Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nichangie kwa ufupi hotuba ya Waziri wa Maliasili na Utalii. Nianze moja kwa moja kwa kutoa pongezi zangu kwa kazi nzuri ambayo inafanywa na Wizara. Kusema kweli Waziri, Mheshimiwa Dkt. Damas Ndumbaro; Naibu wake, Mheshimiwa Mary Masanja; Katibu Mkuu, Dkt. Allan Kijazi; Wakuu wa Taasisi zote ambazo ziko chini ya Wizara na Watendaji wote wa Wizara hii kwa kweli wanafanya kazi nzuri. Mnyonge mnyongeni lakini haki yake apewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na salam zangu za pongezi, nizungumzie tatizo la mipaka. Wabunge wenzangu wameshazungumzia jambo hili kwa kirefu na kwa undani zaidi, lakini nimkumbushe Mheshimiwa Waziri kwamba kule kwenye Jimbo langu Arumeru Mashariki kuna tatizo la mpaka kati ya Arusha National Park na Kitongoji cha Omela. Arusha National Park walichukua ekari takriban 960 mwaka 2017 na baadaye wakarudisha ekari 360. Baada ya kuchukua lile shamba waliwaacha wananchi wakiteseka hawana mahali pa kufanyia kilimo ambacho ndio ajira kubwa kwa wananchi wetu wa Tanzania. Kwa maana hiyo waliwaacha wananchi wakiwa maskini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Wizara kupitia Waziri, watumie busara kidogo waangalie ekari zilizobaki ekari 640 sio tatizo kubwa kwa Taifa hili na sio tatizo kwa hifadhi. Wapime faida ambayo hifadhi inapata na hasara ambazo wananchi wameingia katika kunyang’anywa yale mashamba. Ikiwezekana zile ekari zirudishwe kwa wananchi waweze kuendelea na maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niseme kidogo kuhusu Sekta ya Nyuki. Taifa hili tangu tumepata Uhuru, tumesomesha wataalam wengi sana kwenye sekta ya nyuki na kama tungetumia sekta hii vizuri, mazao ambayo yanatokana na nyuki yana uwezo wa kuingizia Taifa hili fedha nyingi tu hasa fedha za kigeni. Hata ile sumu ya nyuki ina soko sana nje ya nchi. Rai yangu kwa Wizara, iongeze nguvu kwenye sekta ya nyuki iweke kipaumbele ili hatimaye sekta hii nayo iweze kuchangia kwenye pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, wenzangu walizungumza kuhusu kuwekeza kwenye cable cars; ni kweli kabisa kwamba sisi Tanzania utalii tunaofanya kwenye milima ni utalii wa kupandisha watalii milimani kwa miguu. Tukubaliane kwamba kupanda mlima ni zoezi na jinsi watu wanavyozidi kuzeeka mazoezi yanakuwa ni tabu kidogo kuyafanya, huwezi kupanda mlima baada ya kufikisha miaka 80. Kwa hiyo, niseme kwamba Wizara iangalie, ifungue mlango kwa wawekezaji waweze kujenga miundombinu ya cable cars kwenye milima yetu hususan Mlima Kilimanjaro, Mlima Meru na kule Kitulo ambako mwenzangu, ndugu yangu Mheshimiwa Festo Sanga alisema kwamba miundombinu hiyo ikijengwa itaweza kutuingizia fedha nyingi sana za kigeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, niliwahi kutembelea nchi fulani, South Africa Cable mountains ni ngumu sana kupanda, lakini nilishuhudia jinsi ambavyo cable cars ambayo imejengwa pale inavyoingiza fedha nyingi kwa nchi ile. Nina uhakika kabisa kabisa kwamba…

T A A R I F A

MHE. CONSTANTINE J KANYASU: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kanyasu.

MHE. CONSTANTINE J KANYASU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nataka kumpa taarifa Mheshimiwa anayechangia kwamba Nchi ya Thailand inapata watalii milioni 16, lakini asilimia zaidi ya 80 ya watu wanaokwenda Thailand wanakwenda kwenye cable car na hawana milima mirefu kama Mlima Kilimanjaro. Wana milima ya kawaida tu ambayo wameiunganisha na cable car lakini ndiyo inayopeleka watalii wengi ambao ndio wanakwenda kutembea.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Dkt. Pallangyo unapokea taarifa hiyo?

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea kwa mikono 70. Ni kweli kwamba cable cars zina-supplement sana income kutokana na tourism. Ukiangalia fedha zinazoingia pale cable mountains utasema ni kwa nini hatufanyi hivyo na sisi. Niseme kwamba ninavyozungumza sasa hivi kuna ndugu yangu yupo Marekani alinidokeza kwamba ikiwezekana nirushe hiyo karata mezani kwako ili Wizara ilichukue halafu tuangalie namna gani tunaweza tukakaribisha wawekezaji waweze kuja kushirikiana na Taifa hili kujenga ile miundombinu kwa sababu pia nayo ile ni gharama, lakini ni njia mojawapo ambayo ingeweza kusaidia kutengeneza fedha nyingi sana za kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo machache, nakushukuru kwa muda ulionipa na naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)