Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kunipa nafasi ya kuchangia lakini pia, nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, ambaye ananipa afya na nguvu kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayoifanya pamoja na wasaidizi wake, lakini kipekee nimtaje Mkurugenzi wa REA, huyu mtu amekuwa ni mtu wa pekee, ukimtafuta wakati wowote anapatikana na ni mtu ambaye kwa kweli ni msikivu, nimpongeze sana na aendelee hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, umeme ni ajira, umeme ni viwanda, umeme ni uchumi, umeme ni maendeleo. Niongelee umeme kwa upande wa Mkoa wa Kagera, kwa kweli pamoja na juhudi za Serikali, Mkoa wa Kagera tumekuwa tukipata taabu sana tuna umeme ambao hauna uhakika. Kwa siku moja unaweza ukakatika zaidi hata ya mara 20, lakini pia umeme huu umekuwa ni umeme ambao nguvu yake ni kidogo. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali Mheshimiwa Waziri unafanya kazi nzuri mpambane iwezekanavyo, ili Mkoa wa Kagera uweze kuunganishwa kwenye gridi ya Taifa. Kwa sababu, umeme tunaoutumia sasa hivi, ni umeme ambao unatoka katika nchi Jirani na hatuna uhakika nao kwa sababu, sio wa kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niombe sana Mheshimiwa Waziri hili upambane nalo, ili Mkoa wa Kagera na sisi tuwe na umeme wa uhakika na ninaamini, hiki kinaweza kikawa kinachangia kwa Mkoa wa Kagera kuwa miongoni mwa mikoa ambayo ni masikini. Na ukija kuangalia mikoa yote kama Kigoma, Kagera na mikoa mingine ambayo iko kwenye orodha ya mikoa masikini, ni mikoa ambayo haina umeme wa uhakika. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri hili ulifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikija kwa upande wa Kyerwa Mheshimiwa Waziri, nikushukuru tumekaa mara nyingi, ninakuomba sana kwa ajili ya vijiji vyangu ambavyo havijafikiwa. Nina vijiji 99, vijiji 29 bado havijapatiwa umeme. Lakini tumekaa tumezungumza muda mrefu umenipatia vijiji 19 bado vijiji 10 havijapatiwa umeme na nikuombe sana kwenye kata hizi ambazo zilikuwa hazijapatiwa umeme, yaani umeme haujawahi kugusa kabisa. Kwa mfano, ukienda kwenye Kata ya Bugala kuna Kijiji cha Bugala, Mugaba kwenye Kata ya Businde kuna Businde, Nyakashenyi, kwenye Kata ya Kibale kuna Kibale, Kijumbura, Kigorogoro, kwenye Kata ya Rukuraijo kuna Kijiji cha Mkombozi pamoja na Mgorogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia, Kata ya Bugomora kuna Kijiji cha Nyakatera, vijiji hivi havijawekwa kwenye orodha ya kupatiwa umeme. Kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri hili ulipe kipaumbele, hawa watu wanahitaji umeme muda mrefu na nilitegemea mkandarasi anapoenda anapeleka umeme maeneo yote. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri vijiji hivi ambavyo nimevitaja, viweze kupatiwa umeme, nakuomba sana Mheshimiwa Waziri. Lakini jambo lingine mimi nina vitongoji 670, vitongoji 503 bado havijapata umeme, kwa hiyo, unaposema mmepeleka umeme kwenye vijiji bado vitongoji vingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa Kyerwa naweza nikasema umeme haujafika hata asilimia 30 kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri hili uliangalie. Mnasema mmepeleka umeme kwenye vijiji vingi, lakini vitongoji vingi havijafikiwa. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri hivi vitongoji 503 kati ya vitongoji 607, niombe sana vipelekewe umeme. Na umeme wa kwanza ulipokuja ile REA ya kwanza walipitisha nguzo juu, lakini vitongoji vyote ambavyo viko chini pale havikuweza kupatiwa umeme.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine Mheshimiwa Waziri, ulitoa maelekezo ukasema TANESCO wapeleke umeme kwenye taasisi za dini, kwenye mashule, kwenye vituo vya afya, maeneo mengi hayajafikiwa kwa upande wa Kyerwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri hili na lenyewe uliangalie. Jambo lingine ni suala la wananchi kuuziwa nguzo. Hili bado lipo Mheshimiwa Waziri na ikiwezekana niombe utoe maelekezo kwa maandishi, kila Mbunge awe na hii barua tuipeleke kwa wananchi. Kwa sababu, wanapopima wanakuambia mwananchi uko nje ya ramani ambayo tumepewa. Kwa hiyo, wewe unatakiwa ulipie nguzo tatu au nne. Kwa hiyo, niombe Mheshimiwa Waziri hili uliangalie.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, pale Kyerwa kwenye Kata ya Mulongo mpakani na Uganda, kuna mradi wa Kikagati, ule mradi Mheshimiwa Waziri sisi kama wana Kyerwa au wana Kagera, hatuelewi nini kinaendelea! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu, unaona upande wa pili ndio wanashughulika, lakini sisi hata ukienda pale kupata taarifa, haupewi taarifa inayohusiana na ule mradi. Kwa hiyo, tunaomba Mheshimiwa Waziri tujue sisi kama Kagera kwasababu, ule mradi ni wa Uganda pamoja na Tanzania. Tujue sisi kama Kagera tunapata nini? Lakini mradi huu unakamilika lini Mheshimiwa Waziri?

Mheshimiwa Spika, ninaamini mradi huu utakapokamilika ndio unaweza kuwa mkombozi, wakati Mkoa wa Kagera bado hatujaunganishwa kwenye gridi ya Taifa. Mradi huu unaweza ukasaidia angalau kutupunguzia yale makali tunayoyapata kwenye kukatika umeme kila mara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nimpongeze Waziri na nisemee mradi wa Julius Mwalimu Nyerere. Mradi huu ni mradi ambao kwa kweli Mheshimiwa Waziri, Serikali yetu itapata heshima kubwa, lakini pia wewe mwenyewe Mheshimiwa Waziri, ninaamini mradi huu umeuanzisha wewe na mradi huu utakupa heshima kubwa na jina lako litakumbukwa milele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, ninakushukuru ahsante naunga mkono hoja. (Makofi)