Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa fursa nami ya kuchangia hii Wizara ya Fedha ambayo kwa kweli ni muhimu sana katika uchumi wetu na imekuwa ikifanya vizuri sana katika kipindi chote na hata sasa imeendelea kufanya vizuri sana. Nami niendelee kumpongeza Mheshimiwa Waziri na timu yake, kwa kweli wanafanya vizuri sana tena sana. Ukiangalia hata kwa kutulinganisha na nchi za majirani, nchi yetu imekuwa ikifanya vizuri sana na wenzangu wamezungumzia kipindi hiki ambacho tuna changamoto za kiuchukumi kutokana na janga la Corona, lakini nchi yetu ya Tanzania imekuwa ikifanya vizuri sana tena sana. (Makofi)

Mhehimiwa Spika, napenda kumpongeza vilevile Mheshimiwa Rais, naye kwa kulisimamia hilo na kuendeleza pale alipoishia Rais wetu wa Awamu ya Tano, Hayati Dkt. Magufuli. Tunashukuru sana, tena sana. Namshukuru sana Mwenyekiti, hata kwa jinsi tulivyoendelea na makusanyo. Haya makusanyo yanatakiwa yalindwe. Mimi nitazungumzia yale makusanyo ambayo mara nyingi hayazungumzwi hapa ndani. Makusanyo ambayo ni chanzo kizuri, ni kusanyo linaitwa Cost Serving. Namna ya kupunguza gharama; namna ya kupunguza ufujaji wa fedha; nafikiri Mheshimiwa Waziri ukiangalia hilo, chanzo kipya cha mapato kinaweza kutusaidia sana kutusogeza na kutufikisha mahali pazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kutoa labda mfano mmoja tu wa hivi karibuni. Katika ukusanyaji wa Ushuru wa Forodha kulikuwa na mfumo ambao unaotumika mpaka sasa hivi unaitwa ETS. Ni mfumo mzuri sana, lakini gharama yake ya kuuendesha kwa kweli ni gharama kubwa kiasi ambacho gharama inazidi hata yale makusanyo yenyewe. Kwa hiyo, naomba, kwa haya mafunzo tuliyoyapata kutumia mfumo wa ETS na wenzangu wamezungumzia kuhusu uhaba wa wafanyakazi upande wa TRA; tuimarishe hasa Idara ya TEHAMA ili kazi kama hizi za mifumo kama hii ambayo kwa kweli ni generic, ipo mingi, Serikali isiingie hasara ya kuingia kulipa mkandarasi. Zaidi ya shilingi bilioni 34 zimekuwa zikilipwa kwa mkandarasi na hizi hazingii kwenye Mfuko wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haujaleta manufaa yoyote kwa sababu imeonekana kuwa yale makusanyo yaliyokuwepo kabla ya huu mfumo, hasa katika makusanyo kutokana na vinywaji vya bia, hayakuongezeka. Kwa hiyo, ina maana huu mfumo haujatusaidia. Ulisaidia kidogo kwenye vinywaji vikali spirits ambavyo vimeongezeka spirits kama kwa asilimia 40.

T A A R I F A

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Oran pokea taarifa.

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru, ahsante.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, kuongezea mchango wa Mheshimiwa Oran Njeza, Mfumo wa ETS anaozungumza, hizo shilingi bilioni 34 zinahusu kampuni mbili tu; Kampuni ya Serengeti Breweries na ile kampuni nyingine ya bia. Ni kampuni mbili tu za bia. Tukizungumzia Kampuni ya Sigara wao wenyewe wamemlipa Mkandarasi shilingi bilioni 13. Kwa hiyo, tukifanya majumuisho ya makampuni mbalimbali ambayo yanatumia hii huduma ya ETS kwa kupitia Mkandarasi aliyekuwepo, unakuta kampuni binafsi inapata, Serikali haipati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilikuwa nampa taarifa tu kuchagiza, kuonesha kwa namna gani tunapigwa kwa vitu vidogo vidogo vya teknolojia ambayo kama nchi tunaweza tukawekeza. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Oran, unapokea taarifa hiyo?

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, mheshimiwa exceptionally naomba niipokee taarifa yake, ni nzuri; na huu ndiyo mwelekeo wenyewe.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hiyo, ukichukua hiyo shilingi bilioni 34 ambayo imeongeza pressure ya haya makampuni kuongeza bei, ina maana wakiongeza bei, wateja watakimbia na Serikali itapunguza mapato. Vile vile Serikali inapoteza shilingi bilioni 10 kutokana na hizo, kwa sababu hizo zimepunguza faida kutoka kwenye haya makampuni.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tatizo ni kwamba hasara tunayoipata ni kubwa. Kwa hiyo, naomba tunge-localize; acha hii ETS ifanyike na kampuni za ndani au Serikali yenyewe ichukue hili jukumu. Ukichukulia hizi fedha zote, hizo shilingi bilioni 34 zinakwenda nje, ina maana vile vile inaipa pressure foreign exchange reserve ya kwetu. Kwa hiyo, nilikuwa nasema hizi ni hatua ambazo Wizara ya Fedha inaweza kuzichukua kwa ajili ya kuongeza mapato yetu na vilevile kuimarisha uchumi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kingine, namwomba TR, Msajili wa Hazina kupitia kwa Waziri wa Fedha aangalie kuimarisha yale mashirika ambayo yanaweza kutuletea fedha nyingi kuongeza mapato yetu kwenye Serikali. Nilikuwa naangalia utendaji wa TAZARA. TAZARA kwa kipindi kirefu, kwa miaka 26 Serikali imekuwa ikilipa mishahara ya wafanyazi wa TAZARA, karibu shilingi bilioni 14 kwa mwaka; na hiyo ni asilimia 80 tu, lakini hakuna uwekezaji wowote ambao umepelekwa TAZARA. Hii inatufanya sisi ambao hii Dar es Salaam Corridor, ambayo ndiyo kubwa hapa Tanzania kwa njia ya Dar es Salaam kuelekea nchi za SADC; siyo Tanzania tu, ni kubwa nafikiri kwa Afrika, tunakuwa tunakosa ushindani kwa sababu tunashindwa hata kuwekeza kidogo kwenye TAZARA.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, naomba Serikali iangalie, iwekeze angalau shilingi bilioni 50 kwa mwaka, kwa miaka matatu ili tuokoe TAZARA ili iweze kufanya vizuri zaidi ili iweze kupata fedha za kujenga reli zetu nyingine, ukichukulia kwamba Reli ya TAZARA yenyewe haipo kwenye Mfuko wa Reli.

Mheshimiwa Spika, ni kitu cha ajabu ya kwamba tuna reli muhimu ya TAZARA, Reli ya Uhuru lakini hatuitazami kwa karibu kiasi hicho. Naomba Mwenyekiti shilingi bilioni 50 ziende kwa miaka mitatu ili tuweze kuiokoa TAZARA.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)