Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa nafasi uliyonipa nami nijumuike katika kuchangia hii hotuba ya Bajeti ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nami nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri sana anayoifanya kwa Watanzania. Jana tumeona alivyoenda kuzindua kile Kiwanda cha Kusafisha Madini kule Mwanza. Tumeona jinsi anavyoenda kuweka jiwe la msingi kwa ajili ya kile kipande cha Mwanza – Isaka. Kwa hiyo, hii ni kazi nzuri sana ambayo Mheshimiwa Rais wetu ameendelea kuifanya na kuendelea kufuata nyayo vizuri sana za mtangulizi wake bulldozer, Hayati Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nampongeza Mheshimiwa Waziri pia kwa kutuwasilishia hotuba hii nzuri ya bajeti ambayo tutaendelea kuijadili hapa na kushauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na neo la mapato. Mapato unaweza kuyaongeza kwa njia tatu au zaidi ya hizo. Moja, kwa kutumia ukuaji wa uchumi wa Taifa mapato yanaweza kuongezeka; pili, kwa kudhibiti mianya ya upotevu wa mapato pamoja na kuimarisha zile njia zako unazotumia kukusanya mapato; na tatu, kutunga vyanzo vipya vya mapato. Hivi vyote kwa pamoja vinaweza kuongeza mapato ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza na hili moja ambalo nadhani Mheshimiwa Mwakagenda alilizungumza hapa kwamba, kwa nini tunajiuliza kuhusu ile Mahakama ya Rufaa pamoja na Baraza la Rufaa la Kodi pamoja na Bodi ya Rufaa za Kodi, hizi zote zimeshikilia kesi zaidi ya 1,097 ambazo zinaendelea kule na zina hiyo shilingi trilioni 360 na Dola za Marekani milioni 181.4. Mheshimiwa Waziri, kuna shida gani kuimarisha Mahakama zetu za Rufaa, kuimarisha Bodi ya Rufaa ya Kodi, kuimarisha Baraza la Kodi la Rufaa ili hizi kesi zote ziende zikaamuliwe?

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, kwenye bajeti yako umesema kwamba kuna kesi mpya zilizoingia 653 zenye thamani ya shilingi trilioni 2.7. Kwa nini tusiimarishe hizi kesi zikawa zinaamuliwa kwa wakati tukapata mapato? Hapa tunaweza tukakusanya mapato mengi sana ya Serikali. Hatuhitaji kwenda hata kwenye kodi mpya, hizi tu zenyewe katika hili eneo Mheshimiwa Waziri kama tunaweza tukawezesha haya Mabaraza na hizi Bodi kuamua hizi kesi kwa wakati. Kwa sababu yawezekana tu tukawa na upungufu wa Majaji, upungufu wa watendaji, upungufu wa rasilimali fedha. Kwa nini tusipeleke fedha nyingi pale ili hizi kesi zikaamuliwa kwa wakati na mapato haya yaweze kupatikana Mheshimiwa Waziri?

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, ni ukaguzi dhaifu unaofanywa kwenye miamala ya transfer pricing. Miamala hii ya transfer pricing katika nchi yetu tuna kampuni kubwa za Kimataifa 504. MNCE’s ziko 504. Katika 504 tunakagua makampuni matano tu kwa mwaka average ya makampuni matano na miamala sita na haya makampuni yana fedha nyingi sana ambapo nyingine zinapopitia katika utaratibu wa miamala ya transfer pricing, Serikali yetu inapoteza mapato mengi sana. Kwa mfano, katika makampuni 20 tu yaliyokaguliwa yalikuwa na mzunguko wa fedha wa shilingi trilioni 4.2 na kodi iliyokaguliwa ni shilingi bilioni 152 katika lile eneo. Just makampuni 20 yaliyofanyiwa ukaguzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tukienda namna hiyo, kwa mantiki hiyo hiyo, maana yake sasa, kama tutayakagua makampuni yote 504 kwa mwaka, tunategemea kwamba tutapata mzunguko wa fedha zaidi ya shilingi trilioni 105 na tunategemea kodi zaidi ya shilingi trilioni nne katika lile eneo. Tatizo ni kwamba watu wetu wa TRA na hicho kitengo chetu cha ITU, (International Tax Unit) hakijawezeshwa kikamilifu kufanya haya majukumu na matokeo yake hili eneo la transfer pricing tunaendelea kupigwa katika hili eneo. Taifa linaendelea kupoteza mabilioni ya fedha katika hili eneo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, akiwekeza nguvu zake katika hili eneo, tutakusanya matrilioni ya fedha. Hapa tunaweza kukusanya shilingi trilioni nne na zaidi katika hili eneo, lakini ni fedha ambazo hatuzikusanyi na tunapigwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo tunaweza kukusanya mapato ni maeneo tu hayo mengine kama kuziba mianya hiyo kama ya Bandari bubu, ukokotoaji sahihi wa kodi tunaoweza kuufanya katika maeneo; na katika eneo hili peke yake kama tunaweza kufanya vizuri sana, tunaweza kuongeza mapato mpaka shilingi trilioni 4.71.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunao mkataba wa ETS ambao unatumika kukusanya kodi za ushuru wa bidhaa. Mkataba huu umeingiwa tofauti na mikataba mingine. Kwanza, ni mkataba wenye bei kubwa sana, una gharama kubwa sana. Wananchi wanaingia gharama kubwa sana lakini hautoi gawio lolote lile kwa Serikali. Huyu anakusanya fedha zake anakwenda; na sasa hivi haijaelezwa uwekezaji wake ni shilingi ngapi? Haijaelezwa pia hata yeye analipwa shilingi ngapi kwa mwaka? Sasa kutokana na utata huu, kwanza mkataba huu ni lazima uchunguzwe vizuri ili kuona na kuweka uwazi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili mapato yanayopatikana tugawane kama tunavyogawana kwenye mtambo wa TTMS, kwa nini TTMS, kule TCRA tunagawana asilimia 50 kwa 50? Mwekezaji anapata 50 na Serikali inapata
50. Katika huu mtambo wa ETS ambao ni ubia kati ya TRA na kampuni ya CISPA hatupati chochote kama Serikali; na tukigawana hapa tunaweza kupata mapato ya karibia shilingi bilioni 150 kwa fedha anazozipata sasa hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Msajili wa Hazina tunaweza kufanya maboresho madogo tu tukapata fedha nyingi sana. Tuna kampuni nyingi na mashirika mengi sasa hivi ambayo yamekuwa parasite kwenye Taifa ambayo tunalazimika kuyawezesha fedha kila leo badala ya yenyewe kutoa fedha kwa Serikali. Mashirika haya, yanahitaji mtaji tu. Yakipewa mtaji na Serikali yanaweza kutoa gawio kubwa sana kwa Serikali. Sasa hivi tunakusanya mapato kidogo sana na mwaka huu yameshuka kwa zaidi ya shilingi bilioni 81. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, upande wa ardhi hivyo hivyo. Ardhi tuna fedha nyingi kule. Sasa hivi kwa mujibu wa Taarifa ya CAG ana malimbikizo ya shilingi bilioni 61, hatujajua tatizo ni nini kule kwenye ukusanyaji? Huyu naye akiwezeshwa fedha, tunaweza kuongeza mapato. Haya maeneo tunaweza kuongeza mapato hata tukafikia mpaka shilingi bilioni mpya kutoka kwenye kiwango Mheshimiwa Waziri alivyokisia, shilingi bilioni 260 tunaweza tukafikia mpaka hata kwenye shilingi bilioni 300 na zaidi kwenye hili eneo tu la ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye madini na kwenyewe kuna shida kwa sababu masoko yale 39 tuliyoyafungua na vituo vya kuuzia madini 50 vinafanya kazi siku za kazi tu, lakini siku za weekend hazifanyi kazi na kutusababishia kupoteza mapato mengi. Hili eneo pia tunaweza kuongeza mapato mengi. Katika hili eneo tu kwa hesabu zangu nimepata shilingi trilioni 7.1 ambazo zinaweza zikapatikana nje ya bajeti ya Serikali iliyotengwa. Shilingi trilioni 7.1 tunaweza kuzipata tukienda kuimarisha haya maeneo ambayo nimejaribu kuyataja katika huu muda mfupi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la kufanya marekebisho ya Kanuni Na. 15 ya ukokotoaji wa kodi za Kimataifa (transfer pricing) ambapo Waziri anapendekeza kuondoa faini ya asilimia 100 katika miamala ya transfer pricing. Mheshimiwa Waziri, ukifanya hili kosa la kuondoa hiyo faini, nchi yetu utakuwa umeiingiza kwenye mtego wa kupigwa kila siku. Ni bora ukasema unataka upunguze adhabu ili kuongeza compliance, lakini ukisema hawa ma- tycoon hawa ambao wanafanya biashara kubwa na ziko organized na wanahamisha faida kutoka nchini na kuzihamisha kupeleka nchini kwao, unasema wakifanya miamala yao hiyo ya wizi halafu then fine yao ikaondolewa, tutapigwa na hakuna duniani kote ambako sasa hivi wanaweza kuikubali hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata best practice duniani kote, kwa sababu upigaji mkubwa na wizi mkubwa wa kodi sasa hivi uko kwenye eneo la transfer pricing. Ni lazima tukawekeza vizuri kuhakikisha kwamba tunawabana ili kila mtu alipe katika hii miamala. Tuhakikishe kwamba ukaguzi wa kampuni zote 504 unafanyika ili Serikali yetu iendelee kupata fedha zinazostahili. Tukifanya hivyo, mapato ya Serikali tutakuwa tumeyaongeza kwa kiwango kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)