Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii kuweza kuchangia mada hii iliyoko Mezani.

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kuipongeza Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi kwa utekelezaji wa miradi ya REA nchi nzima. kwa ujumla Serikali imefanya kazi kubwa kuanzia Serikali ya Awamu ya Tano na hii ya sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Waziri Kalemani na timu yake bila kinyongo kwa moyo mweupe maana kati ya miaka hii mitano iliyopita na kipindi hiki tulichoanza wamejitahidi sana kwenye miradi hii ya REA. Mimi niseme tu kwamba Waziri amejitahidi sana, ameenda kwenye Jimbo langu karibu mara tatu, nampongeza na kumshukuru na Mungu aendelee kumbariki. Mchango wake ulikuwa mkubwa kwa mimi kurudi hapa Bungeni kutokana na hii miradi aliyotekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sasa nichangie kidogo kwenye Wizara hii. Kwanza mradi huu unaokuja tunauomba uanze na kata ambazo zimerukwa. Kuna kata ambazo aliahidi kule kwangu akiwa Naibu Waziri na baadaye Waziri; Kata za Murai, Silaloda, Masieda na Nasei.

Mheshimiwa Spika, eneo hili limetusumbua kwa sababu ya jiografia na umbali kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wakandarasi mliowateua, niwapongeze wale waliowasiliana na Wabunge wao lakini nimewasiliana na Wabunge wa Mkoa wa Manyara kwa kweli, mkandarasi wetu hadi sasa hajaweza kuonesha utayari wa kuwasiliana na sisi ili tujue mipango yake anayokwenda kutekeleza ikoje. Hii itasaidia sana ikiwa Madiwani, Waheshimiwa Wabunge watafahamu jinsi ambavyo miradi hii itakavyotekelezwa ili baadaye tuwe kitu kimoja na hata tunapokwenda kwa wananchi tuwe na kauli ya pamoja tukijua utekelezaji wa mradi utaendaje.

Mheshimiwa Spika, nirudi kwenye utekelezaji pia wa Mradi wa Ujazilizi. Nina kata 17 ambapo saba ziko mjini na 10 ziko vijijini, lakini watu wa REA wanasema wewe wa mji huduma yako ni TANESCO na TANESCO hata miaka 10 hawataweza kupeleka umeme kwenye kata hizo kwa sababu, mbili hazikupelekewa umeme moja kwa moja Kata ya Silaloda, lakini pia na Kata ya Ilboru kwa kiasi kikubwa sana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba kama itawezekana, kata zile zilizoko pembezoni kwenye eneo la mji wangu au eneo la Mji wa Mbulu ziingie kwenye REA kwa sababu bado hazijafikiwa. Kama nilivyokudokeza Mheshimiwa Waziri, wewe ni msikivu na pia unatusikiliza sana huku Bungeni, lakini tuna hofu kidogo na utekelezaji wa ahadi zako unazotoa. Ukiwaagiza wao hawana majawabu na pia hawatekelezi kwa wakati, utakumbuka mwaka 2019 tulikwenda Mbulu, tulifanya ziara, ukaagiza umeme uende Gunyoda na Murai, lakini mpaka leo bado. Sasa kupitia hii REA inayoanza waanze na kata hizo ili wananchi wale waone ahadi ya Waziri ni ahadi ya Serikali na hiyo ahadi ya Serikali iweze kutoa matokeo chanya.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba kama kuna maeneo ya namna hii, kwa mfano kwenye Jimbo la Mbulu Mji kuna vijiji toka 2009/2010 wamepelekewa umeme kwa kaya kama 20 mpaka 50, kaya nyingine bado zinasubiri kwenye maeneo ya vijijini. Najua timu ya Wizara ilipita wakati ule ikatambua maeneo ambayo umeme haujapelekwa na ramani ilishachorwa basi waanze kwenye hivyo vijiji ambavyo vinahitaji ujazilizi kwa ajili ya kufanikisha jambo hili.

Mheshimiwa Spika, udhibiti wa magenge na kuchukua fedha za wananchi. Kumekuwa na tatizo kubwa wananchi wanahitaji umeme, wanaambiwa umeme utakuja, baadaye wanaambiwa hampo kwenye orodha. Kwa hiyo, kuna uchukuaji rejareja wa fedha kwa wananchi Sh.50,000, Sh.100,000, mianya ambayo sio mizuri sana kwa taswira ya Serikali yetu. Nashauri kama itawezekana watu hawa wadhibitiwe na TANESCO na mamlaka zilizoko na pia wananchi wahojiwe kwa nini nguzo tatu zilipelekwa kwa fulani ambaye yuko kijiji fulani badala ya ule mradi unaoendelea.

Mheshimiwa Spika, jambo hili ni la muhimu sana na kwa namna ya pekee nashauri kama itawezekana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Zacharia Issaay.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Naunga mkono hoja kwa asilimia 100, tuko pamoja. (Makofi)