Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano, kwa kazi nzuri anayoendelea kuifanya, lakini pia kwa mwanzo mzuri katika kuongoza nchi yetu katika hii Awamu ya Sita ya uongozi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama walivyotangulia waliomaliza kusema, naomba nitumie nafasii hii kuipongeza sana Saerikali kwa kazi nzuri na kubwa ambayo wameendelea kuifanya na kazi ambayo imeanzwa na ndugu yangu Dkt. Mwigulu Nchemba na Engineer Masauni kwa kweli inatia imani kubwa sana na kwa hakika naamini tunapokwenda ni kuzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi hiki cha bajeti hii ambayo kwangu naiita bajeti ya kwanza ya Uongozi huu wa Awamu ya Sita, ningependa nianze kwa kuwapongeza sana, kwa sababu yapo mbapo ambayo yamefanyika au yameelezwa kwenye bajeti ambayo mimi binafsi nataka niwashawishi Wabunge wenzangu, tuunge mkono moja kwa moja asilimia mia moja ili mambo haya yaende yakafanyiwe kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, lipo jambo la kuondoa ushuru katika bidhaa kwa mfano zinazotoka Zanzibar kuja Dar es Salaam. Hili jambo zuri na limekuwa ni kilio cha muda mrefu na kwa kweli sasa kimeenda kupatiwa muarobaini wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, wameeleza wenzangu waliotangulia, juu ya posho sasa zinazokwenda kulipwa kwa Maafisa wetu Tawala katika maeneo yetu, kwa maana wale Maafisa Tarafa. Pamoja na hilo pia kwa ajili ya sisi wanamichezo; viwanja vya michezo kuondolewa zile tozo za nyasi bandia, kwa kweli ni jambo zuri sana. Alizungungumza juzi ndugu yangu Mheshimiwa Sanga, kwa maelezo marefu sana na sitaki kurudia huko, lakini kwa kweli ni jambo la kupongezwa na tunaishukuru sana Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, nigusie malipo ya wanafayakazi kwa maana ya PAYE, kushusha kutoka 9% mpaka sasa 8%, hili ni jambo kubwa na ni jambo la msingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kutumia nafasi hii kuiomba Serikali yangu kwa sababu yapo mambo pamoja na uzuri wake, lakini pia yamekuwa ni sehemu ya mambo ambayo tunamwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kujibu hapa, atuwekee sawa kidogo. Lipo jambo katika mapendekezo ya Serikali kwenye bajeti hii ya kwamba sasa Mahakama inakwenda kukusanya kodi. Hilo limeelezwa na lilielezwa kwa vizuri sana na Mheshimiwa Waziri, lakini mimi kwa nafasi yangu au kwa masomo niliyosoma, pia nimewahi kufanya kazi mahakamani, nikiwa kama Mwanasheria, lakini pia nikiwa mtu anayesimamia kuona kwamba haki inatokea katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, binafsi, sitaki kuamini kwanza tunakwenda kuipa kazi Mahakama ambao siyo ya kwake. Kwa sababu unapoipa kazi mahakama ya kukusanya kodi, maana yake katika mwongozo wa yale mambo ambayo Serikali inatakiwa kufanya hili sio mojawapo. Sasa Mheshimiwa Waziri atakapokuja kutoa maelezo ya majawabu ya baadhi ya mambo ambayo wachangiaji wameeleza, ningemwomba aliangalie jambo na atueleze vizuri. Ni kwa utaratibu gani mahakama inakwenda kuwa sehemu ya chombo cha kukusanya kodi; maana hatari ninayoiona hapa tusije kufika sehemu mahakama ikalazimika kuwapa watu mafaini makubwa ili mradi tu waweze kutimiza malengo au maelekezo ya Serikali ambayo wamepewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia liko jambo la kivutio chetu au alama yetu Tanzanite. Tanzanite inatambulika kama bidhaa inayotokea Tanzania. Kwa mkakati ambao umefanyika na Wizara ya Madini bado naona kwamba kuna jambo moja halijakaa vizuri, kwa sababu mpaka leo tunapozungumza bado Tanzanite inaonekana kwamba inatokea Kenya, Tanzanite inatokea India na Tanzanite na wakati mwingine inatokea Hong Kong. Sasa kama sisi wenyewe hatutochukua initiative za kuhakikisha kwamba Tanzanite hii inakuwa branded ikaonekana kwamba ni bidhaa ya Tanzania; kwa kweli tunakazi kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kufanya hili juzi Mheshimiwa Rais wakati anazindua Kiwanda cha Kuchenjua, kama itakuwa ndio lugha nzuri, maana nisijekuwa naongea Kikwere hapa, kama itakuwa lugha nzuri hiyo, wakati anazindua kiwanda kule Mwanza, alieleza umuhimu wa Benki Kuu kushiriki katika ununuaji wa madini haya hasa akitia msisitizo katika eneo la dhahabu. Naamini kabisa, kama Tanzanite itatengenezewa mkakati mzuri itakuwa ni sehemu kubwa ya vyanzo vya mapato kwa ajili ya kusaidia uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo pia naomba sana nimpongeze na kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuwa mtu mwenye maono ya mbali. Mheshimiwa Rais juzi alizungumzia juu ya cryptocurrency au wengine wanasema bitcoin ambayo ndio future ya pesa za dunia hii. Tunaona nchi kama Marekani wenzetu wamefikia sehemu sasa wanatengeneza hata sarafu zao kwa kutumia dhahabu na vito vinginevyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwangu mimi kwa wito wa Wizara, wayachukue maangalizo au maono haya ya Mheshimiwa Rais, yakafanyiwe kazi ili tusije kukutwa na sisi kama vile tupo nyuma ya muda wakati dunia imetukimbia mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sanjari na hilo pia jambo la riba alieleza hapa Mheshimiwa mzee Sanga na mimi sitaki kurudia sana lakini ni ukweli usiofichika Mheshimiwa Waziri wa Fedha na wenzake ndani ya Wizara wanayo kazi kubwa ya kuhakikisha kwamba jambo hili linawekwa sawa. Watanzania walio wengi wanalalamika sana, riba zimekuwa kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na riba kuwa kubwa sana, lakini ukopeshaji nao katika mabenki umepungua sana. Sasa inaweza kuwa kuna matatizo huko ndani ya mfumo wa kibenki, lakini kwangu niwaombe sana, Serikali iangalie jinsi ambavyo Benki Kuu inaendelea kusimamia mfumo wa ukusanyaji wa pesa ili mambo yake vizuri katika upande wa riba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, lakini kwa kupitia Mheshimiwa Waziri nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kushusha baadhi ya tozo katika maisha ya vijana. Vijana wengi wao walikuwa wanalalamika sana hasa wale vijana wanaoendesha bodaboda. Juzi tulikuwa tunagawa bodaboda pale Chalinze, niliwakumbusha vijana wenzangu, kwamba hakuna jambo kubwa ambalo Mheshimiwa Rais amelifanya kama kuondoa tozo au faini za bodaboda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo naomba nirudie tena hapa hasa kuongea na vijana wenzangu wa Tanzania. Kuondolewa kwa tozo au kushushwa kwa tozo hizo, si kibali cha sisi kufanya makosa ili Serikali ituadhibu. Tuwe makini sana na huo ni upendo wa dhati ambao Mheshimiwa Rais ameonesha kwetu sisi vijana na tutumie fursa hii kwa ajili kuhakikisha nchi inajengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo pia, nataka nizungumzie jambo la TARURA. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuleta shilingi milioni 500 katika majimbo yetu. Jambo hili ni zuri na kwa kweli kama ni machungu, ametupunguzia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiofichika kwamba TARURA inahitaji nguvu ya ziada. Hizi pesa zilizotolewa na Mheshimiwa Rais, uwe mwanzo wa kupanga mkakati mzuri kwa Serikali kuhakikisha kwamba inaongeza fedha nyingi katika Ofisi za TARURA ili barabara zetu ziweze kukaa vizuri. Kwa mfano, kule Chalinze, huko iko Kata ya Talawanda ambayo kama tusipokuwa makini, kata ile inakwenda kuwa kisiwa. Hakuna njia ya kuingilia wala ya kutokea. Matokeo yake tusipokuwa makini tunaweza kujikuta mwisho wa siku nchi yetu hii inakuwa na maendeleo katika maeneo ya miji lakini siyo kule kwenye vijiji ambapo yanatakiwa maendeleo yaende; na huko ndiko bidhaa kubwa zinakozalishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, kwenye bajeti ya Mheshimiwa Waziri, amezungumza jambo la maji, nami namshukuru sana kwa sababu Wana-Chalinze bado wanaendelea kuishukuru Serikali kwa hatua kubwa wanayoifanya. Ila namwomba sana Mheshimiwa Waziri, tutakapompitishia mafungu yake hapa, pesa hizi za miradi ya maji ziende mapema ili mambo yakakae vizuri katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, leo hii tuna mradi kama ule unaotoka Ruvu unakwenda Mboga, bado mimi binafsi kama Mbunge mwakilishi wa wananchi sijaridhika na ile speed yake. Nafikiri kwamba zikipelekwa pesa na mambo yakawa mazuri zaidi tutaendelea kufanya vizuri. Siyo hilo tu pia hata kwenye miradi ya mabwawa na miradi ya umwagiliaji nako pia tunahitaji sana fedha zifike kwa wakati ili mambo yetu yaweze kukaa vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho lakini siyo mwisho kwa umuhimu, nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano kwa kazi nzuri anayoifanya. Amezungumza na akina mama, amezungumza na vijana leo na uelekeo wake ni maelekezo kwa Serikali na kwetu sisi viongozi tunaoongoza makundi hayo kuweza kwenda kusimamia vizuri ili nchi hii anayoiongoza iweze kwenda katika mstari ulionyooka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Ahsante sana. (Makofi)