Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona niweze kuchangia kidogo kwenye Wizara hii ya Nishati ambayo kimsingi ni Wizara ya kazi, kimkakati na maendeleo na bajeti nzima percent 98 ni maendeleo tu.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu wake, Katibu Mkuu na watendaji wote kwenye Wizara kwa kazi nzuri ambayo wanafanya pamoja na taasisi ambazo ziko chini ya Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli ukiangalia jinsi ambavyo mambo yanakwenda sasa hivi kuhusu hii bidhaa ya umeme nchini utaona kwamba kuna tofauti kubwa sana. Kabla ya mwaka 2015 ukitaka kupata umeme ilikuwa ni kizungumkuti lakini siku hizi ukitaka umeme unafungiwa na unaelewa ufuate hatua gani ili uweze kupata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeza sana Waziri, naungana na ndugu yangu Mheshimiwa Elibariki kwa kweli Waziri Kalemani na Manaibu wake ni watu wastaarabu, wapole, unazungumza nao na wanaonyesha kabisa wana kiu ya kufikia malengo yao. Hongera sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia pia mafanikio kwenye Bwawa la Nyerere, nilikwenda kule mwaka juzi mwishoni nikiwa chini ya Wizara ya Maliasili na Kamati yetu kazi ambayo ilikuwa imefanyika ni kidogo sana. Sasa hivi bwawa limetengenezwa kwa kiwango cha percent 52, ni kazi kubwa napongeza sana Wizara.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda, naomba sasa nizungumzie kidogo habari ya jimbo langu kuhusu umeme wa REA. Kuna mafanikio makubwa sana over all ni percent 86 lakini ukija kwenye jimbo langu zipo percent 43 tu za kazi iliyofanyika. Kwa faida ya Wizara na Waziri naomba nitaje vijiji ambavyo viko gizani, jimbo upande wa Mashariki na Kusini liko gizani; Kata ya Kingori, Vijiji vya Muungano, Oldonyongilo, Ngonoheri, Mboleni, Ngosio, Nsengoni viko gizani. Kata ya Malula; Vijiji vya Kolila, Ndumangeni, Malula, Ngajisosia, viko gizani. Kata ya Maruwango; Vijiji vya Mowaro, Maruwango yenyewe, Mbasenyi, Nombele, Songambele viko gizani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kata nyingine ni Kata ya Ngarinanyuki iko gizani kabisa, Olukung’wado pale mjini wana umeme kidogo sana. Kata ya Uwilo; Kijiji cha Kimosonu wako gizani, Ngwandua Kijiji cha Nkoavele wako gizani. Kata ya Songolo; Vijiji vya Ulisho, Songoro, Malula, Kilinga wako gizani. Kata ya Kikatiti; Sakila Juu, Sakila Chini, Njeku, Nashori Kikatiti wako gizani. Kata ya Maroroni; Migadini, Kwaugoro, Samaria wako gizani. Kata ya Ngwalusambu; Kijiji cha Mfuloni, Ngwalusambu yenyewe, Kimundo wako gizani. Kata ya Maji ya Chai; Vijiji vya Maji ya Chai, Kitefu, Lerai, Ngurudoto wapo gizani. Kata ya Mbuguni; Kambi ya Tanga, Kikileto, Migungani wako gizani. Kata ya Shabarahi; Bulka na Karangai wako gizani. Kata ya Kwikwe; Luwainyi na Malala wako gizani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kifupi pamoja na kwamba over all kazi iliyofanyika ni nzuri lakini kwa kweli jimboni kwangu hali si nzuri. Hivi vijiji viko karibu karibu kama Wizara ingejipanga vizuri ile kazi isingekuwa ngumu sana. Nadhani kuliwa kuna tatizo kidogo wakati wa kuanza kazi hii nakumbuka walileta nguzo sehemu zingine wakachimba mashimo wakayaacha wazi, wakaacha nguzo zikaendelea kuoza pale, kuna hadithi nyingi ambazo kwa kweli hazifurahishi.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni kuhusu hii bei ya kuunganisha umeme wa REA Sh.27,000, bado ni kizungumkuti. Kuna watu ambao walikwenda wakajaza fomu wakitegemea kwamba wanaunganishiwa kwa Mpango wa REA wakapelekewa bili kubwa badala ya Sh.27,000 anapelekewa bili ya Sh.337,000, kiwango ambacho kimekuwa kigumu sana kwa wao kuweza kufungiwa umeme.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, naskuhukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja. (Makofi)