Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Nishati.

Mheshimiwa Spika, nami niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Kalemani na Naibu wake, Mheshimiwa Stephen Byabato. Bahati nzuri Waheshimiwa Madiwani kutoka Ludewa walikuja, Mheshimiwa Kalemani aliwapokea, alizungumza nao, alisikiliza changamoto za Ludewa, kwa hiyo, nampongeza na namshukuru sana. Halikadhalika Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Byabato, naye nampongeza anatupa heshima sana wanafunzi tuliomaliza Chuo Kikuu cha Tumaini pale Iringa. Hongera sana Mheshimiwa Naibu Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niipongeze sana Serikali kwa bajeti nzuri ya Wizara ya Nishati kwa sababu umeme siyo anasa ni maendeleo. Nadhani kila mtu anaelewa, kwa hiyo, ni vema sana kuhakikisha kwamba hii mipango ambayo inatekelezwa inapewa fedha za kutosha ili wananchi waweze kupata umeme wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, halikadhalika niishukuru sana Serikali tulipata mkandarasi, kule Jimboni kwangu Ludewa kuna kata zile za mwambao ambazo zina mazingira yenye changamoto sana kutokana na uwepo wa Ziwa Nyasa na milima mikali sana. Hata hivyo, nashukuru kwenye Kata za Lupingu, Lifuma na Makonde tayari mkandarasi ameshapeleka nguzo za umeme, kwa hiyo, wananchi wanamuomba tu aongeze kasi zile nguzo wameziona vya kutosha sasa wanatamani kuona umeme. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba utusaidie hapo. Halikadhalika tumempata mkandarasi mwingine kwa ajili ya kata zilizosalia; Kata za Ibumi, Lumbila na Kilondo, tunashukuru sana Serikali kwa hilo.

Mheshimiwa Spika, sambamba na pongezi naomba Mheshimiwa Waziri afahamu kwamba kuna kata tano za kule Ludewa zina changamoto sana ya umeme; Kata hizo ni Milo na Mawengi. Kata hizi mbili zina mradi ambao ulikuwa unasimamiwa na mzalishaji binafsi ambaye alikuwa chini ya Kanisa Katoliki. Tumshukuru sana Baba Askofu Alfred Maruma huko aliko apumzike kwa amani, alitusaidia sana kupata umeme kwenye Kata za Milo na Mawengi kabla maeneo mengi nchini hayajapata umeme. Kwa bahati mbaya ule umeme sasa hivi unasumbua sana. Kwa hiyo, naomba Serikali iingilie kati ili wananchi wa Kata za Milo na Mawengi waweze kupata umeme wa uhakika kwa sababu kata hizi mbili zina wakazi wasiopungua 21,000, hospitali kubwa ya Milo ambayo iko chini ya Kanisa la Anglican, shule za sekondari na zahanati ambazo zinahitaji umeme.

Mheshimiwa Spika, pia kuna umeme ule wa Lugarawa ambao unahudumia vijiji 20 kwenye Kata za Lupanga, Madilu, Lugarawa, Mlangali, Lubonde na Madope. Nako huku kuna wakazi wasiopungua 51,000 na umeme huu pia ulikuwa chini ya mzalishaji binafsi unakuwa wa mgao zaidi ya saa 12 vilevile mzalishaji anashindwa kuuza umeme kwa maelekezo ya Serikali kwa sababu gharama zake za uzalishaji ziko juu. Kwa hiyo, wananchi 51,000 katika vijiji 20 kupata umeme wa mgao wa saa zaidi ya 12 na wakati mwingine mitambo ile inazima kwa muda mrefu inakuwa siyo sawa. Mheshimiwa Waziri niombe kwanza tuwashukuru wale wazalishaji binafsi kwa sababu walitusaidia sana lakini Serikali iweze kuingilia kati kwa sababu tayari TANESCO wameshaingia mkataba mdogo kununua umeme kwa kampuni ile ya Madope basi inunue umeme wote ili shughuli ya kusambaza na changamoto nyingine ziweze kufanywa na Serikali. Wananchi hawa wa vijiji 20 ndiyo waliokichagua Chama cha Mapinduzi, kwenye kata hizi zote wamechagua madiwani wa Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)