Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi wakati huu ya kuweza kuchangia Sekta hii ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwanza siku ya leo kuniamsha nikiwa salama na Mungu akipenda nategemea kutinga pale Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye Uwanja wetu wa Jamhuri pale, ili twende tukaweze kuchuana na hawa TBC. Niwaombe Wabunge wahudhurie, ili waweze kushabikia timu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza, naomba kaka yangu Mheshimiwa Damas Ndumbaro pamoja na dada yangu Mheshimiwa Mary Masanja, nijikite leo kwenye ushauri kuliko kuwapondea sana. Sekta hii ni sekta ngumu sana, maana ni sekta ambayo wanafanya kazi na watu. Ni sekta ambayo Wasukuma wanalia, wafugaji. Niliona jana Mheshimiwa Waziri ametengeneza Operation Ondoa Mifugo Kwenye Hifadhi. Unajua kuna vitu vingine unaweza ukakiona kama tu kitu cha rahisirahisi ukakitengeneza mtu mkubwa, lakini baadaye kikaumiza sana wenzako, binadamu wenzio. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kwa niaba ya wananchi wa Mbogwe. Ninalo pori ambalo ni la Kigosi, namshukuru Waziri ameniahidi kwamba, endapo atapata advantage kwenye ufalme wake atanisaidia kwani lile pori limesahaulika, barabara hazipitiki, hata wale wataalam wa Mheshimiwa Waziri wale wanaolilinda hawana barabara nzuri za kuweza kupitika. Ni vyema sasa muweke kwenye bajeti hii ili barabara ziweze kuchongwa na ziweze kupitika vizuri ili kuweza kupambana na ujangili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya pili niombe tu kuishauri hii Wizara, sheria zibadilishwe, binadamu wathaminiwe kuliko kuthamini tembo pamoja na nyoka na wanyama wakali ambao hawana faida kwetu sisi binadamu. Nikisoma maandiko, sisi binadamu tuliumbwa kwa mfano wa Mwenyezi Mungu, lakini wapo watu ambao wanalinda
kwenye mapori yetu haya hawana huruma, ni watu ambao kweli wanatekeleza hizi sheria. Kwa kuwa, sheria sisi ndio tunazitunga, Waheshimiwa Wabunge pamoja na Waziri, tuzirekebishe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, inakuwa ni hatari sana mtu labda hata amepotea njia tu akapita kwenye mapori yetu ambayo hayana sifa ya kuwa hata mapori anapigwa risasi. Vilevile ng’ombe, nikiangalia ng’ombe wanachukiwa sana kwenye hii Wizara kana kwamba, yaani sio pato lenyewe. Nikiangalia wengi humu tumeolea ng’ombe, hakuna mtu aliyeoa akatoa mahari ya tembo, kwa hiyo, niombe ng’ombe wathaminiwe sana, tutengeneze utaratibu mzuri kwenye hii sekta. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unajua katika utalii wasiangalie tu wazungu ndio watalii, hata ng’ombe nao ni watalii, tukipunguza fine, badala ya laki kila kichwa cha ng’ombe tukaweka elfu hamsini hamsini kila ng’ombe atakayekamatwa porini tutakuwa tumepata watalii. Mimi ukiniambia neno watalii kwanza silijui maana Ngorongoro sijawahi kufika. (Kicheko

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Waziri itakuwa ni vyema na Wabunge wengine maana wanaongelea tu hili suala la utalii, hawajafika kwenye pori lolote na wanajaribu kutoa mifano ya Indonesia ya uwongo mtupu. Kwa hiyo, ni vema… (Kicheko)

T A A R I F A

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kiruswa, Taarifa. Mheshimiwa Maganga kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kiruswa.

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumfahamisha mzungumzaji kwamba, kuna bidhaa ya utalii wa mseto ambapo kule ulaya wazungu wanasema go to Serengeti and Ngorongoro to see the lion and the Masai. Kumaanisha kwamba, unaweza kwenda Ngorongoro au Serengeti ukamwona Mmasai ambaye ni binadamu na mifugo na wanyama. Kwa hiyo, biashara ya utalii mseto inawezekana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Yaani unampa taarifa kwamba, Mbogwe pia, wanaweza wakakaa na wanyama porini, ndio unachojaribu kusema?

Nadhani hilo mmefanikiwa ninyi Wamasai, sina uhakika na wao kwa sababu, wao wanyamapori wanakula, ninyi kule kwenu Ngorongoro mmewaacha wanyama waendelee na maisha.

Mheshimiwa Nicodemas Maganga.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nilindie muda wangu nina vitu vya msingi hapa na vya maana sana. Naomba Mheshimiwa Waziri anisikilize vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya wananchi wa Mbogwe, Pori la Mkweni, lilishamaliza sifa ya kuwa pori maana halina tembo, halina wanyama wale wanaoangaliwa na watalii. Pori lile sasa hivi wamejaa Wachina, wanachimba usiku, lakini binadamu wakionekana mle wanavunjwa miguu pamoja na ng’ombe wakiingia mle wanatozwa laki.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile wapo vijana wa Mheshimiwa Waziri, ng’ombe wakiwa wanapita hata barabarani, maana pori lile limepakana na barabara ya lami, ile barabara kuu iendayo Kongo, wakionekana ng’ombe wanapita barabarani wanakamatwa wanaingizwa kwenye pori. Lengo na madhumuni kwa kuwa fine ni kubwa, ni laki moja, wanapata mwanya wa kupatia rushwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye sekta hii , nataka nimweleze ukweli Mheshimiwa Waziri, maana nampenda pamoja yuko na dada yangu, wakae wakijua kabisa watu wanateseka sana walio jirani na mapori. Kwa maana hiyo, ni vyema sasa hata wanapotengeneza huu mpango wa Operation Ondoa Mifugo Porini kwanza wajue kabisa kwamba, wana watu wa aina gani na kidogo Waziri ajaribu kuonesha makucha wasiwe wanawaonea tu watu wenye ng’ombe, maana sisi sote tumetoka huko kwenye ng’ombe, tunajua machungu ya ng’ombe hatujui thamani ya tembo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, mimi binafsi namchukia sana mtu anayechukia ng’ombe na kuthamini tembo. Maana tembo hawa tunategemea mpaka watu watoke Canada na sehemu nyingine ili tupate pesa za kigeni, lakini sisi wenyewe tukiwekeana utaratibu, tukawa tunachungia kwenye mapori yetu, kwa kuwa mapori yetu haya tuliyopewa na Mwenyezi Mungu ni makubwa, tukaweka fine hata ya shilingi 50,000, lakini vilevile kwenye Ilani ya Chama chetu Cha Mapinduzi kwenye ukurasa wa 52 tuliahidi kwamba, tutatenga kwenye mapori yetu maeneo ya kuchungia ng’ombe. Ni vyema na lenyewe hizi Wizara naziona zinafanana, ni kama kurwa na doto, sekta hii pamoja na sekta ya ardhi, wakakaa ili kusudi wakalitengeneza hili suala ili watu waweze kuishi vizuri kwenye mapori yao hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)