Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kunipatia nafasi hii ili na mimi niweze kuchangia katika hoja hii muhimu sana ya sekta ya afya, kwa kweli bila afya hatuwezi kuwa hapa ndani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nipongeze sana hotuba ya Kambi ya Upinzani na ile ya Mwenyekiti wa Kamati ya Huduma za Jamii na Maendeleo kwa sababu ndiyo ukweli wenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaenda kuzungumzia statistics za Wizara na uhalisia wa mambo yanavyokwenda kwa sababu mimi ni Mjumbe wa Kamati hii.
Kabla ya kuanza kwa sababu Wizara hii pia inahusika na masuala ya maendeleo ya jinsia, nitoe masikitiko yangu kwa jinsi ambavyo Mheshimiwa Naibu Waziri ambaye anasema kwamba yeye ni balozi wa wanawake ameweza kukemea mambo yaliyotokea nje, lakini yaliyotokea humu ndani ameshindwa kukemea. Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Naibu Waziri kama kweli wewe ni balozi ungekuwa muwazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala zima la upungufu wa wataalam. Ni jambo la kusikitisha na nichukue fursa hii kuipongeza sana Taasisi ya Benjamin Mkapa kwa jinsi ambavyo inafanya kazi kubwa ya kuboresha afya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jambo la kusikitisha na nashangaa Serikali inakuwa wapi. Tumeambiwa na Benjamin Mkapa Foundation wametengeneza theatres tisa, wameshazikabidhi kwa Halmashauri, tena zile za mipakani Rukwa, Kishapu na nashangaa Mbunge wa Kishapu anayesema shapu lakini kwake upungufu wa wauguzi ni 86%. (Makofi)
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, theatre hizi tisa zimekabidhiwa kwa Serikali ni tatu tu zinafanya kazi, sita zipo tu na kuna watumishi lakini hazifanyi kazi, sasa tunajiuliza hii Serikali ya namna gani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili ni vibali, tuna wataalam wa afya 4,491 wame-graduate toka mwaka 2014 mpaka leo hawajapata ajira. Madaktari Wauguzi na wataalam wa maabara wako mitaani, lakini hapo hapo tunasema tuna ukosefu mkubwa wa watumishi, sasa tunajiuliza kuna tatizo gani? Vibali hivi vinaenda kumaliza muda wake tarehe 30 Juni, watu wako nje. Kwa hiyo, naomba tutembee kwenye maneno yetu, tufanye kwa vitendo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tuje kwenye suala la dawa, hapa tunapoongea dawa muhimu yaani essential medicine tuna upungufu wa asilimia zaidi ya 87. MSD ambao wanaohitaji shilingi bilioni 21 kwa mwezi kununua dawa wanapewa shilingi bilioni mbili tu za dawa muhimu. Ina maana kwamba kwa mwaka wanatumia fedha za mwezi mmoja tu. Hii ina maana gani? Ina maana Watanzania zaidi ya asilimia 80 hawapati dawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikirudi kwenye suala la ukosefu wa watumishi na hapa nizungumzie lab technician. Tumetoka kwenye suala zima za symptom yaani mtu haangalii tu dalili zako kwa macho, inatakiwa upimwe majibu yatoke laboratory lakini tuna upungufu wa asilimia 100 kwenye maeneo mengi nchini hapa. Tunaambiwa mikoa ya pembezoni zahanati hazina wataalam hata mmoja. Kwa hiyo, muuguzi au daktari anaenda kwa kukuangalia tu unaeleza historia yako anakupa dawa, ina maana Watanzania wengi wanapata dawa ambazo labda siyo za magonjwa yanayowasumbua. Kwa hiyo, hili ni tatizo kubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ambacho kinasikitisha zaidi ni data tulizopewa za wanawake wanaokufa kila siku. Haiwezekani whether ni za Serikali kwamba ni wanawake 24 au hizo ambazo zinatoka kwenye National Bureau of Statistics kwamba leo wanawake 42 wanakufa kwa siku maana yake ni wanawake 1,300 kwa mwezi, kwa mwaka ni wanawake 15,000 sawa na wapiga kura wa Jimbo moja kule Pemba au Zanzibar. Hatuwezi kama akina mama kukubali hali hii iendelee. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu nchi hii ina uwezo, kama tuliweza kununua magari ya washawasha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia, kama tuliweza kununua magari ya washawasha 777 na ni 50 tu yalitumika kwenye uchaguzi na gari moja nime-google kwa Alibaba ambao ndiyo wanaleta magari lina gharama ya shilingi milioni 150 mpaka 400 lakini tuchukue wastani wa dola 300,000 kwa moja ina maana kwa magari 700 ni dola 210 milioni. Ukizipeleka kwenye hela za Kitanzania ni bilioni 420…
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Shilingi bilioni 420 kwa kata 3,990 tulizonazo Tanzania nzima zingeweza kupata ambulance. Nime-google ambulance moja ambayo tena ni advance inaenda kwa shilingi milioni 105, ukigawanya ina maana kila kata hapa Tanzania ingepata ambulance. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunajiuliza priorities za nchi hii ni zipi, ni afya ya Mtanzania au ni kitu gani? Kwa sababu nimesema magari 77 ya washawasha yangeweza kubaki, tunazungumzia yale 700 yaliyobaki yaani yangetosha kununua ambulance kila kata hapa nchini. Kibaya zaidi hayo magari ya washawasha yametumika 50 according to data. Sasa tunajiuliza hivi huu utaratibu ukoje? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na mbwembwe sana, tukaambiwa kwamba CT-Scan imenunuliwa, hela zilizokuwa zifanye sherehe ya Wabunge zimenunua vitanda. Tumeenda Muhimbili ile CT-Scan ilitoka UDOM. Sasa watueleze hivi Wagogo na watu wengine wanaoishi Dodoma hawahitaji kutibiwa? Vilevile tunaambiwa hata vitanda vilitoka sehemu nyingine havikununuliwa. Sasa tunataka kujua zile hela za sherehe ya Wabunge zilienda wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la Benki ya Wanawake. Kumekuwa na mazungumzo mengi hapa Bungeni kwa nini hatufungui matawi mikoani. Serikali hii hii ambayo iliahidi kutoa shilingi bilioni mbili kila mwaka kwa ajili ya hii benki hawajatoa. Mwaka huu ukiangalia kwenye kitabu cha maendeleo wametoa shilingi milioni 900. Tuliwashauri Wizara, Wizara hii ina taasisi kubwa nyingi, ni kwa nini taasisi kama ya Bima ya Afya, MSD, NIMR na nyingine wasipitishe fedha zao kwenye benki hiyo ili benki hiyo iweze kukua na kwenda mikoani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisikitika sana Mheshimiwa Waziri alivyomgombeza sana Mkurugenzi wa Benki hii lakini kwa kweli ukiangalia haiwezi kutoa riba nafuu kwa sababu haina fedha. Kwa hiyo, naomba kutoa pendekezo kwa Mheshimiwa Waziri kwamba ni lazima ifike mahali kama Serikali haina fedha iweze sasa kuchukua hayo mashirika niliyoyazungumza waweze kuwekeza fedha zao kwenye benki hii. Vilevile na Wabunge wanawake tunaweza kufungua akaunti kwenye benki hiyo ili iweze kwenda mikoani kusaidia akina mama ambao wanateseka sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie sasa na suala la wazee. Naomba ni-declare interest mimi ni Makamu Mwenyekiti wa Wazee wa CHADEMA Taifa. Wazee nchi hii wanajulikana kwa idadi lakini kibaya zaidi Sera ya Wazee imetungwa toka mwaka 2003 mpaka leo tunavyoongea miaka 14 baadaye hakuna sheria, hakuna kanuni, hakuna mwongozo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli wazee wameteseka sana katika nchi hii, wameuwawa kwa sababu ya macho mekundu lakini hakuna sheria. Leo Waziri anasema mwezi wa tisa wataleta Muswada, tunakushukuru lakini tuseme tu kwamba umechelewa. Tunashukuru kwa hatua hiyo lakini ni kweli umechelewa. Tunaamini sasa huo Muswada na Sheria ikipitishwa, kanuni nazo zitatungwa mara moja ili wazee hawa waweze kuona kwamba wanaishi katika nchi yao kwa amani lakini wajue mchango wao katika nchi hii unathaminika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.