Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Kavejuru Eliadory Felix

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Kwanza nianze kumpongeza Waziri wa Nishati na Naibu wake na viongozi wote wanaoshirikiana kwa utumishi wao uliotukuka, Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nikushukuru wewe binafsi kwa kuniona lile la vinasaba kurudi kwenye TBS na Wabunge wote wakaamua litungiwe sheria. Hili ni jambo jema na la ukombozi kwa uchumi wa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa muda ni mchache, naomba niende moja kwa moja kwenye changamoto za umeme katika Mkoa wa Kigoma. Umeme ndiyo ufunguo wa maendeleo ya viwanda na ni uhai wa maendeleo ya jamii. Mkoa wetu mpaka sasa haujaungwa na Gridi ya Taifa na katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati amesema hapa kwamba ifikapo 2023, Mkoa wetu utakuwa umeungwa na Gridi ya Taifa na hilo limekuwa likizungumzwa kwa muda mrefu. Kuna vituo viwili vya kupozea umeme, Kituo cha Nguruka na Kidahwe. Nilikuwa nawasiliana mchana huu, je, ile site ambayo ilipendekezwa kijengwe kituo cha kupozea umeme kuna shughuli yoyote inayofanyika, jawabu ni kwamba hakuna chochote kinachoendelea na muda unaendelea kusonga mbele. Watu wa Kigoma tumekaa kwenye giza kwa muda mrefu, watu wa Kigoma wanaasili ya kufanya kazi sana, tuna mazao ya kimkakati ya michikichi ambapo mwaka kesho tunahitaji tuwe na viwanda, tunaomba tuungwe kwenye Gridi ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende kwenye Jimbo langu la Buhingwe, namshukuru Waziri na mkandarasi ambaye alitupa amesonga mbele, lakini naomba kasi iendelee kwa kuweka umeme kwenye Vijiji vya Janda, Murungu, Changwe, Kilelema na vingine vyote vilivyobaki ili na sisi pale pafunguke. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe ushauri ustawi wa Taifa lolote ule utategemea maendeleo yaliyopo lakini ukiwa unaongezwa na kukuzwa na tafiti. Nimshauri Waziri wa Nishati awekeze kwenye utafiti kwa kuwa kule Uganda pamekwishagunduliwa mafuta kwenye Ziwa Albert na wataalam wa miamba wanasema kwenye Ukanda wa Maziwa Makuu ambapo sisi Tanzania ni matajiri yawezekana tuna hazina kubwa ya mafuta na gesi basi utafiti uendelezwe na kuwepo mtaji wa kuweka kwenye tafiti ili tafiti ziendelee na tuendelee kubaini utajiri ambao Mwenyezi Mungu ametujalia.

Mheshimiwa Spika, kwa hayo machache, naunga mkono hoja kwa asilimia 100, ahsante. (Makofi)