Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Awali ya yote niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu. Nianze kwa kumpongeza sana Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan hasa kwa kauli yake aliyoitoa akiwa Mwanza kuhusu madini ya Mchuchuma na Liganga. Jana nilikwenda Ludewa Jimboni na kauli ile ilivyotoka nimepokea meseji nyingi sana kutoka kwa wananchi wa Ludewa kwamba sasa Mama yetu kweli ameikumbuka Ludewa kwa kuanzisha miradi hii na wanaomba sana viwanda vijengwe eneo lile lile la Ludewa, ili kuweza kufanya kitu ambacho wachumi wanaita diversification of economy na hizo decentration of industries.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii itasaidia sana kupunguza wale vijana wa Mkoa wa Njombe ambao wanahama sana kwenda maeneo ya mbali kutafuta ajira. Kwa hiyo kukiwa na viwanda kule tutapunguza msongamano wa watu kwenye Jiji la Dar es Salaam, Dodoma na Miji mingine mikubwa kama Mwanza na maeneo mengine. Vijana wengine wabaki kule ili na mimi niwe Mbunge ambaye nina nguvu kazi ya kutosha, sio vijana wakishakua wanakwenda kutafuta ajira maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile wameomba sana katika miradi hiyo kuwe na maandalizi ya wale wananchi waweze kupewa elimu waone namna ya kunufaika na hizo fursa; kwa sababu miradi hii inakwenda kunufaisha kwa kiasi kikubwa Taifa letu kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wengine wameeleza. Vile vile tukiwaandaa wananchi na ile local content na ile community base inayozunguka mradi ikaweza kupata manufaa na wakati na Taifa nalo linapata manufaa kutokana na miradi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo wananchi wa Ludewa licha ya kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu, wameomba vilevile wasaidizi wake waiangalie Ludewa kwa macho ya karibu. Kwa sababu imeonekana kuna miradi yake mingi ambayo inakwama; kuna daraja la Ruhuhu limekwama kwa takriban miaka sita. Jana nilikwenda kule Mwenyekiti wa Kijiji alinipeleka pale, wamelima sana mpunga bonde la Ruhuhu, soko lipo Ruvuma kwa sababu Kyela ni mbali, lakini wale wachuuzi wanashindwa kwenda kwa sababu kuna kivuko pale toka mwezi Septemba, 2020 hakifanyi kazi na daraja hilo ndio toka mwaka 2016 limekwama. Kwa hiyo haya yanaweza kusaidia kuleta tafsiri nzuri ya uchumi jumuishi, uchumi shindani iwapo na wananchi wote wanaweza kupata manufaa. Kwa hiyo naomba hilo liweze kuangaliwa kwa karibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulisema hapa pia mradi mwingine ambao umekwama kwa muda mrefu ule wa VETA. Miaka karibu 10, ulichimbwa msingi, wamezungusha mabati, kwa hiyo wananchi wa Ludewa wanajiona wao ni losers wakati wote. Kwa hiyo hili la Mama kuweza kutaja jana kwamba Serikali sasa imepania kuanza kushughulikia Mradi wa Mchuchuma na Liganga limeleta faraja kubwa sana kwa wananchi wa Ludewa na wamekuwa na Imani kubwa sana na Serikali hii na kimsingi mimi sina sababu za kutounga mkono bajeti hii. Kwa hiyo naunga mkono kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono kwa sababu nimeangalia vile vile kuna maeneo kama ya sekta ya afya, kuna changamoto ile ya watu kwenda kupata dawa. Mtu anakuwa na bima ya afya, anakwenda hospitali lakini walikuwa wanachelewa kupata dawa. Kwa hiyo sasa naona kwa bajeti hii inakwenda kumwangalia mwananchi wa chini ili aweze kupata matibabu ambayo ni ya uhakika. Ila tu niiombe Wizara ya Afya waangalie pia baadhi ya sheria ambazo wamezitoa kwenye Vituo vya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna sheria inazuia Kituo cha Afya kumwandikia mgonjwa baadhi ya dawa. Sasa sisi ambao tupo maeneo ya pembezoni, kuna mwananchi anatakiwa kutembea kilometa 140 kutoka Mavanga mpaka Ludewa kwenda kufuata matibabu. Kwa hiyo kama kuna Kituo cha Afya pale Jirani, Daktari aliyopo Kituo cha Afya sasa hivi tunashukuru Serikali imetuletea qualified Doctors, kwa hiyo wangeruhusiwa, lazima tuangalie intension of ile legislation, ile dhamira ya kuweka ile sheria ya kuzuia. Miaka hiyo kulikuwa hakuna wataalam kwenye Vituo vya Afya, sasa hivi tunao. Kwa hiyo miongozo ya aina hiyo kwa kweli tuweze kui-review na kuweza kuruhusu Vituo vya Afya kuandika dawa kwa sababu kuna wataalam wa kutosha. (Makofi)

Mheshiwa Naibu Spika, nipongeze pia agizo moja liliwahi kutolewa na Mheshimiwa Ardhi, Mheshimiwa William Lukuvi kwamba kwenye maeno ya hii miradi mikubwa ya mikakati kama kwenye SGR kufanyiwe mipango ya matumizi bora ya ardhi ili sasa mindset zetu ziweze kubadilika. Zibadilike kwa sababu watu wengi wanavyoona kwamba reli imetoka bandarini na kwenda maeneo mbalimbali, wanadhani iko maalum kwa ajili ya kusafirisha mizigo inayotoka viwandani peke yake au inayotoka nje ya nchi, kumbe maeneo yale ya ardhi ya pembezoni kufanyiwa mipango ya matumizi bora ya ardhi kama ilivyoelekezwa katika Sheria ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi Na. 6 ya mwaka 2007, wananchi wanaweza kutenga maeneo kwa ajili ya kilimo, mifugo na vile vile kuzalisha mazao yakasafiri kupitia reli hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii itasaidia sana kuinua kipato cha wananchi na wanaoishi kandokando ya Reli. Wataweza kuzalisha mazao ya kutosha, kunaweza kukawa hakuna mwingiliano wa matumizi ya ardhi baina ya wakulima na wafugaji, matokeo yake hii reli itapata mzigo wa kutosha, kwa sababu kilimo nacho kinatoa mazao kwa ajili ya viwanda vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa kuangalia lile eneo la malipo ya mbele wakati mwananchi anamiliki ardhi premium. Eneo hili lilikuwa linawasababisha wananchi wengi sana wanashindwa kuchukua hati miliki za ardhi kwa kushindwa gharama. Kwa hiyo kitendo cha kupunguza ada hii ni ukombozi mkubwa sana kwa wananchi hasa wa hali ya chini. Kwangu kule Lugarawa wananchi wale wameanza kufanya mambo ya urasimishaji na Mlangali na maeneo mengine. Naamini nao watamudu kupata hati miliki bila kikwazo. Kwa kweli hii nipende kuipongeza sana Serikali na tuangalie pia maeneo mengine ambayo Waheshimiwa Wabunge wameendelea kuyalalamikia na kushauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi baadhi ya Wabunge wamezungumzia kwenye ile kodi ya Majengo. Ni vema sana tukaziangalia halmashauri zetu ambazo vyanzo vingi vya mapato vilichukuliwa. Kwa hiyo tujitahidi sana kuwaajiri wale vijana waliosoma GIS ile Geographical Information System. Wale wanaweza kukusanya taarifa za majengo yote wakayaweka kwenye mifumo ya kompyuta, ukiwa pale ofisini unaweza ukaona kila jengo na kuweza kujua kirahisi uweze kutoza kodi kiasi gani. Vijana hawa wanasoma katika Vyuo vya Ardhi, kuna Chuo cha Ardhi Tabora na Chuo cha Ardhi Morogoro na vyuo vingine ambavyo vinatoa mafunzo kama hayo wanaweza kusaidia sana kuboresha ukusanyaji wa kodi ya majengo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vile vile nilichokuwa namwomba Mheshimiwa Waziri waangalie hiyo asilimia 15 kupeleka kwenye halmashauri ni changamoto haitoshi, wangefikiria kuongeza ongeza kidogo, kwa sababu Wakurugenzi wengi ukiwaangalia ukiwakuta kama hana ugonjwa wa moyo, basi ana presha au ana kisukari au tatizo lingine. Inakuwa hivyo kwa sababu wana matatizo mengi sana lakini hawana fedha. Kwa hiyo eneo hili tungeliangalia, hata halmashauri zingeachiwa asilimia 50, ingesaidia hata kujenga madarasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimetembelea baadhi ya madarasa kwenye jimbo langu, yana hali duni sana. Unakuta darasa ni la vumbi. Nilikwenda Shule ya Msingi Liunji, nashukuru Serikali ilipeleka fedha pale, lakini ndio maana naomba sasa halmashauri zifikiriwe kuongezewa mapato. Wakurugenzi wataweza kumudu changamoto ndogo ndogo za madarasa na vituo vya afya. Nitatoa mfano kwenye jimbo langu, kuna kata saba ambazo zimejenga vituo vya afya lakini wanashindwa kumalizia. Wakurugenzi wangekuwa na fedha mambo yangekuwa mepesi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo machache, nirudie kumpongeza sana na kumshukuru Rais mpendwa kwa hoja yake ya jana ya Mchuchuma na Liganga. Wananchi wa Ludewa wanampenda, wanamwombea na wanamkaribisha sana Ludewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo machache, nashukuru sana na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.