Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwanye Wizara hii ya Fedha. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa bajeti nzuri na pia Naibu wake na wataalam wote.

Mheshimiwa Spika, nilikwenda pale Hazina kwa sababu Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa walikuwa hawakupata zile fedha, nilivyowaona tu wasaidizi wa Mheshimiwa Waziri waliweza kutoa fedha zile kwa asilimia 100. Kwa hiyo, naomba niwe muungwana, nianze kwa kuwashukuru watumishi wa Hazina na naomba sana na awamu ijayo kwa sababu Ludewa na Njombe kuna muda mrefu sana wa mvua muda wa kufanya kazi unakuwa mchache sana, huu mwezi wa tano mpaka wa kumi ndio muda wa kufanya kazi. Ndiyo maana juzi nilimuona hapa Waziri wa Ujenzi baada ya kuona zile barabara zimesimama kwa sababu kule Hazina walikuwa hawajafanya malipo kwa mkandarasi muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo machache, naomba sasa nijikite kwenye hoja ambazo nilikuwa nimejipanga kuzisema kwenye Wizara hii. Niliwahi pia kuzungumzia ile kodi inayoitwa Capital Gain Tax, kodi ambayo inalipwa kwa mwananchi ambaye ameuza ardhi. Kodi hii Serikali inakosa mapato mengi sana kwa namna tu ambavyo sheria zimekaa na namna ambavyo inakusanywa. Kwa hiyo, nina mapendekezo machache ya kuboresha. Moja, naomba sana Wizara ya Fedha ikutane na wataalamu wa Wizara ya Ardhi watafute namna kodi hii iwe inakusanywa na ofisi moja, sanasana Wizara ya Ardhi. Kwa sababu mwananchi akishauza ardhi yake anakwenda kwa Afisa Ardhi anaambiwa aende TRA, wakati uthamini wa kodi wanafanya watu wa Ardhi, kwa hiyo, kunakuwa na mizunguko mwananchi nenda pale nenda pale. Kwa kweli tunampotezea muda sana mwananchi na ili wananchi waone raha kulipa kodi ni muhimu sana ikawa ina mazingira rafiki ya kuweza kuikusanya. Kwa hiyo, tuangalie namna mamlaka moja ikusanye kodi hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile nachoweza kusema ni kwamba ile asilimia 10 ya kodi hii inayokusanywa mwananchi akishafanyiwa uthamini kwa ajili ya kulipa ile kodi ya kuhamisha umiliki wa ardhi, kama umeuza kiwanja milioni 70 akiambiwa asilimia 10 milioni 7, mwananchi anachukua nyaraka zake anaondoka haji tena. Kwa hiyo, hata tukifanya sampling tukasema wananchi ambao wamenunua ardhi hawajaweza kubadilisha wafike tutagundua kwamba kodi nyingi sana hapa iko nje ambayo Serikali ingeichukua tungeweza kuipeleka kwenye miradi na mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vilevile hata namna hii ya kuwa na makisio ya kodi kwa mtu kuonana na mteja moja kwa moja tungeangalia namna ya kupunguza mifumo hii. Kwa sababu tuna wataalamu wanamaliza vyuo vikuu wanaweza kututengenezea mifumo ya computer ambayo tukitengeneza mwongozo mzuri wanaingiza tu data kwenye mifumo hii kodi inakadiriwa, lakini tukimpa mtu binafsi madaraka ya kukadiria kodi, saa nyingine mtu anaweza akakadiria kodi kubwa ili kutengeneza mazingira ya majadiliano kidogo na mwisho wake mazingira ya rushwa lakini ikiwa mtu akifanya mouse click kodi imekuja, kidogo inajenga trust kwa mwananchi. Kwa hiyo, tuondoke kwenye ule mfumo wa manual twende kwenye mifumo ya computer. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile nizungumzie maeneo ambayo hayajapimwa. Ukisoma Sheria ya Usajili wa Ardhi, Sura ya 334, inasema kodi hii inapaswa itozwe kwenye ardhi iliyopimwa tu, lakini kuna maeneo mengi ambayo hayajapimwa, kuna miamala mingi na mikubwa ambako tungeweza kupata kodi nyingi sana. Kwa hiyo, tuangalie maeneo haya ikiwezekana turekebishe sheria ili ituruhusu tukishirikiana na Wenyeviti wa Mitaa, tukawapa hata posho kidogo Wenyeviti wa Serikali za Mitaa, watatusaidia kupata mapato mengi sana ambayo yatalisadia Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, Kibaigwa na sehemu nyingine unakuta mji mkubwa watu wanauziana petrol stations, majengo na ardhi kwa fedha nyingi. Kwa hiyo, unakuta kodi hii maeneo mengine Wenyeviti wa Mtaa wanakusanya na hawatoi risiti. Kwa hiyo, nafikiri ni eneo ambalo tunatakiwa tuliangalie.

Mheshimiwa Spika, maeneo ya vijijini kuna vikundi vinaanzishwa ambavyo vinachukua hadi tenda labda ya kufyeka barabara au kujenga mifereji, vikundi vya akina mama na vijana. Sasa vikundi hivi wanavyotaka kwenda kulipwa malipo yao wanaambiwa wawe na mashine za EFD, halafu wanatambuliwa kama wakandarasi. Mimi nafikiri hili eneo tungeangalia kwa sababu wale wanajikimu tu kwa zile kazi za kufyeka na kutengeneza mitaro miwili/mitatu. Kwa hiyo, kuwaambia wale wawe na EFD machine ambayo inauzwa Sh.590,000 na kuwawekea kama ni sharti la muhimu, nafikiri tungeangalia kwa sababu wale akina mama na vijana wanajikimu tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, vilevile tuendelee kutoa elimu hasa kwa wale wajasiriamali wa vijijini kwa sababu kuna malalamiko kwamba wanakadiriwa kodi kubwa sana. Kwa hiyo, nipongeze sana juhudi za Rais wetu Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kuonesha kwamba eneo hilo sasa anakwenda kuliangalia kwa karibu. Vilevile Mheshimiwa Waziri nimemsikia mara kadhaa ameonesha naye ana dhamira ya kusimamia suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siku moja nilikaa na wananchi pale Jimboni kwangu Ludewa, kundi la wafanyabiashara, wakaniambia kwamba suala la ulipaji kodi kiserikali mwananchi anapaswa awe mzalendo na anatambua umuhimu wake. Hata kwenye Imani, ukisoma Marko 12:17 wale Mafarisayo walimuuliza Yesu, je, ni halali kwa wananchi hawa kwenda kupeleka mapato kwa Kaisari? Kwa hiyo, aliwajibu pale, mpeni Kaisari yaliyo yake Kaisari. Kwa hiyo, hata misingi ya kiimani inatambua umuhimu wa kulipa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia wale maaskari waliambiwa watosheke na mishahara yao, wasichukue zaidi na wasimsingizie mtu mashtaka. Kwa hiyo, haya mazingira ya Afisa wa TRA kukadiria kodi yeye binafsi na siyo mfumo yanajenga mazingira, hasa maeneo ya vijijini kwa mwananchi kukadiriwa kodi kubwa ili kuwe na negotiation na kuwe na malipo ya pembeni. Kwa hiyo, kukiwa na mfumo kwa kweli wananchi wanapenda sana kulipa kodi kwa sababu kwa sasa hivi wanaziona kodi zao zinakoenda; wanaona miradi ya maendeleo inafanyika kwa hiyo, wanapenda kulipa kodi. Kwa hiyo, tukitengeneza mazingira rafiki wananchi watalipa kodi bila shida yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niendelee kusisitiza kwamba wale wafanyabiashara wa vijijini huwa wanaambiwa wanunue zile mashine za EFD. Sasa ile mashine Sh.590,000/= wanaambiwa watarejeshewa lakini unakuta inachukua miaka mitatu mpaka minne kumrejeshea. Mtaji wa mwananchi wa kijijini unaweza ukakuta Sh.1,000,000, sasa ukimwambia mashine Sh.590,000/= kidogo tungetafuta namna nyingine ama Serikali ingekuwa inaziagiza nje na kuhakikisha zinapatikana kwenye ofisi za TRA ili bei ipungue kuliko kuacha wananchi waendelee kununua mashine kwa gharama kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo machache, nashukuru sana ila nimuombe tu Mheshimiwa Waziri wa Fedha pale Hazina akipitapita yale malipo ya Barabara ya Lusitu – Mawengi yafanyike. Ile barabara imejengwa kwa miaka sita haiishi na chanzo kikubwa ni kucheleweshwa malipo kwa mkandarasi, hivi sasa amendoka site.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. (Makofi)