Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Daniel Baran Sillo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Spika, kwanza nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangai walau kwa uchache katika Wizara hii ya Fedha na Mipango. Nachukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, Mheshimiwa Naibu Waziri Eng. Hamadi Masauni, Katibu Mkuu pamoja na Manaibu Makatibu Wakuu wote na Watendaji wote wa Wizara ya Fedha kwa ushirikiano wao mkubwa sana kwenye Kamati yetu ya Bajeti, sambamba na hotuba nzuri ya Mheshimiwa Waziri asubuhi hii ya leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naomba kuchukua nafasi hii kumpongeza Makamu Mwenyekiti wa Kamati yetu ya Bajeti kwa kuwasilisha taarifa yetu vizuri, pamoja na wanakamati wetu wote kwa ujumla kwa kweli kwa ushirikiano wao mzuri na umakini wao mkubwa katika uchambuzi wa bajeti mbalimbali ikiwemo bajeti hii ya Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Spika, nitajielekeza katika utendaji wa TRA. Kwanza kabisa nachukua nafasi hii kwa kweli kwa moyo wa dhati kuwapongeza TRA kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kukadiria, kukusanya na kuhasibu mapato ya Serikali yetu, tunawapongeza sana. Nasi wote ni mashahidi, mwaka 2015/ 2016 tulikuwa na wastani wa shilingi bilioni 850, mwaka 2019/ 2020 tuna wastani wa shilingi trilioni 1.5 na lengo hasa ni kufika shilingi trilioni mbili, tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ili TRA iendelee kuboresha makusanyo ya mapato ya Taifa letu, naomba nishauri mambo machache. Jambo la kwanza ni kupanua wigo wa kodi kwa maana ya kuongeza walipa kodi wapya. Tukibaki na walipa kodi wachache hawa kwa miaka mingi, tunawaumiza. Tuongeze wigo wa kodi kwa kuwasajili walipa kodi wapya. Hii inaenda sambamba na kuajiri watumishi wa TRA. Kama kuna upungufu, basi Mheshimiwa Waziri wa Fedha nakuomba sana, tuongeze watumishi wa TRA, wafanye physical surveys, waimarishe block management ili kuwatambua walipa kodi ambao hawako kwenye mfumo.

Mheshimiwa Spika, sehemu ya pili ni kuimarisha mifumo ya TEHAMA katika ukusanyaji, ukadiriaji pamoja na kutoa taarifa sahihi za walipa kodi wetu. Bahati nzuri Ilani ya CCM ukurasa wa 13 umesisitiza sana hili kwamba tuongeze mifumo pamoja na kuongeza walipa kodi pamoja na wigo mpana wa walipa kodi wetu. Hatua hii itarahisha ulipaji wa kodi na kuongeza ulipaji wa kodi wa hiari (voluntary task compliance) na bahati nzuri Mheshimiwa Waziri ameshamteua balozi humu ndani, nadhani kazi inakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni kupata taarifa sahihi za walipa kodi wazawa (resident tax payers) ambao wanafanya biashara nje ya nchi kwa kutumia wale wenzetu ambao tunawa-share mambo ya kodi. Nchi kama Italy, India, South Afrika na kadhalika, kwa sababu Sheria ya Kodi ya Mapato inasema, ni lazima mlipa kodi ajaze returns zake kuonyesha mapato yake ya dunia nzima yaani well wide income, yote iwe tax kwa mujibu wa Sheria ya Kodi ya Mapato. Kwa hiyo, ni vizuri kupata taarifa hii ya mapato sahihi ili tupate kodi sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine kwa kweli ni kuwapatia watumishi wa TRA mafunzo ya ukusanyi wa kodi hasa kwenye biashara za kidijitali. Leo dunia yetu inakusanya kwenye digital economy, kwa hiyo, ni muhimu sana watumishi wa TRA wakapata mafunzo ya kutosha katika mambo ya online businesses; ni maeneo ambayo dunia tulipofika leo. Tusipowekeza kwenye technolojia hii ya habari, kwa kweli tutapoteza mapato mengi ya Serikali yetu.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni maslahi ya watumishi wa TRA naomba sana Waziri wa Fedha waangalie watumishi wa TRA hasa katika upandishaji wa madaraja. Mtu anakaa kwenye daraja moja miaka mitano mpaka saba, anakosa morali ya kazi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri alichukue hili kwa uzito wa hali ya juu, maana hii ndiyo pale hata anashawishiwa na rushwa, maana mtu anakaa daraja moja miaka mitano, saba, mpaka kumi hapandi. Naomba sana liangaliwe kwa jicho la pili.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni kuwapanga wafanyakazi kutokana na maeneo ya kodi. Kwa mfano, mikoa mikubwa ya kodi kama Ilala, Temeke, Kinondoni tupange wafanyakazi kutokana na weledi. Pia nia na malengo kwa mfano kwa Mkoa wa Ilala unakusanya karibia asilimia 80 ya kodi za ndani. Kwa hiyo, kuna umuhimu wa kuwapanga wafanyakazi vizuri hasa kwenye ukaguzi wa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ni ucheleweshaji wa misamaha ya kodi kwenye miradi ya Serikali. Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) section 6 (2) inampa Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango mamlaka ya kutoa msamaha wa kodi kwa kutoa tangazo kwenye Gazeti la Serikali. Hata ukisoma hata pale 2(c) na kadhalika Waziri wa Fedha ana mamlaka ya kuteua Technical Committee, wataalam kutoka Wizara ya Fedha, TAMISEMI, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Wizara ya Fedha yenyewe. Hawa ndio wanaomshauri Mheshimiwa Waziri ili aweze kutoa msamaha huo. Taarifa tulizonazo ni kwamba mizigo inayobaki bandari mingi sasa ni ya miradi ya Serikali kwa sababu ya kutokupata GN. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, miradi hii ni ya kwetu, ni ya Serikali; mradi ni wa Serikali, Waziri ni wa Serikali, timu ya wataalam ni wa Serikali, timu ya watalaam ni wa Serikali, gazeti ni la Serikali, tunakwama wapi? Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri kwa kweli alichukulie kwa uzito mkubwa. Miradi inapokwama, tunachelewesha maendeleo ya nchi yetu wenyewe. Kwa hiyo, namwomba kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, mtani wangu, tafadhali kwenye hili tuache utani, tufanye kazi.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)