Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nianze kwa kushukuru kwa nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii muhimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nianze tu kwa kuishauri Wizara hii juu ya migogoro kati ya wafugaji na wahifadhi. Wabunge wengi, hasa wa majimbo ya maeneo ambayo shughuli kuu ni ufugaji na wanapakana na hifadhi wamezungumza juu ya madhara mengi sana yanayotokana na migogoro hii kati ya wafugaji na wahifadhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina mambo mawili tu ya kushauri kwa Wizara hii. Kwanza naomba Wizara hii ifanye upya tathmini na upimaji wa hifadhi zao na waweke upya mipaka yao. Tuache kutumia mipaka ya zamani, kuna ramani tunaambiwa sijui mwaka themanini, mwaka wa ngapi, miaka kama ishirini, thelathini iliyopita. Tuache kutumia kutumia ramani hizi, tufanye upimaji mpya kwa sababu tayari kuna mabadiliko makubwa sana yamekwishafanyika kwenye ramani hizi na watu wamekwishaishi kwenye baadhi ya maeneo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna baadhi ya vijiji Wabunge wake humu ndani unakuta kijiji chote ni eneo la shoroba au eneo la hifadhi. Kwa hiyo tukitumia ramani za zamani maana yake hata kuna baadhi ya Wabunge humu wananchi wao wote wame-trespass. Kwa hiyo tufanye upimaji upya.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika upimaji huo basi kama ambavyo maeneo ya hifadhi yako landlocked na GN kwenye sheria zetu, basi na sisi maeneo ya vijiji, maeneo ya kulima na maeneo ya ufugaji yawe landlocked hivyo hivyo ili tuanze kuiwajibisha Wizara hii pale ambapo na wao wanyama wataingia kwetu na sisi tuwajibishwe pale ambapo wananchi wetu wataingia kwao. Kwa hiyo ulinzi wa kisheria uwe kwa pande zote mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na mzungumzaji aliyepita juu ya hili suala la usafirishaji wa viumbe hai kwenda nje. Nianze tu kwa kusema kwamba kama ilivyooneshwa kwenye wasilisho la Mheshimiwa Waziri, Wizara hii inachangia asilimia 21 ya GDP ya nchi hii. Kati ya asilimia hizi 21, asilimia 17.6 zinatokana na utalii peke yake na asilimia 80 ya suala hili la utalii kwa maana ya hii 17.6, inatokana na utalii wa wanyama. Maana yake ni kwamba watalii wengi wanakuja kwenye nchi yetu kwa sababu tuna wanyama mbalimbali ambao wangependa kuwaona, aidha, kwa sababu wa kwetu ni tofauti sana au hawapatikani kwenye sehemu nyingine ya dunia hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa sambamba na hayo, Wizara hii inachangia asilimia 25 ya fedha zote za kigeni zinazoingia katika nchi yetu, lakini vijana milioni 1.6 wameajiriwa katika sekta hii ya utalii ikiwa ni pamoja na madereva, tour guides, hotelini na sehemu mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni rai yangu kwamba hili ni suala la kizalendo; tukiruhusu wanyama wetu ambao wanapatikana kwa upekee kabisa kwenye nchi yetu, wakapelekwa katika nchi zingine, maana yake tunasema watalii hawatakuja tena kuangalia wanyama hawa, lakini pia hawatakuja tena kwa shughuli zozote za kiutafiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatutakuwa tu tumeathiri hii asilimia 17.6 ya pato letu la ndani, bali tutakuwa tumeathiri hizi ajira milioni moja na laki sita za vijana wa Kitanzania ambao wanategemea utalii kama shughuli kuu ya uchumi katika maisha yao. Pia tutakuwa tumeathiri biashara ya Shirika letu la Ndege la ATC ambalo tumetumia fedha nyingi sana kulifufua mpaka sasa. Vile vile, tutakuwa tumeathiri sekta binafsi ya hoteli, usafirishaji, yote haya yataathirika kwa kiasi kikubwa kama tukiruhusu usafirishaji wa wanyama kwenda nchi za nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano, hebu tutafakari, kama ingekuwa madini, kwa mfano gold, inaweza ikapandwa na ikaota kama mti, tunategemea wale watu wangeendelea kuja kuwekeza kwetu? Wangechukua wakaenda wakapanda wakaendelea na mambo yao. Sasa hivyohivyo wanyama leo hii tukiruhusu waende wakazalishwe kwingine maana yake species ambayo tungetaka wale watalii waje kuiona kwa upekee katika nchi yetu itapatikana sehemu zingine zote duniani. Hakutakuwa na haja ya mtu kufunga safari. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Haya, naona jirani anataka kumpa taarifa, Mheshimiwa Asia Halamga.

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba Kanda ya Kaskazini tunategemea sana utalii na kipindi hiki kifupi cha COVID-19 kimeathiri sana uchumi, hasa uchumi wa vijana wa Kanda ya Kaskazini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi zimeahidiwa ajira zaidi ya milioni nane za vijana zitakazotokana na masuala ya utalii na masuala mengine ili kuweza kufikia ajira milioni nane. Naamini kabisa tukiruhusu wanyama wakatoka nje ya nchi, hatuwezi kufikia kwa sababu nchi zingine hazitakuwa na sababu ya kuja katika nchi yetu ya Tanzania. Ahsante.

NAIBU SPIKA: Naona huo ulikuwa ni mchango wa Mheshimiwa Asia Halamga kwenye hii Wizara kuliko taarifa. Mheshimiwa Ng’wasi Kamani, malizia mchango wako.

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Niwakumbushe tu Waheshimiwa Wabunge kwamba Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, akiwa anazungumzia sekta ya madini wakati bado nchi yetu haijapata nafasi ya kutosha kuwekeza huko alisema kama bado hatujawa tayari kuwekeza na madini haya yakawafaidisha Watanzania, basi tuache uwekezaji huu ili uje uwafaidishe Watanzania pale ambapo tutakuwa tayari.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama bado Watanzania hatujawa tayari kutumia wanyama wetu vizuri ikatuletea tija, kuliko kukubali tuwasafirishe kwenda nje, tuwaache ili tutakapokuwa tayari wawafaidishe Watanzania wenyewe. Rai yangu tulinde ajira hizi za vijana ambazo zinakwenda kupotea, tulinde mapato haya ambayo tutayapoteza kama tukiruhusu suala hili likaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kumalizia, napenda tu kuchangia kwenye suala zima la misitu. Tunaishukuru sana Serikali yetu, imekuwa ikiweka mkazo sana kwenye upandaji wa miti, misitu ya Serikali na misitu ya watu binafsi. Hata hivyo, changamoto kubwa kwenye sekta hii ya misitu imekuwa ni uchomaji moto wa misitu. Wote tunakubali kwamba kumekuwa na uharibifu mkubwa sana wa mazingira ambao umesababisha mabadiliko ya tabianchi yanayotuathiri nchi na hata dunia kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna watu wamejitolea kwa rasilimali zao wenyewe kupanda misitu kwenye mikoa mbalimbali ya nchi hii ambayo inatusaidia. Kwanza inaisaidia Serikali kutunza mazingira; lakini pili, inasaidia sana katika suala zima la kuleta mvua na kusaidia kwenye kilimo ambacho zaidi ya asilimia 70 ya Watanzania tunakitegemea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye misitu ya Serikali nafahamu suala hili la moto ni changamoto, lakini wao wana watu ambao wanawasaidia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.

NAIBU SPIKA: Sasa naona umeishia neno wanasaidia, malizia sentensi yako.

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwenye misitu ya Serikali wao wana vijana wao ambao Serikali imewaweka kwa ajili ya kusaidia kulinda moto, kitu ambacho mtu binafsi hana rasilimali hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningeomba Wizara hii itafakari upya namna gani wawekezaji wanaowekeza kwenye misitu nao wanalindwa kwenye suala hili la moto, ikiwa ni pamoja sasa na Serikali kuona kama inaweza kusaidia kuweka walinzi hawa kwenye misitu ya watu binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)