na hizi ndoto za mazao ya kibiashara ya kimkakati ambayo tunaenda kuyapeleka kwenye maeneo yetu, haya mazao pia itakuja kufikia hatua wananchi wamelima mazao haya lakini watakosa barabara za kuzipitisha mazao haya kwa ajili ya kwenda sokoni na kwenda kwenye viwanda vyetu. kwa hiyo mwisho wa siku hatutakuwa na tija kwenye suala zima la malengo ama na matarajio yetu ya kwenda kupandisha uchumi wa taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeiona barabara hii kwenye mpango, lakini kwenye bajeti mmeweka kujenga barabara kilometa 20. Nikuombe Mheshimiwa Waziri, kwa umuhimu wa zao la alizeti ambalo tunalima Mkoa wa Dodoma na Singida niombe barabara hii Mheshimiwa Waziri ukaingalie kwa jicho la kipekee iende ikajengwe kwa haraka ili tuweze kupata tija kwenye suala la zao hili la mkakati ambalo Serikali mmeweza kuliona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusiana tena na suala hilo hilo la ujenzi wa barabara zetu hali kadhalika Serikali imekuwa ikipata kigugumizi sana kwenye suala zima la ulipaji wa fidia. Tunapokwenda kujenga barabara zote na maeneo mengine suala la ulipaji wa fidia Wizara ama Serikali mmekuwa mkipata kigugumizi na kuchelewesha ulipaji wa fidia ambao umetusababishia miradi mingi kushindwa kumalizika kwa wakati na hivyo hasara kwa wakandarasi wetu pamoja na kuchukua muda mrefu kumaliza miradi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mnapokwenda kutekeleza miradi ya kimikakati niwaombe sana, kwa suala la ulipaji wa fidia, fedha hizo zitoke kwa haraka na hatimaye tuweze kuwa tunakwenda kwa kadri ambavyo tunajipangia sisi wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala zima la utekelezaji wa bajeti na nitazisema wizara chache, pia suala zima la utekelezaji wa fedha kwenye miradi ya maendeleo kwenye wizara mbalimbali hali kadhalika Serikali imekuwa na kigugumizi sana. Waziri wa Fedha kwa kweli Wizara yako imekuwa na changamoto kubwa kwa kuwa mmekuwa mkichelewesha kupeleka fedha kwenye wizara zetu. Vilevile hata mkizipeleka pia hamzipeleki kama Bunge lilivyopitisha, mnapeleka kidogo kidogo ambazo mwisho wa siku haziendi kwenda kuleta tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Kilimo kwa kipindi cha miaka mitano Wizara hii imepelekewa fedha za maendeleo asilimia 19.3, lakini Wizara ya Mifugo kwa miaka mitano pia mfululizo wamepelekewa fedha za maendeleo kwa asilimia 21, yaani hata asilimia 30, 50 haijafika. Kwa hiyo tunaona ni kwa namna gani Wizara ya Fedha mnakwamisha maendeleo ya taifa letu kwa kuvuta miguu kwenda kupeleka fedha kwenye shughuli za maendeleo kwa ajili ya kuweza kuleta tija kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Sheria ya Petrol kuongeza tozo ya mafuta ya taa, na Mheshimiwa Waziri pendekezo lake anasema anakwenda kuongeza tozo ya mafuta ya taa ili kudhibiti wafanyabiashara wakubwa wanaokwenda kutumia mafuta ya taa kuchakachua diesel na petrol. Mheshimiwa Waziri yaani umekaa na watalaam wako, mkachakachua, mkapanga, mkapangua mkazichanga karata ukaona mbinu rahisi ama njia rahisi ni kwenda kupandisha mafuta ya taa ambayo ndiyo nishati peke yake iliyobaki kwa wananchi wengi ambao bado hawajafikishiwa umeme vijijini?. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri niombe nenda kwenye suala zima la uongezaji mafuta ya taa hiyo shilingi mia moja uliyoiongeza, hebu nenda kajipangeni upya. Tunafahamu fika, hata wewe Iramba kwako unajua ni vijiji vingapi vyenye umeme? Nenda, watu leo bado wanatumia mafuta ya taa, tunapoendelea kuongeza huu mzigo wa shilingi mia kwa wananchi wetu haikusaidii, hata wewe utakuja kuulizwa ulikuwa na maana gani? tuwaache hawa watu, tafuta namna ya kuwadhibiti hawa wanaochakachua huku, punguza mzigo kwa mtanzania mnyonge asiyekuwa na hatia. Kwa hiyo nenda ukaondoe kodi hii ili wananchi wetu waweze kupata nafuu ya maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ongezeko la shilingi mia moja pia kwenye lita ya kila mafuta ya petrol na diesel; nimalizie tu. Pia hili nalo nikuombe Mheshimiwa Waziri nenda kaliangalie, ukiongeza tozo tena kwenye petrol na diesel hali kadhalika maisha yatapanda, nauli zitapanda, vyakula vitapanda kwa sababu vinasafirishwa, kwa hiyo gharama ya maisha inakwenda kupanda huo mzigo anaenda kubeba mwananchi wa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie la mwisho. Ahadi nyingi za viongozi wetu waliopita zimekuwa zikisemwa humu ndani mara kwa mara na ni wajibu wetu kwa sababu ahadi ni deni; na siku zote ahadi zinazoahidiwa na viongozi wetu kwa mfano Mheshimiwa Rais au Makamu wa Rais ama Waziri Mkuu inakuwa ni taasisi siyo mtu binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mwaka 2015/2020 Serikali Awamu ya Tano iliwaahidi Watanzania kuwapatia milioni 50 kila kijiji, lakini mpaka sasa bado sijawahi kuisikia wala kuiona hii milioni 50. Ahadi ni deni, Mheshimiwa Waziri wa Fedha niombe hii milioni 50, kwa kuwa ni ahadi kama ahadi zingine na wananchi wetu Watanzania waliopo huko bado wana matumaini wanasubiri milioni 50 kila Kijiji, niombe sasa hii milioni 50 kila kijiji itolewe ili wananchi wetu waende wakapate mitaji yenye tija na waweze kujenga uchumi wa taifa lao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa nafasi, nakushukuru sana, ahsante. (Makofi)