Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji wa jioni hii. Awali ya yote, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na timu ya Wataalamu wote kwa jitihada kubwa ambazo wanazifanya za kuboresha utalii na kutunza Mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwenye eneo la Mbuga ya Katavi. Mkoa wa Katavi una Mbuga ya Katavi na jirani Mkoa wa Kigoma tuna Mbuga ya Gombe na Yamahale ambazo ziko Jirani. Eneo hili halijawekewa mazingira mazuri ya kutangaza utalii kwenye ukanda huu. Naomba sana Serikali iangalie ukanda wa Magharibi kwamba kuna vivutio vingi na vizuri ambavyo vinaweza vikashawishi watalii wakaja kwenye maeneo ya kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalo Ziwa Tanganyika; ni utalii ambao unaweza kabisa ukawavutia wawekezaji na watalii wakaja kuangalia madhali nzuri ya kule. Sasa karibu asilimia kubwa, utalii unaotangazwa ni wa upande mmoja tu wa mikoa ya Kaskazini. Naiomba sana Wizara ielekeze nguvu kama walivyokuwa wameagiza kwamba sasa watawekeza kwenye ukanda wa kusini na nyanda za juu, halikadhalika kwetu kule magharibi wapeleke nguvu kuutangaza utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie eneo la game reserve ya Lwafi. Game reserve ya Lwafi inapakana na msitu wa Nkamba Forest ambao unamilikiwa na Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika. Kwa bahati mbaya sana, Pori la Akiba la Lwafi linatoa leseni ya uwindaji; na karibu sehemu kubwa wanapoenda kuwinda wanaenda kwenye pori la msitu wa Nkamba. Sasa msitu huo tunaishia tu kuuhifadhi lakini hatuna manufaa ya aina yoyoye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri, pale ambapo wawindaji wanapotokea kwenye Pori la Lwafi, wanakuja msitu wa Nkamba Reserve, fedha zinazoitajika pale tuzipate kupitia Halmshauri ya Tanganyika. Ni eneo muhimu ambalo hatunufaiki nalo. Naamini wahusika watalifuatilia ili wajue ukweli ukoje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo hifadhi ya misitu inayomilikiwa na TFS ya Pori la Msaginya, Mpanda North East na Msitu wa Kabungu. Maeneo haya yalishapoteza sifa ya kuwa na uhifadhi kwenye hii misitu. Mheshimiwa Rais alipokuja akiambatana na timu ya Mawaziri, walitokea ufafanunzi kwenye maeneo haya ambayo hayana uendelezwaji. Msitu wa Msaginya umejaa wafugaji humo ndani, kuna miji ya watu, kwa hiyo, sifa ile haipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Msitu wa Mpanda North East kwanza kuna makazi ya Katumba ambayo yana watu wengi. Katika msitu huu, sifa iliyokuwa imewekwa katika kipindi hicho, haipo. Nilikuwa naomba mshungulikie ile migogoro ambapo tunacho Kijiji cha Ngomalusambo, Kijiji cha Vikonge, Kijiji cha Majalila na vijiji vinginevyo ambavyo viko kwenye Jimbo la Mheshimiwa Anna Lupembe muweze kuvishughulikia tutoe ile migogoro ambayo haipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya haya tutakuwa kwanza tumemuenzi Mheshimiwa Rais ambaye alitoa maelekezo na ninaamini Katibu Mkuu wa sasa ana kumbukumbu, pale tulipofanya ziara tukapitia kwenye Mbuga ya Hifadhi ya Katavi, tukaandaliwa chakula; karibu wanyama wa aina zote walipatikana pale. Kwa hiyo, naomba eneo hili mlishungulikie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao Msitu wa Tongwe Mashariki na Msitu wa Tongwe Magharibi ambapo tunapakana na eneo la Mbuga ya Mahale na pia tuna Msitu wa Nkamba. Misitu yote hii mitatu inamilikiwa na Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika na tumefaulu kuilinda vizuri, kwa sababu tunadhamini kile ambacho kinafanywa; na wananchi sasa hivi walishaanza kuelimika, wametunza ile misitu wakiamini inawasaidia. Tayari tumeanza kunufaika, tunavuna hewa ya ukaa na vijiji sasa hivi vinapata fedha kupitia utunzaji wa misitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Mheshimiwa Waziri, najua yupo Meneja wa Kanda ya Magharibi wa TFS. Huyu amekuwa akijihusisha kuhujumu misitu kwenye maeneo ya kwetu. Huyu Meneja anashirikiana na wavunaji haramu wa misitu na kuwanyanyasa wafugaji wa nyuki wapatao 12,000 ambao wamo kwenye ile misitu. Sasa naomba huyu mumshungulikie ipasavyo. Kinyume na hapo, mtaleta matatizo na watu watakaa bila kuwa na imani. Pia ameenda mbali sana, badala ya kulinda huo msitu, anafikiria kugawa vitalu vya wafugaji. Nashangaa sana kwamba bado mko naye mpaka sasa hivi. Naomba hili mkalishughulikie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa hii nafasi, naomba Serikali ishungulikie migogoro ya vijiji nilivyovitaja hapo. Ahsante. (Makofi)