Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nakushukuru sana kwa kuniona ili nipate kuchangia kidogo kwenye bajeti hii ya Serikali ambayo ipo mezani kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kumshukuru Mungu sana mwingi wa rehma ambaye ametupa uhai na nguvu hata nikaweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu hili siku ya leo, lakini namshukuru zaidi kwa ajili ya kulipenda sana taifa letu hili. Tumeshuhudia mambo makubwa Bunge hili la 12. Tulianza kushuhudia aliyekuwa Rais wetu Hayati Dkt, John Pombe Magufuli akiapishwa tarehe 5 Novemba, 2020 baadaye na sisi tukaja tukaapishwa, tarehe 13 Novemba, 2020 akaja akazindua Bunge akatoa hotuba nzuri sana. Kwa kiwango kikubwa bajeti hii ya Wizara ya Fedha, bajeti hii ya taifa imebeba maono yaliyokuwa kwenye ile Hotuba ya Marehemu Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii, baada ya yale matukio kwa upendo wa Mungu Rais wetu Mama yetu Samia Suluhu Hassan alichukua kijiti, na tumeshuhudia akifanya mambo yake kwa umahiri mkubwa. Alitupitisha kwenye taharuki ambayo tulipata baada ya kuondokewa na kipenzi chetu, Rais wa Wwamu ya Tano, Dkt. John Pombe Magufuli ambaye alifariki tarehe 17. Alitupitisha kwenye ile taharuki kwa umahiri mkubwa sana na ameendelea kuijenga Serikali na sasa hivi tunaendelea kupaa. Nichukue nafasi hii kumpongeza sana, anafanya kazi nzuri na kila mmoja anaamini hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sasa nichukue nafasi hii kumpongeza sana Waziri Dkt. Mwigulu Nchemba, Naibu wake Mheshimiwa Engineer Masauni, Katibu Mkuu na watendaji wote kwenye Wizara hii ya fedha kwa kazi nzuri ambayo wameendelea kufanya.

Tumeshuhudia uchumi wa nchi yetu ukipanda kwa percent 6.9, lakini pia na hali ya umasikini kupungua kutoka percent 28.2 hadi percent 26.4; haya ni mafanikio makubwa sana. Nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri ambayo anaifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na baada ya hayo machache sasa niseme kidogo kuhusu hii bajeti ambayo imeletwa mbele yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru Wizara imekuwa inasikiliza hoja za Wabunge na hatimaye fedha zimetolewa milioni 500 kwa kila Jimbo kwa ajili ya kuiwezesha TARURA ili wajenge barabara za vijijini. Kwakweli kwa hilo ninaishukuru sana Serikali yetu, ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuliona hilo; kwa sababu Wabunge tumelalamika muda mrefu hapa kwamba hali ya barabara za vijijini ni tatizo na fedha hazitoshi. Kwa kuanzia ameamua kutoa hizo milioni 500, tunaamini kwamba itapunguza yale makali na kelele ambazo tulikuwa tunazipata kutoka kwa wananchi kwa sababu ya ubovu wa baarabara za vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende kwenye sekta ya kilimo. Kama tunadhamiria kweli kweli kuhakikisha kwamba tunakuwa na uchumi wa kijani, kama kweli tumeamua kwamba tufanye kilimo cha uhakikani lazima tuachane na kutazama mawingu, ni lazima turudi sasa tujenge miundombinu ya umwagiliaji ili tuweze kufanya kilimo kinachoeleweka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya kilimo imeajiri Watanzania takribani percent 65 lakini mchango wake kwenye Pato la Taifa ni chini ya percent 25, hiyo hali haina uwiano kabisa na kusema kweli tunapaswa tubadilishe hiyo hali na namna pekee ya kubadilisha na kuhakikisha kwamba nchi inakuwa ya kijani na kwamba tunavuna sawasawa ni tuhakikishe kwamba tunatengeneza miundombinu ya umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninaishi milimani kule Arusha Wilaya ya Arumeru. Kule kuna mvua za kutosha na kila mwaka kunatokea na mafuriko. Mafuriko haya yanakwenda yanaharibu mashamba na miundombinu sehemu za tambarare . Rai yangu kwa Serikali, tuhakikishe kwamba tunavuna maji haya na kuyatumia kwa ajili ya kumwagilia mashamba yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu ahadi za Mheshimiwa Rais. Kwenye hotuba ya Rais ya tarehe 13 Novemba, 2020 alisema atatoa vipaumbele kwenye ahadi zake alizozitoa wakati wa kampeni. Nimkumbushe Mheshimiwa Waziri atenge fedha kwa ajili ya kutekeleza ahadi zile, maana sasa hivi zile ahadi ni wosia, na usipotekeeza wosia unapata laana, na haya maneno si yangu, aliyazungumza Rais wetu mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan wakati akiapisha viongozi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kusema kwamba Halmashauri zetu nyingi zimeendelea kufanya kazi kwa shida kwa kuwa hazina mapato ya ndani. Kwa mfano Halmashauri ya Arumeru mwaka juzi ilikuwa imetengewa fedha kwa ajili ya mradi wa kituo cha mabasi lakini fedha zile zilirudishwa, sijaelewa kwanini ule mradi ulikatizwa. Nimuombe Mheshimiwa Waziri aliangalie hili sasa. Kwamba ili Halmashauri zifanya kazi vizuri zinapaswa ziwezeshwe, watekeleze miradi mkakati kwa kule Halmashauri ya Meru tunahitaji bado kile kituo cha mabasi lakini pia kuna soko la Tengeru, lile soko la Tengeru linatoa huduma kwa wananchi wengi; linatembelewa hata na wananchi kutoka nchi za jirani kuja kufanya biashara na kuja kununua mazao pale. Niombe Serikali iliangalie ili hilo soko liweze kujengwa na kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanafanya biashara zao vizuri kwa ajili ya kuboresha maisha yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado nipo kwenye ahadi za Mheshimiwa Rais, nakumbushia barabara ya King’ori na nitaendelea kuikumbusha, kila nikisimama nitaendelea kuikumbushia; na hizi ni pamoja na ahadi ya kilometa tano ambazo Marehemu aliitoa pale USA River tarehe 6 Oktoba, 2015. Kwa bahati mbaya mpaka leo hakuna hata mita moja iliyojengwa pale USA River pamoja na kwamba ule mji ulishatangazwa kwamba Mamlaka ya Mji Mdogo. Niombe Serikali iendelee kuwazia Mji wa USA River ili uingizwe kwenye ule mpango ule mradi wa TACTIC angalau nao miundombinu yake ijengwe kwa sababu ule mji ni Makao Makuu ya Wilaya ya Arumeru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa muda mfupi huu. Yako mengi yakusema lakini niishie hapa; nashukuru kwa muda ulionipa naunga mkono hoja (Makofi).

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsantse sana.