Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi nami niweze kutoa maoni yangu. Pia namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya ili niweze kutoa maoni yangu katika Kamati ya Maliasili. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Wizara kwa ujumla kwa kazi nzuri wanazozifanya. Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wamekuwa wakitoa ushirikiano wa kutosha kwetu sisi Wabunge mara tunapofikwa na matatizo. Niendelee kuwaomba waendelee hivyo hivyo kutusaidia sisi Wabunge wenzao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na kuishukuru Serikali kwa kuipatia Wilaya ya Meatu shilingi milioni 51 kwa ajili ya kulipa fidia na kifuta machozi. Fedha hii imelipwa kwa wananchi 272 kati ya wananchi 520, lakini malipo haya yamefanyika kwa walioathirika kwa kipindi cha nyuma kwa mwaka 2017/2018 na 2018/2019, hivyo kuendelea kuwepo kwa madeni kwa wananchi walioathirika kwa 2019/2021. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, viwango hivi vimekuwa ni vya muda mrefu. Naomba kanuni ile ya mwaka 2011 ifanyiwe marekebisho ili viwango hivi viendane na hali halisi kwa kuwa haviridhishi wala haviakisi thamani ya uharibifu unaofanywa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, mimi nilipenda Serikali ijikite zaidi katika kuzuia uharibifu ambao unasababisha vifo na pia kuiingizia Serikali gharama kubwa. Tunavyoelekea, Serikali inaweza ikashindwa kumudu kulipa fidia na kifuta machozi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali kwa mikakati ambayo imekuwa ikiiweka. Imekuwa ikiandaa vijana kwa kuwapa mafunzo ya namna ya kukabiliana na wanyamapori wakali na waharibifu ambao pia wanasababisha vifo kwa wananchi, lakini mafunzo haya yamekuwa yakidumu kwa muda kidogo na baadaye yanashindwa kwa sababu wale tembo wamekuwa wakizoea zile mbinu na kuleta uthubutu kufanya uharibifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niungane na Kamati ya Maliasili kwa maoni yake kwamba ni vyema kuimarisha utendaji wa TAWA ili kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, ikiwemo masuala ya kibajeti. Naamini TAWA inao watumishi wa kutosha. Katika Pori la Akiba la Maswa hadi Januari 21, kulikuwa na watumishi 87. Watumishi hawa wanatosha; wakiwezeshwa kikamilifu wataweza kufanya doria zao kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe maoni yangu, TAWA wajikite zaidi katika ile miezi ambapo sasa wananchi wameanza kuivisha mazao yao kwa kuweka doria zaidi ili tuweze kuokoa yale mazao yasifanyiwe uharibifu, lakini hata kuzuia vifo. Katika Wilaya ya Meatu miaka miwili iliyopita wananchi 16 waliuawa na wananchi tisa waliuawa na tembo, lakini kama tukiweza kukabiliana vifo vitapungua na Serikali itapunguza gharama inayotokana na kulipa gharama za uharibifu huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna mwananchi anayependa kufanyiwa uharibifu ili alipwe fidia. Hakuna ndugu anayependa ndugu yake auawe ili eti alipwe shilingi milioni moja kwa ajili ya kufuta machozi. Tuwekeze zaidi katika kuzuia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mbinu nyingine nilitaka Serikali katika kukabiliana na wanyamapori wakali iwezekeze zaidi katika kutumia teknolojia kwa baadhi ya tembo, kuwawekea vifaa maalum vya kielektroniki kwa lengo la kufuatilia mienendo yao. Kazi hii imefanyika katika Pori la Akiba la Maswa katika Ranch ya Wanyamapori ya Makao; tembo 18 waliwekewa radio call. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili limeshindwa kuleta ufanisi kwa sababu, kwanza access ilitolewa kwa maafisa wanne akiwemo DGO wa Meatu na walifanikiwa kuwaona wale tembo wakitoka kwenye maeneo kuingia katika maeneo ya wananchi, lakini changamoto kubwa hata wakiwaona, hawana magari, hawana silaha. Ni kwa namna gani wataweza kwenda kukabiliana? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, maeneo manne yaliweza kubainika ambapo tembo wanaweza kutoka. Eneo la N’hanga lililopo Jimbo la Kisesa, Mwanyaina sehemu ya Landani, Sabha na Witamia.

Ombi langu kwa Serikali, kijengwe kituo Mwamongo katika Jimbo la Meatu kwa Askari wa Wanyamapori, kijengwe Kituo cha Askari katika eneo la Landani Mwanyaina katika Jimbo la Meatu. Tukifanya hivyo tutarahishia kuweza kuwarudisha wanapoonekana katika zile call walizowekewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru mwekezaji Mwiba, kupitia Frederick Conservation, walifadhili ule uwekezaji wa kuweka radio call. Nami naamini wako tayari kuendelea kuleta ufadhili huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuwawezesha TAWA naishauri Serikali ikubaliane na ile kanuni waliyoomba ibadilishwe katika kikao chao walichokifanya cha ujirani mwema TAWA na Maafisa Wanyamapori Meatu kwamba, asilimia 40 ya fedha inayotoka kwenye asilimia 25 ya uwindaji ipelekwe TAWA ili kuongeza nguvu zaidi. Kwa maana hiyo, wakiwa huko watanunua vifaa, watakuwa na magari kuliko urasimu unaofanywa na ofisi ya Mkurugenzi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa. Ahsante sana.

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naunga mkono hoja. (Makofi)