Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba nianze kwa kufanya marekebisho ya jina langu mimi ni Hamida Mohamed Abdallah, ukisema Hamidu ni mwanaume na sio mwanamke. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, baada ya marekebisho hayo, nikushukuru kwa kunipa nafasi, lakini nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Kalemani, Waziri wa Nishati pamoja na timu yake ya Wizara kwa kazi ambayo wanaifanya na wamefanya kazi nzuri sana kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita. Bahati njema nilikuwa kwenye Kamati hiyo ya Nishati na Madini najua nini kilichokuwa kinaendelea katika utekelezaji wa masuala mazima ya maendeleo na kuleta mapinduzi makubwa ya umeme nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niipongeze sana Serikali kwa kutekeleza miradi mbalimbali ya kipaumbele, kama ambavyo taarifa imeelezea katika kasi ya kuongeza uzalishaji wa umeme lakini pia utekelezaji wa mradi mkubwa wa LNG ambao tunategemea tutakwenda kuutekeleza. Nipongeze sana ndugu zetu wa TANESCO kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya ya kuendelea kutupatia huduma ya umeme katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, bahati mbaya sana katika maeneo yetu ya Lindi Manispaa hatukuguswa na mradi wa REA. Kwa hiyo, bado tuna changamoto kubwa katika maeneo mbalimbali kutofikiwa na umeme. Ndugu zetu wa TANESCO hawana uwezo mkubwa wa kuweka miundombinu katika maeneo yote ya Mji wetu wa Lindi Manispaa, kwa hiyo, bado tuna changamoto.

Mheshimiwa Spika, tunajua tuko kwenye mpango wa Mradi wa Peri-Urban, lakini kwa namna ambavyo mradi huu unatekelezwa unaenda taratibu mno na sisi tuna hamu kubwa ya maeneo yetu yote kufikiwa na umeme kwa sababu tunajua kwamba uwekezaji wowote unahitaji uwepo wa umeme. Kwa hiyo, naiomba Serikali kuhakikisha kwamba Mradi huu wa Peri-Urban kwa namna yoyote unakwenda kwa kasi kubwa na sisi wana Lindi tunahitaji kupata mradi huu.

Mheshimiwa Spika, sisi Lindi Manispaa tuna Majimbo mawili na Majimbo haya yana changamoto kubwa kwa sababu tuna maeneo ya pembezoni mwa mji na maeneo hayo sasa kuna uwekezaji mkubwa wa kilimo. Pia tunajua kwamba sasa wananchi wanakwenda kuwekeza katika kilimo cha umwagiliaji ambacho kinahitaji uwepo wa umeme. Kwa hiyo, naiomba Serikali kuhakikisha kwamba mradi wa Peri-Urban unaharakishwa ili sisi wananchi wa Lindi tuweze kufaidika na mradi huu ambao utakuwa na gharama nafuu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado ndugu zetu wa TANESCO wamekuwa na changamoto kubwa sana kwa sababu wananchi wanahitaji umeme lakini gharama za ulipaji wa umeme wa TANESCO ni shilingi 300,000. Hizi ni gharama kubwa sana mwananchi wa kawaida hawezi kumudu kulipa shilingi 300,000 ili apate umeme, kwa hiyo, kuna changamoto hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini wanasema hawawezi kutekeleza kwa kulipa shilingi 27,000 kwa sababu hawana waraka wowote kutoka kwa Mheshimiwa Waziri. Mheshimiwa Dkt. Kalemani nilikuwa na wewe kipindi kirefu na kila unapokwenda kwenye eneo la mkutano ulikutana na hoja hii na uliweka wazi kwamba kila mwananchi atapata umeme kwa gharama ya shilingi 27,000 bila kulipia nguzo. Hata hivyo, suala hili bado linaendelea na wananchi wetu wanashindwa kumudu kuweka umeme.

Mheshimiwa Spika, pia TANESCO wana changamoto ya nguzo kwa sababu wananchi wengi sana wamelipia ili waweze kufungiwa umeme pale Lindi Mjini lakini TANESCO hawana nguzo hivyo wananchi wanashindwa kupata umeme. Hili ni suala la kushangaza watu wako katikati ya mji wanakosaje umeme?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, suala la kutokuwepo kwa nguzo ni changamoto kubwa, tunaomba Serikali isimamie suala hili kuhakikisha kwamba changamoto hii inaondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunao mradi wa matumizi ya gesi majumbani pamoja na magari. Bahati njema sana mwaka uliopita tumezindua mradi huu katika Kata ya Mnazi Mmoja eneo la Lindi Mjini. Tumefarijika sana na wananchi wana hamu kubwa ya kuona umeme huu sasa wanaendelea kufungiwa.

Mheshimiwa Spika, Serikali ilitoa offer kwa wananchi wa Lindi nyumba 300 kufungiwa umeme kupitia mradi huu wa matumizi ya gesi majumbani. Hata hivyo, tangia mradi huu umezinduliwa mpaka leo hakuna chochote kinachoendelea. Tunahitaji Mheshimiwa Dkt. Kalemani utuambie ni lini sasa mradi huu unakwenda kutekelezwa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante.

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nikushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)