Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia katika bajeti ya Wizara hii na Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, huwezi kuongelea maendeleo ya Wizara hii bila kutaja Kanda ya Kaskazini hususani Mkoa wa Arusha. Wameongea vizuri sana Wabunge wa Majimbo wa Mkoa wa Arusha, jana ameongea kaka yangu Mrisho Mashaka Gambo, ameongea vizuri kuhusiana na Wizara hii, umuhimu wa Wizara hii katika mkoa wetu. Vilevile baba yangu Mheshimiwa Dkt. Kiruswa, Mbunge wa Longido ameongea vizuri sana kuhusiana na umuhimu wa Wizara hii na mimi kama mwakilishi wa Mkoa wa Arusha, naomba nisisitize umuhimu wa Wizara hii katika Mkoa wetu wa Arusha (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba pia niwashauri Wizara hii ya Maliasili na Utalii waendelee kuwashirikisha wadau wakuu wa maendeleo wa Mkoa wa Arusha katika maendeleo ya Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda naomba niongelee suala moja tu la sintofahamu iliyoko katika Wilaya ya Longido kuhusiana na maamuzi ya Serikali kutenga maeneo yao kuwa Mapori ya Akiba. Naomba niikumbushe Wizara kwamba asilimia 95 ya wakazi wa Longido wanajihusisha na ufugaji na wanategemea sana mapori haya kwa ajili ya malisho ya mifugo yao. Maamuzi haya ya Wizara yataathiri Zaidi ya vijiji 19, vya Tarafa ya Ketumbeine na vijiji 11 vya Tarafa ya Engarenaibor na kijiji kimoja cha Tarafa ya Longido. Tukumbuke kwamba pia katika maeneo haya kuna wakazi zaidi ya 90,000 ambao wanategemea pori hili katika masuala yao mbalimbali ya kuishi na katika kuinua kipato cha uchumi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi hawa pia kwa juhudi zao binafsi wameendeleza miundombinu ya masuala ya kijamii kama afya, elimu na kadhalika. Kwa hiyo sidhani kwamba ni suala la busara kuwaondoa katika maeneo haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Rais wetu wa Awamu ya Tano yake alifanya jitihada kubwa sana kurudisha zaidi ya vijiji 900 kwa wananchi ili waweze kupata maeneo ya kuishi na kufanya shughuli zao mbalimbali za kiuchumi. Vile vile katika hotuba ya Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan, aliyoisoma tarehe 22 Aprili, hapa Bungeni alionyesha dhamira kubwa ya Serikali katika kuongeza maeneo ya wafugaji hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua hizi za Wizara hii ya Maliasili na Utalii, naona dhahiri zinakinzana na dhamira njema ya Serikali kwa wananchi wetu. Naiomba sana Serikali yangu sikivu kupitia Wizara hii, itumie busara katika jambo hili ili basi lisiweze kuleta madhara kwa wananchi wetu. Naomba pia wizara hii kabla ya kufanya maamuzi kama haya iweze kuwashirikisha wadau mbalimbali hususani wa maeneo yale ili waweze kutoa maoni yao juu ya mambo haya. Vile vile naomba sana Wizara kabla ya kufanya maamuzi haya iweze kutembelea maeneo haya ili ijue basi, kama kweli maeneo haya ni mapori ama ni makazi ya wanadamu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, naomba kutoa hoja. (Makofi)