Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Agnes Elias Hokororo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, ahsante nakushukuru kwa kunipa nafasi, kwanza awali ya yote niipongeze Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Rais wetu mpendwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri inayoendelea kuifanya na hasa kuwaunganisha watanzania wote wa mjini na vijijini kwenye mtandao wa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali kwa sababu imetambua kwamba umeme ni suala la msingi na wala si la luxury na kwa msingi huo inaendeleza ujenzi wa mradi wa umeme ambao unajulikana kwa jina la Mwalimu Nyerere ambao utazalisha megawatts nyingi na kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wamesema mradi huo utatusaidia kwa kiasi kikubwa kuondokana na giza.

Mheshimiwa Spika, lakini Serikali pia inaendeleza mradi wa REA kwa sasa ni mradi wa REA awamu ya tatu mzunguko wa pili ambapo na hiyo inafanyika kwa nia njema ya kuwaunganisha wananchi vijijini wao waweze pia kupata umeme. Natambua juhudi zinazofanywa na Serikali ya Chama Cha Mapinduzi, lakini naomba tu nichangie kwa uchache sana katika Mkoa wa Mtwara ambapo ninawawakilisha wanawake wa Mkoa wa Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwamba katika Mkoa wa Mtwara bado tunavyo vijiji 281 ambavyo havina umeme, lakini natambua pia kwamba ipo jitihada Mheshimiwa Waziri anaifanya ya kuwapelekea vijiji hivi 281 umeme wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa pili, lakini ningeomba tu kwamba kwakuwa vijiji hivi ni vingi pengine wakandarasi wawili wasingetosha na ili pia mradi utekelezeke kwa haraka. Pengine wakandarasi wangeongezeka wangekuwa watatu kama ambavyo tuliahidiwa huko nyuma pengine vijiji hivi 281 vingefikiwa kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, niishukuru sana Serikali, huko nyuma kabla ya mwezi wa 3 Mkoa wa Mtwara ulikuwa na tatizo kubwa la kukatikakatika kwa umeme kwenye wilaya zote sita. Lakini Serikali ilituletea mashine mbili za kuchakata umeme, kila mojawapo ilikuwa na uwezo wa kuchakata megawati 4.3. Ninaishukuru sana Serikali kwa sababu, sasa kwenye wilaya nne umeme umekaa vizuri hauna tatizo kubwa la kukatikakatika. Changamoto imebaki katika Wilaya za Masasi na Nanyumbu, huku kuna tatizo kubwa la kukatika kwa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe ushauri kwa Serikali na kwa kuwa natambua ni Serikali sikivu. Kwa upande wa Masasi, ambako kumekuwa na tatizo kubwa la kukatika kwa umeme kwa sababu tu, umeme wake unaunganishwa kutoka Mkoa wa Ruvuma kule Madaba. Unatoka Madaba unapita Songea, unapita Namtumbo, unapita Tunduru, unakuja Mangaka ndio unakuja Masasi. Lakini pia, kuna njia nyingine inayotoka Mahumbika ambayo iko Mkoa wa Lindi. Kwa hiyo, hizo zote mbili haziwapatii wananchi wa Masasi umeme wa uhakika na hivyo wameendelea kuukosa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashauri, ili kuondoa tatizo hili kwa suluhisho la muda mfupi, Serikali ijenge line mpya kutoka Mahumbika kwenda Masasi na hii itaondoa tatizo la umeme ule wa Masasi kutumika njiani kabla haujafika Masasi. Lakini halikadhalika watu wa Nanyumbu waunganishwe pia kwenye gridi hiyo, ikiwezekana sasa hivi waunganishwe watu wa Nanyumbu kwenye gridi ya Mtwara, ambayo imeimarika itasaidia kuondokana na hilo tatizo. Lakini, pale Masasi tunacho kifaa ambacho wataalam wanajua tunakiita AVR Automatic Voltage Regulator tunacho pale Masasi. Lakini wakati mwingine pengine hakitusaidii kwa sababu, tayari ule umeme unapofika unakuwa umeshapungua nguvu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaiomba Serikali kifaa hiki AVR, kiwekwe Tunduru na kiwe kifaa kikubwa kisaidie sasa ule umeme wa Tunduru, lakini pamoja na Nanyumbu na Masasi kwa sasa ambao ndio tunatumia uwe ni umeme wa uhakika. Lakini kwa suluhisho la muda mrefu nilikuwa napendekeza pia, kwa sababu Mtwara tunatambua kuna gesi ambayo tayari imeshaanza kutumika. Kwa suluhisho la muda mrefu kwa Wilaya za Masasi na Nanyumbu ni vyema pia, kungejengwa bomba la gesi kutoka Mahumbika kuja Masasi, ambapo pia wanufaika watakuwa Wilaya za Masasi na Wilaya za Nanyumbu na kuendelea kwa sababu bado tutakuwa tunauhitaji huu umeme kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napendekeza hayo kwasababu, tunatambua kwamba kwa sasa, Serikali inafanya jitihada pia ya kutafuta wawekezaji kwa ajili ya kuweka viwanda mbalimbali katika Mkoa wa Mtwara na hasa Masasi pia, kwa ajili ya kuchakata korosho, mabibo na yale mabibo yaliyokauka ambayo tumependekeza kutengenezwe spirit na viwanda vya mafuta ambapo kuna uhaba wa mafuta ya kula. Tunao ufuta na karanga kule, lakini wawekezaji hawa watakwama kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wamechangia kutokana na kukosa umeme wa uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni imani yangu umeme ukiimarika kwa Serikali kuweka hayo masuluhisho ambayo nimeyapendekeza, hiyo changamoto itakuwa imeondoka. Na hivyo wawekezaji watavutika kuja kuwekeza katika Mkoa wa Mtwara katika wilaya zote kwa sababu ya uhakika na hivyo kutakuwa na shughuli za uzalishaji mali na wananchi wataondokana pia na umasikini ambao kwa namna moja au nyingine, wanashindwa kujikwamua kutokana na mazingira ambayo kimsingi Serikali yetu sikivu inaweza kuyatibu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwa sasa tatizo la kukatika kwa umeme lililopo, inapelekea wajasiriamali na wananchi kwa ujumla kuunguza vitu vyao na tunajua sote kwamba, hakuna utaratibu mwananchi mmoja mmoja anapofanya shughuli zake kama labda ana mashine, labda saluni, ama mashine ya kusaga, ama fridge wapo wakinamama wanaotengeneza ice cream, waweze kuuza na shughuli zingine zozote zinazohusisha umeme. Vifaa hivyo vimekuwa vikiungua kwa sababu, umeme unakuja na nguvu kubwa pengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, wananchi wanaathirika kwa hiyo, wanapata hasara kubwa, lakini hata wale wafanyabiashara wanaouza hivyo vifaa vya umeme. Kwa sababu, kama wanapewa warrant ina maana kila siku wakiuza wanatakiwa warudishe ama wafidie, wakiuza wafidie. Kwa hiyo, kwa kiasi kikubwa hiyo imekuwa ni changamoto kubwa kwa wajasiriamali, lakini na kwa wafanyabiashara wa Mkoa wa Mtwara, ambapo ninaamini kabisa, Serikali yangu ya Chama Cha Mapinduzi, inaweza ikalitibu hili tatizo kwa njia hiyo ya muda mfupi lakini pia kwa njia hiyo ya muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaamini kabisa umeme huu utakapokuwa umeimarika hata zile changamoto za Kituo cha Afya kama Nagaga na vingine kule Newala vitakuwa pia ambapo hawapati umeme wa kutosha, Newala, Nanyamba, Mtwara Vijijini, Jimbo la Ndanda, Lulindi ambako kumekuwa na tatizo la umeme usiokuwa wa uhakika basi hiyo changamoto itaondoka. Katika Wilaya ya Masasi pale mjini tunavyo vijiji 19 lakini pia, tuna mitaa kadhaa ambayo haijaunganishwa kabisa haina umeme. Ni imaniā€¦ (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa...

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)