Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Simai Hassan Sadiki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nungwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji jioni hii ya leo. Napenda kutumia fursa hii kuipongeza sana Serikali yangu ya Chama Cha Mapinduzi kwa kuja na bajeti ambayo Watanzania waliokuwa wakiililia kwa muda wa miaka mingi sana. Sambamba na hilo napenda kutuma pongezi za pekee kwa Waziri wa Fedha kwa kuja na bajeti iliyokusanya mawazo ya wananchi. Hiki kinadhihirisha wazi kwamba yeye mwenyewe ni mshabiki na mpenzi namba moja wa wananchi wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa leo, ningependa sana nijikite sana katika masuala ya kilimo. Kwa mujibu wa wasilisho la Waziri wa Fedha, ukiliangalia kwa undani kabisa utabaini kwamba sekta ya kilimo ndio sekta ambayo inaendesha uchumi wa nchi hii. Sekta hii ya kilimo ndio sekta pekee inayowaajiri Watanzania wa kila aina. Hata hivyo, cha kusikitisha licha kwamba sekta hii ya kilimo kuwa ni driving sekta ya uchumi wa nchi bado haijawa na mchango mzuri katika pato Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siri ya mafanikio ya uchumi unaotokana na kilimo ni kuwepo kwa viwanda. Kuwepo kwa viwanda ambavyo vitakuwa vinasindika na ku-process mazao ya kilimo vitatusababishia sisi kuweza ku-control uchumi na mazao yetu yatakuwa na thamani ndani na nje ya Taifa hili. Kwa sababu tukiwa na viwanda vingi ambavyo vina uwezo wa ku-process mazao yetu tutaepuka ile biashara ya kupeleka mazao, malighafi nchi za nje na badala yake tutakuwa tunapeleka products zinazotokana na mazao yale ya mashamba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lazima tukubali kwa miaka mingi sana, kilimo hakikuwa kikiwekwa kipaumbele kinachostahiki. Ndio maana hakikuwa kikichangia kwa asilimia kubwa katika uchumi wa Taifa hili. Labda niseme kuna mtaalam mmoja Profesa wa Chuo Kikuu cha Mzumbe pale, Profesa Aida alisema kwamba mchango wa Serikali katika sekta ya kilimo bado ni mdogo sana, tena ni wa maneno matupu kuliko vitendo. Kwa sababu kasi ya kupunguza umaskini bado haijatekelezwa kwa mujibu wa vile tunavyotarajia.

Mheshimwia Naibu Spika, katika suala zima la kilimo kuna masoko mengi mno duniani. Kuna masoko Nchi za Asia, kuna masoko ya mahindi Nchi za jirani zetu kama Kenya. Bunge hili lina nafasi ya kipekee katika kujadili hotuba na bajeti pamoja na sera za uchumi wa Taifa hili. Katika majadiliano hayo ni lazima tujadili kwa kuangalia vizuri sana faida na hasara zilizokuwemo katika kila bajeti na mpango. Isipokuwa bajeti na mpango iliyowasilishwa juzi na Mheshimiwa Waziri wa Fedha, kiuhalisia kabisa vinakwenda sambamba na uhalisia na wananchi wa nchi hii na vinakwenda kujibu matarajio ya wananchi wa kipato cha chini ambao ni wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna masoko mengi mno duniani, bado hatujaweza kuyatangaza mazao yetu ndani ya nchi na nje ya nchi Kimataifa. Tukiweza kuzitumia vizuri balozi zetu, ukiangalia takwimu za balozi zetu tulizokuwa nazo na ukiangalia matunda na mazao tunayozalisha katika nchi hii, basi utaona bado balozi hazijafanya kazi tunayoitarajia kufanywa. Lazima imefikia hatua Serikali ikae na wakulima, ikae na mabalozi wajue namna gani wana uwezo wa kuyatangaza mazao yetu katika nchi za nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia takwimu za Balozi zetu tulizkuwa nazo, na ukiangalia matunda na mazao tunayozalisha katika nchi hii, bado utaona bado Balozi hazijafanya kazi tunayoitarajia kufanya. Lazima ifikie hatua Serikali ikae na mabalozi wajue namna gani wana uwezo wa kuyatangaza mazao yetu katika nchi za nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoke katika mazao ya kilimo, niende katika sekta ya ufugaji. Tanzania hii ni nchi ya pili kujaaliwa kuwa na mifugo mingi Barani Afrika ikitanguliwa na Ethiopia. Ingawa Ethiopia wana mifugo mingi kutushinda sisi, lakini ardhi yao ni ya jangwa, ni kame. Hawana maeneo safi ya ulishia mifugo ukilinganisha na sisi. Tanzania hii kila unapopita ni ardhi ya kijani. Tuna sehemu nyingi za kulishia mifugo, ardhi yetu imejaaliwa kila aina ya neema, rutuba na baraka lakini bado tunashindwa na nchi kama Ethiopia na Sudan kusafirisha mazao yanayotokana na wanyama. Kuna soko kubwa sana katika nchi za Asia, hususan Arabic Countries, kuna soko la ng’ombe mbuzi na kondoo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ukiangalia kitakwimu, Ethiopia na Sudan ambao ardhi yao ni jangwa, wao wanasafirisha sana mazao ya nyama kuliko sisi. Sasa kitu kama hiki kusema kweli inakuwa inaaibisha sana Taifa hili la Tanzania. Ni kitendo cha ajabu mno, mbuzi au ng’ombe anayetoka Sudan kwenda katika soko la Kimataifa ashinde bei kuliko mbuzi anayetoka Tanzania ambaye kuna kila aina ya neema ya malisho ya wanyama. Ni kitendo cha aibu sana kwamba Tanzania hadi hii leo tunaagiza nyama, tunakula sausage za ng’ombe au mbuzi na kuku wanaotoka Brazil wakati sisi ndiyo ambao tulitakiwa tu-process nyama hizi kusafirisha, lakini sisi tunapokea kutoka nchi za nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lazima Wizara ya Fedha mkae na sekta ya ufugaji mwangalie hili tatizo. Tutumie hizi fursa, tusitarajie kwamba kuna neema nyingine zaidi ambazo za kutunufaisha kama hizi. Kwa sababu kilimo na ufugaji ndizo zinazowagusa moja kwa moja maisha ya masikini wa chini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoke hapo niende nikazungumzie suala zima la mabadiliko ya tabianchi. Juzi katika wasilisho la Mheshimiwa Waziri wa Fedha alizungumza kitu ambacho kilituvutia sana sisi Watanzania hususan Watanzania Visiwani. Nafasi ya Zanzibar na mgawanyo wa Zanzibar katika masuala yanayokuja, pesa zinazotokana na mabadiliko ya tabianchi. Mheshimiwa Waziri alisema kwamba wametenga fedha kwa ajili ya kwenda ku-support kingo za mito Wilaya ya Kaskazini A. Ni wazo zuri sana kwa sababu Zanzibar kwa kiasi kikubwa sasa hivi kuna mabadiliko na kuna athari kubwa zinazotokana na mabadiliko ya tabianchi.

Hata hivyo tungependa Mheshimiwa Waziri aende mbele zaidi, kwa sababu sisi Zanzibar hasa huko Kaskazini A hatuna hata mto unaosafiria hata kwa mtumbwi. Sisi ukiangalia bahari inatulea zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda maeneo ya Nungwi, mwanzo wa kisiwa, ukienda Kaskazi bahari inakula kisiwa, ukienda Magharibi bahari inakula kisiwa, ukienda Mashariki bahari inakula kisiwa. Tulitarajia zaidi kwamba Mheshimiwa Waziri ataacha hiyo process, maana inaonekana kwamba tafiti iliyofanyika labda haikuzingatia wapi iende. Bahari ina athari kubwa zaidi kuliko hiyo mito. Mito ya Zanzibar ni mito ambayo ikinyesha mvua dakika mbili, ikikata hakuna tena mito. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana hili lifanyiwe kazi kwa sababu mabadiliko ya tabianchi, kule Kaskazini A visima vingi sana mwanzo vilikuwa vinatoa maji safi, lakini kutokana na mabadiliko ya tabianchi maji yanapatikana katika visima vile ni maji ya bahari. Sasa hayo ndiyo mambo ya kwenda kuyashughulikia kuliko hizo kingo za mito. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni wazo zuri na kwa mujibu wa haya ambayo kayaelezea Mheshimiwa Waziri naona iko haja ya kukutana na hawa Wabunge wa Kaskazini kuweza kumpa ile picha halisi ya yale malalamiko yetu yanayotukabili kutokana na athari za mabadiliko ya tabianchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja mia juu ya mia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.