Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. ANTHONY P. MAVUNDE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii nami kipekee kabisa kuipongeza Serikali chini ya Rais wetu mpendwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo wamekuja na bajeti inayogusa maisha na maendeleo ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti hii kwa kiwango kikubwa kabisa imeweka mkazo mkubwa kwenye maji, barabara, na naamini kabisa wananchi wangu wa kule Mkoyo, Ntyuka, Michese TARURA wakiongezewa fedha hapa maana yake watakwenda kuwagusa pia na wao kwenye utatuzi wa changamoto hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo naomba nijikite katika maeneo makubwa matatu tu, na ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri Dkt. Mwigulu na Engineer Masauni, Katibu Mkuu Tutuba na Ndugu Alphayo Kidata Kamishna Mkuu wa TRA ninyi wanne nimewataja kwa majina mnao uwezo wa kuacha historia katika nchi yetu, mnao uwezo wa kuifanya nchi hii ipige hatua kwenda mbele, kama tu tutafuatilia ushauri wa Wabunge na kuufanyia kazi hasa katika maeneo ambayo nitayasema hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ninakuamini sana, Mheshimiwa Naibu Waziri nakuamini sana, mnayo nafasi kubwa ya kuacha legacy kwenye nchi yetu. Uchumi wa nchi yetu, maendeleo ya nchi yetu yapo mikononi mwenu ni ninyi sasa muamue kuipeleka nchi hii mbele na kwa umri wenu naamini kabisa mnayo nguvu ya kutosha kulipeleka gurudumu hili mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri la kwanza ambalo nataka nianze nalo Sera ya Fedha – fiscal policy, Mheshimiwa Waziri lazima mipango yetu na mikakati tuliyojiwekea iendane sawa na sera zetu zinavyosema. Ilani ya Uchaguzi ya CCM inasema kuhusu ajira milioni nane, Mheshimiwa Waziri ajira milioni nane hizi zinatokea mikononi mwenu kupitia kanuni, kupitia sera na sheria katika usimamizi wa masuala ya fedha. Hakuna uchawi mwingine wowote isipokuwa hapo Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri tuangalie namna nzuri ya kukuza uwekezaji na kuvutia wawekezaji waje nchini, hiyo ndiyo itakuwa namna nzuri zaidi ya kumsaidia Mheshimiwa Rais kwenye kupatikana ajira hizo milioni nane kwa sababu ajira hizi zitatokana na kazi kubwa ambazo zitafanywa na wawekezaji wa kuja kuwekeza hapa nchini. Mheshimiwa Waziri vipo vitu ambavyo lazima tuviangalie kwa haraka na kuvifanyia kazi mapema sana, lazima tuondoe tozo na kodi zote ambazo zinawatisha wawekezaji. Zipo kodi, zipo tozo ambazo ukiziondoa leo impact yake siyo kubwa sana na ikaathiri mapato ya nchi, lakini ukiziondoa zina mchango mkubwa kuwavutia watu, watu wakiona makodi yamejazana wanakimbia na zipo kodi ambazo hazina mchango mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nikuombe tuipitie tena sera yetu ya fedha tuziondoe kodi hizi. Kwa mfano, kwenye sekta ya utalii, Mheshimiwa Waziri hatuna haja tena ya kuendelea kuongeza tozo, wenzetu wote washindani wetu hakuna mtu kaongeza tozo. Kenya na Rwanda na nchi zingine ambazo zipo karibu nasi wanafikiri kupunguza sisi Mheshimiwa Waziri tunaongeza hii haiwezi kutusaidia ongezeko la tozo hasa katika park fees, land base rent itatuletea changamoto kubwa sana. Nikuombe Mheshimiwa Waziri uliangalie eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri pia nashauri na kupendekeza tufanye mabadiliko ya corporate tax, Mheshimiwa Waziri hivi sasa kodi ya makampuni ni asilimia 30 ya mapato yanayotozwa kodi, Mheshimiwa Waziri ukiangalia Kenya ni asilimia 30, Rwanda asilimia 30, Uganda asilimia 30 nchi nyingi za Afrika ni asilimia 30, Mheshimiwa Waziri kwa nini Tanzania leo tusiishushe kodi ya makampuni kutoka asilimia 30 mpaka asilimia 25 ili kuanza kuwavutia watu wengi zaidi kuja kuwekeza Tanzania, hatupotezi kitu Mheshimiwa Waziri kwa sababu hata ukiiacha mwisho wa siku haumpati mtu anayekuja nchini, umebaki na asilimia 30, lakini ukiipunguza unawavutia wengi na ile deficit utaipata kutoka kwenye pay as you earn, tax ambayo italipwa na kodi zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nashauri pia sheria itungwe kuhusiana na masuala corporate tax kwamba mwekezaji yeyote atakayekuja kuwekeza Tanzania akiwekeza Dar es Salaam na Pwani atozwe asilimia 25, akitoka nje ya Pwani na Dar es Salaam ili kuvutia wawekezaji wengi zaidi atozwe asilimia 12.5 ili watu waende Mbinga, watu waende Njombe, watu waende Ifakara na maeneo mengine, vinginevyo viwanda vitajaa Dar es Salaam tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na Mheshimiwa Waziri ukienda Ghana, Ghana amefanikiwa kupitia hivi. Ghana wanayp programu inaitwa one district, one factory kila wilaya na kiwanda chake, wametoza asilimia 12.5 ya corporate tax ndiyo dunia inapoelekea huko Mheshimiwa Waziri, nikuombe Mheshimiwa naamini hili unaliweza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nikupe mfano mwingine rahisi sana, tukiweka asilimia 25 utawavutia wawekezaji kwa nini aende Kenya kwenye asilimia 30, kwa nini aende Uganda, kwa nini aende Rwanda atakuja Tanzania na kwetu tutakuwa na manufaa makubwa sana. Mheshimiwa Waziri hivi sasa kwa Ulaya nchi ya Ireland ndiyo nchi ambayo inatoza corporate tax asilimia ya chini sana, asilimia 12.5, hivi sasa Facebook makao yake makuu wamepeleka Ireland kwa sababu tu wamevutiwa na corporate tax, nakuomba sana hili eneo uliangalie vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri tunao uwezo wa kufanya jambo kubwa sana na mimi nakuamini sana Mheshimiwa kwa sababu yapo mabadiliko yaliyofanyika hapa, tumeona yalifanyika mabadiliko ya kodi hapa, tulishusha corporate tax katika viwanda vinavyoanzishwa vipya vya masuala ya madawa na ngozi mpaka asilimia 20, lakini viwanda vya kuanzisha vya kuunda magari mpaka asilimia 10 kwa nini hili pia lisiwezekane Mheshimiwa Waziri naomba uliangalie hilo na ninaamini kabisa lipo ndani ya uwezo wako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili naomba sasa tutunge sera ya kuchukua michango ya kuchukua remittance kutoka katika diaspora. Mheshimiwa Waziri wapo Watanzania wenzetu wapo nje ya nchi ambao wana uwezo wa kuchangia maendeleo ya nchi yetu tusiziachie hizi fedha Mheshimiwa Waziri. Kwa hivi sasa kuna takribani Watanzania 1,300,000 wapo nje ya Tanzania. Mheshimiwa Waziri hawa wana uwezo wakawa wana mchango mkubwa kwenye nchi yetu na maendeleo yetu, niwaombe Serikali mtunge sera maalum ya kusaidia kuwawezesha hawa diaspora kuchangia nchi yao. Mheshimiwa Waziri ukienda Nigeria, Nigeria mwaka 2018/2019 diaspora wa Nigeria wamechangia dola bilioni 25 katika uchumi wa maendeleo ya nchi yao ambayo ni sawasawa na asilimia 83 ya bajeti ya Federal Government of Nigeria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Kenya diaspora wanachangia dola bilioni 2.2, Tanzania ni dola milioni 430. Mheshimiwa Waziri tuwajengee miundombinu rafiki waweze kuchangia katika nchi yetu pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho….

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Lugangira.

T A A R I F A

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru ningependa kumpa taarifa Mheshimiwa Mbunge Anthony Mavunde kwamba Kenya wameweka mazingira wezeshi zaidi kwa diaspora wetu wa Tanzania kuwekeza kwa hiyo hivi sasa diaspora wa Tanzania wanawekeza Kenya kuliko wanavyowekeza hapa Tanzania. Ahsante.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Anthony Mavunde taarifa hiyo unaipokea.

MHE. ANTHONY P. MAVUNDE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa na nimuombe Mheshimiwa Waziri aliangalie hili ili tuweze kwenda mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ni kuhusu riba. Mheshimiwa Waziri jana Mheshimiwa Rais katoa maelekezo pale Mwanza maana yake najua maneno yake ni maelekezo juu ya riba, kaeni na BOT tunawatesa watanzania kwa riba kubwa, riba ya Tanzania ni kubwa sana, asilimia 21, asilimia 22, nani anaweza akakopa akaweza kufanya biashara hapa Tanzania kwa asilimia hizi. Mheshimiwa Waziri kaeni na BOT nendeni mkaangalie hati fungani, mkakae huko asilimia kule zishuke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri tuna CRB - Credit Reference Bureau hivi mimi nikikopa mwaka wa kwanza nimelipa, mwaka wa pili nimelipa mabenki tofauti, tofauti hivi kwa nini nikijakukopa kwa mara ya nne riba yangu iwe ile ile tena huku mmeshaona kuwa mimi ni mlipaji mzuri? Mheshimiwa Waziri hili naomba mlifanyie kazi kwa sababu vinginevyo hata makampuni yetu hayawezi kukua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kushindana na mchina anayetoka China kuja kuwekeza Tanzania anayelipa riba ya asilimia 4 vis-a-vis riba asilimia 21, Watanzania hawataweza kuwa washindani kwenye soko lolote la kibiashara na hasa kwenye ujenzi. Mheshimiwa Waziri nikuombe sana kaeni na BOT, tafuteni namna bora ya kupunguza riba, riba yetu ni kubwa inawaumiza sana watanzania na hasa wafanyakazi wa Serikali, hasa Walimu ukiwaangalia, walimu wengi sana makochi yao na TV zao zipo kwenye taasisi za fedha. Anakopa…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Anthony kuna taarifa huku. Taarifa Mheshimiwa Munde, nenda kwenye mic sasa.

T A A R I F A

MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kuhusu suala zima la riba hasa kwa vijana wetu wa bodaboda, Mama lishe ambao wanakopa Brac, Pride zile taasisi ndogondogo wanapata riba mpaka ya asilimia 30, kwa hiyo jambo hili ni jema tuwaombe BOT wahakikishe wanashusha riba kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge na Mheshimiwa Rais.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Anthony Mavunde.

MHE. ANTHONY P. MAVUNDE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hiyo kwa mikono miwili ni muda muafaka sasa Serikali muone namna nzuri ya kuweza kurekebisha hili vinginevyo tunawatesa sana wafanyabiashara wa Tanzania, tunawatesa sana Watanzania kwa sababu wengi wana changamoto nyingi. Wakienda kuchukua mkopo mwisho wa siku mikopo yenyewe hii hailipiki, lakini vilevile hata wakienda kuchukua mikopo hii kama issue kubwa ni ya risk ambayo na mabenki wanaiogopa zipo namna, wapo watalaam wengi wa uchumi, yupo hata Dkt. Kimei hapa na watalaam wengine kaeni nao wawashauri vizuri namna ya kuweza kufanya, mimi naamini haya mambo yanawezekana kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huku kwenye riba huku. Naunga mkono hoja, nakushukuru sana. (Makofi)