Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami nianze kwa kumpongeza sana Rafiki yangu Waziri pamoja na Naibu wake; timu nzima ya Wizara pamoja na wadau wa utalii na maliasili kwa kazi kubwa wanayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia kwenye maeneo kama manne hivi. Kama muda hautaniruhusu, nitapeleka kwa maandishi. Nitachagia suala la Half Mile, wapigakura wangu wamenituma kule Moshi kwamba niombe kitu kuhusu Half Mile. Halafu nitatoa ombi la Wizara ikiwezekana wafungue route mpya za kupanda mlima Kilimanjaro kupitia Kata za Mpakani za Uru na za Old Moshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda tutambue uwepo wa mti mrefu kuliko yote Barani Afrika wenye mita 81.5; na huu ndiyo mti mzee kuliko miti yote duniani, uko Kilimanjaro kwenye Kijiji cha Tema kwenye Kata ya Mbokomu. Pia nitazungumzia mgogoro uliopo wa kwenye hifadhi ya Ngorongoro kama muda utaruhusu kwa sababu watu wameongezeka kama alivyosema Mheshimiwa Paresso na kuna tatizo kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa half mile. Half mile ni nini? Half mile ili ni eneo linalotenganisha Mlima Kilimanjaro eneo la hifadhi na makazi ya wananchi. Kwa hiyo, ni eneo lenye upana wa nusu maili ambalo linatengenisha watu na Mlima Kilimanjaro. Historia ya watu Kilimanjaro inaonesha kwamba tulianza kuishi pale karibia miaka 2,000 iliyopita. Kwa hiyo, tumekaa pale muda mrefu tu. Pamoja na kukaa huko kwa muda mrefu, lakini tuna experience mbaya sana watu wa Kilimanjaro kuhusiana na umiliki wa ardhi kule kwetu na hizi hifadhi za asili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi vitu tumevirithi, lakini niseme tu mwaka 1921 tulipata shida kidogo na Wakoloni, walipitisha sheria ya kusema kwamba watu wasiende kule Kilimanjaro kule mlimani, iliwekwa sheria kabisa kwamba mtu akienda kule ni kosa. Mwaka wa 22 Gavana aliyekuwa anatawala nchi yetu alisema ardhi yote ni yake; na mwaka 23 wakaanza program mbaya kabisa ya kuwanyang’anya watu ardhi yao na kujimilikisha na kuanza mashamba ya masetla. Mashamba hayo tuna bahati kwamba yalitaifishwa mwaka 1967 kupitia Azimio la Arusha, lakini bado hayajawa mikononi mwa wananchi moja kwa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla Wakoloni wametuletea matatizo makubwa sana kwa sheria kandamizi za umiliki wa ardhi pamoja na zile maliasili zetu. Pamoja na ukatili wa Wakoloni, niseme kwamba mwaka 1941 walianzisha kitu kinachoitwa half mail. Walituonea huruma wakasema ruksa sasa nusu maili wananchi mwingie mpate huduma za misitu kama kuni, mboga kama mnavu za kwenda kupika kitalolo, kuna chakula cha kienyeji kule nyumbani, mkajipatie mbao za kujenga na vitu vingine. Kwa hiyo, walituruhusu, walikuwa na huruma kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliendelea hivyo mpaka mwaka wa 2004. Matumizi yalikuwa mabaya kwenye hii half mail, Serikali yetu ya Tanzania ikasimamisha ule utaratibu ambao wakoloni walituonea huruma Serikali ikasema sasa basi kwa sababu mmeshaharibu sana; ni ukweli kulikuwa kuna uharibifu kwa sababu usimamizi haukuwa mzuri sana kwenye hii half mail, Serikali ikasimamisha, kwa hiyo, ikawa tena hakuna half mail na lile eneo likawa declared ni eneo la Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zuio hili la Serikali liliondoa ile huruma ya wakoloni ambao walituhurumia watu wa Kilimanjaro. Eneo hili sasa hivi linalindwa na maaskari wa KINAPA (Kilimanjaro National Park). Jamani, hawa watu ni wakorofi, wapiga kura wangu wameniambia kwamba wakati naomba kura watu wamepigwa, wameuawa na akina mama wamebakwa. Kwa hiyo, kuna mambo yanaendelea kule ambayo siyo mazuri sana. Wakati Makamu wa Rais, Mheshimiwa Dkt. Ali Mohammed Shein alipotembelea Kilimanjaro mwaka 2008 kwenye safari ya kikazi, wananchi walimweleza hii kero na alikuwa na Mheshimiwa Prof. Jumanne Maghembe kwenye hiyo ziara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Wizara ilikaa ikaelekeza TANAPA wachore ramani mpya. Kwa hiyo, Wizara ilipelekewa barua ambayo iliandikwa na Mheshimiwa Waziri Maghembe na Katibu Mkuu, Dkt. Ladislaus Komba kwamba wachore ramani ili eneo lirudishwe kwa wananchi. Bahati mbaya mpaka leo hakuna kitu ambacho kimeshafanyika na bado half mail strip hatujaipata. Kwa hiyo, tunamwomba Waziri achukulie pale walipoachia wenzake ili atusaidie. Hizi sheria ni kandamizi na zinafanya wananchi waichukie Serikali yao bila sababu. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa Muda wa Mzungumzaji)

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, chonde chonde, nakuomba ulibele hili na hii mtakapopeleka kwa Mheshimiwa Mama Samia tunamwomba sana alifanyie kazi mara moja, nasi tupate haki ya kumiliki na kutunza ule mlima ambao ni wa kwetu. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Prof. Ndakideni.

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Ahsante sana. Naomba kuunga mkono hoja.