Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante, nami niunge mkono hoja kwa asilimia 100.

Mheshimiwa Spika, nitachangia eneo la Mradi wa Umeme Vijijini (REA). Katika jimbo langu utekelezaji wa mradi huu hauendi vizuri. Nimekwenda mara kadhaa kwa Mheshimiwa Waziri, nimemuomba afanye ziara aje ashuhudie kinachoendelea. Bahati nzuri aliniahidi mwezi wa pili tungeenda naye lakini bahati mbaya mambo yaliingiliana hakufanikisha. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri afanye ziara hiyo kwa sababu haiwezekani hapa kila Mbunge anayesimama anampongeza ameenda mara mbili, tatu au nne kwenye jimbo au wilaya yake, sasa mimi nashindwa kusema. Kwa hiyo, naomba na mimi nataka nije hapa kusema alikuja jana, juzi na siku nyingine.

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa ni vijiji 34 tu ndivyo vilivyofungiwa umeme kati ya vijiji 117, kata 16 zote hazina umeme ziko gizani. Hata hivyo vijiji 34 ni kituko, utakuta kijiji kimoja ni nyumba sita tu ndiyo zimeingiziwa umeme. Sasa hivi kuna wananchi 2,100 waliomba kufungiwa umeme katika nyumba zao, wameshafanya kila kitu na wamelipia mita, ni zaidi ya miaka mitatu baadhi ya wananchi hawa hawajafungiwa umeme. Navyomuomba twende akashuhudie tafadhali afanye hivyo.

Mheshimiwa Spika, wiki iliyopita Baraza la Madiwani limekaa kikao na lilitoa maazimio. Azimio mojawapo ni la kunitaka mimi nishike shilingi mpaka Waziri aende kule akawaambie ni lini watafungiwa umeme hawa wananchi 2,100 ambao zaidi ya miaka miwili, mitatu wamelipia umeme lakini hawafungiwi; mita hazipo, vifaa fulani havipo, sasa tunafanyaje?

Mheshimiwa Spika, siyo hivyo tu kuna Kata tatu za Matili, Mkumbi na Litembo tulisema miradi ingekamilika Desemba lakini haikukamilika. Miradi hii mingine ni ndani ya miaka mitano ya kipindi kilichopita leo zinakuja nguzo, kesho wanaleta nyaya, keshokutwa wanachimba mashimo mpaka leo miradi hii wananchi hawajaona umeme. Kwa hiyo, ni kero kubwa sana mpaka wanasema hivi sisi tunachagua CCM kwa nia ipi? Wanakuwa na mawazo mengine, sasa si vizuri Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni ukatikaji wa umeme, Wilayani Mbinga umeme unakatika sana yaani usipokatika chini ya mara 15 siku hiyo kuna umeme, ni mara
20 mara 40 na kuendelea. Hali hii imesababisha wafanyabiashara kupoteza mali zao na mitaji yao na sasa hivi wengi hawafanyi biashara, shida ni nini Mheshimiwa Waziri?

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri sisi pale tuna vyanzo vya umeme pale pale; kuna watu binafsi wanazalisha umeme wa kutosha lakini unaenda kwenye Gridi ya Taifa hapa Mbinga kilometa 2 tu hamna umeme. Kuna mwingine anazalisha mjini pale lakini hamna umeme. Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kutoa majumuisho hapa atuahidi anakuja lini lakini hizi kata ambazo zina mradi sasa hivi umekaa miaka mitano hauishi lini tunaenda kuwasha umeme? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa na mengi lakini naona muda huu hautoshi, niseme tu naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)